MKUU wa Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, Chelestino Simbalimile Mofuga amempongeza Rais John Magufuli kwa kufanya maendeleo makubwa kwenye uongozi wake wa awamu ya tano mithili ya Rais aliyekaa madarakani kwa muda wa miaka 40.

Akizungumza kwenye uzinduzi wa ujenzi wa jengo jipya la makao makuu ya halmashauri hiyo linalojengwa na Kampuni ya Mzinga Holding Ltd, katika kata ya Dongobesh litakalogharimu kiasi cha shilingi bilioni 4.7 Mofuga alisema Rais Magufuli amewatendea mengi watanzania.

Alisema pamoja na miradi mikubwa ya kimkakati aliyoitekeleza ikiwemo ya ujenzi wa barabara za juu, kununua ndege, elimu bila malipo na mradi mkubwa wa umeme pia amefanikisha miradi ya maendeleo kwenye elimu, afya na maji.

Alisema kwa muda wa miaka minne ya utawala wa awamu ya tano serikali ya awamu ya tano imefanyika maendeleo mengi kwenye kila sehemu hapa nchini huku wilaya ya Mbulu ikiwa na miradi mingi ya maendeleo.

"Tunawashukuru sana viongozi wa dini kwa kumuombea Rais Magufuli kwani maendeleo aliyoyafanya Tanzania utadhani amekaa madarakani kwa muda mrefu wa zaidi ya miaka 40," alisema Mofuga.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo, Hudson Kamoga alimshukuru Rais John Magufuli kwa kuwapatia fedha za ujenzi wa jengo hilo litakalokuwa mfano wa majengo bora mapya ya halmashauri nchini. Kamoga alisema Rais John Magufuli ameipendelea halmashauri ya wilaya ya Mbulu kwani ameiwezesha kufanikisha miradi mingi ya maendeleo.

"Pamoja na jengo jipya la halmashauri ya wilaya litakalogharimu shilingi bilioni 4.7 pia amewezesha ujenzi wa bwawa la umwagiliaji Dongobesh na fedha kwenye idara za afya, elimu na miundombinu," alisema Kamoga.

Mbunge wa jimbo la Mbulu Vijijini, Flatei Maasay alimshukuru Rais Magufuli kwa kufanikisha mradi huo na ujenzi wa hospitali ya Wilaya, kituo cha afya Dongobesh, kwani ndiyo faida ya kuchagua kiongozi anayetekeleza ilani ya uchaguzi.

Massay alisema wanamshukuru Rais Magufuli kwa utekelezaji wa miradi mingi ya maendeleo ya elimu, afya, maji, miundombinu ikiwemo na ujenzi huo ambao utasogeza huduma ya jamii karibu zaidi na wananchi wa jimbo hilo.

Alisema ili mwananchi wa Haydom afike Mbulu mjini makao makuu ya halmashauri hiyo atakwenda kilomita 86 na Dongobesh kilomita 52 hivyo hapo patakuwa karibu zaidi.

Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Mbulu, Joseph Mandoo alisema madiwani wa halmashauri hiyo ndiyo waliamua makao makuu yawe Dongobesh baada ya wataalamu kupendekeza eneo hilo.

Mandoo alisema wataalamu hao waliagizwa na madiwani wafanye utafiti wa kata inayofaa kuwa makao makuu ya halmashauri hiyo nao wakapendekeza kata ya Dongobesh.
 Mkuu wa Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, Chelestino Simbalimile Mofuga akizungumza na wananchi wa kata ya Dongobesh wakati akizindua ujenzi wa jengo la makao makuu ya Halmashauri ya Wilaya hiyo lenye thamani ya shilingi bilioni 4.7.
 Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, Hudson Stanley Kamoga (kushoto) akimuangalia mzee wa Kata ya Dongobesh aliandika historia ya eneo la ujenzi wa jengo jipya la makao makuu ya Halmashauri hiyo.
 Mkuu wa Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, Chelestino Simbalimile Mofuga (watatu kushoto) akichimba kwa sururu wakati azindua ujenzi wa jengo jipya la makao makuu ya halmashauri ya wilaya hiyo lenye thamani ya shilingi bilioni 4.7 kwenye kata ya Dongobesh litakalojengwa na kampuni ya Mzinga Holding Ltd.
Mkuu wa Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, Chelestino Simbalimwile Mofuga (katikati) akizungumza wakati akikagua ramani ya jengo jipya la Halmashauri ya Wilaya hiyo linalojengwa na Kampuni ya Mzinga Holding Ltd kwa gharama ya shilingi bilioni 4.7 katika kata ya Dongobesh, kushoto ni mbunge wa Jimbo la Mbulu Vijijini Flatei Maasay na kulia ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya hiyo Joseph Mandoo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...