*Asema huu si wakati wa kubembelezana na kuambiana maneno matamu
 *Awapa maagizo mazito Waziri Viwanda na Biashara , Kamishna TRA


Na Said Mwishehe, Michuzi TV
RAIS Dk.John Magufuli amesema ataendelea kutengua tu iwapo aliowapa nafasi watashindwa kufanya kazi ambayo anaitarajia na kwamba huu si wakati wa kubembelezana na kuambiana maneno mazuri. 
Amesema Watanzania wanahitaji kuona matokeo mazuri kutoka serikalini na yeye atahakikisha anatimiza kiu hiyo, hivyo ambaye atashindwa hatamuacha abaki huko. pia ametumia nafasi hiyo kueleza kuwa hata ambao amewaapisha leo wakishindwa kutimiza majukumu yao atawaondoa tu. 
Rais Magufuli amesema hayo leo Ikulu jijini Dar es Salaam wakati wa hafla za kuwaapisha Waziri wa Viwanda na Biashara Innocent Bashungwa, Katibu Tawala Mkoa wa Njombe Charles Kichere na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania(TRA). 
"Ujue Watanzania wanataka kuona matokeo. Kuambiana maneno mazuri hakusadii.Sisi tunataka matokeo. Mimi jukumu langu ni kuteua ili kiu ya Watanzania ifanikiwe. 
"Nimpongeze Kakunda(aliyekuwa Waziri wa Viwanda na Biashara) amekuja hapa na huko ndiko kukomaa kisiasa. Hizi kazi ni za muda, maisha yenyewe ni ya muda. Joseph Kakunda amejitoa, amesimama hapa na hiyo ndio sawa. 
"Mimi nataka matokeo  na Watanzania wanataka kuona utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ambayo tumeahidi inatekelezwa. Changamoto za wafanyabishara ni nyingi, kulikuwa na ubaya gani, Waziri wa Viwanda na Biashara, Naibu Waziri na Katibu Mkuu kukutana na wafanyabiashara na kuzungumza nao. Kuna ubaya gani? Nani aliwazuia?Amehoji Rais Magufuli. 
Ameongeza kitendo cha Waziri wa Viwanda na Biashara kutokutana na wafanyabiashara na kutatua matatizo yao ndio maana wanasema hawamjui. "Hata ningemsimamisha Stella Manyanya huenda wangesema hawamjui".

Rais Magufuli ameongeza kuwa, kuna korosho zimekaa tu kwenye maghala , tena wakati zinavunwa hakukua na nchi nyingine iliyokuwa na korosho lakini Wizara ya Viwanda na Biashara ikasubiri hadi nchi nyingine nazo zimevuna korosho na kuingiza sokoni.

"Waziri Bashungwa najua baada ya kukuteau wapo ambao wamekupongeza lakini mimi nakupa pole, maana nikiona mambo hayaendi natakutengua tu. Waziri Kabudi na Mpango wanashindwa kusema ukweli lakini pumbavu nimeshawaambia mara nyingi, inakuja tu licha ya kunizidi umri.

"Tuko kwenye vita haiwezekani tuko kwenye vita halafu tunabembelazana, lazima tuseme ukweli.Katika korosho Wizara ya Kilimo imefanya kazi yake kwa kukusanya korosho tani  223, 000 ambazo zipo kwenye maghala.

"Wametimiza wajibu wao lakini Viwanda na Biashara wamebangua tani 2000, hizi zingine abangue nani? Wizara ya Viwanda na Biashara ndio inayofanya biashara lakini wameshindwa na ilikuwa nitengue kuanzia juu hadi chini.

"Waziri Bashungwa ukienda pale Viwanda na Biashara nenda kafanye kazi.Usimchekee mtu , ni afadhali wakuchikie lakini niliyekuteau ni kusifu.Yale ambayo yapo pale nenda katatue,"amesema Rais Magufuli.

 "Viwanda ambavyo vimeshindwa kufanya kazi sio tu kuviorodhesha bali kavichukue.Kwa mfano kiwanda cha nguo pale Mbeya kinakwenda kubadilishwa kuwa cha Pipi, haiwezekani hii nchi iwe ya kula mapipi."

Kwa upande wa TRA, Rais Magufuli amesema kuwa Dk.Philipo Mpango akiwa Kaimu Kamishna pale  TRA alifanikiwa kukusanya kodi kutoka Sh.bilioni 850  hadi Sh.trilioni 1.3 na ndipo alipoamua kumteua kuwa Waziri wa Fedha. 
"Wengine wote mkienda pale mnabaki kuwa tu hapo hapo mtadhani mmekariri.Aliyekuwa Kamishna wa TRA nimemtumia sms zaidi ya 30 za malalamiko lakini ukifuatilia hakuna matokeo.Dhambi ambayo ninayo siwezi kusahau jambo lazima nifuatilie. 
"Haiwezekani Kamishna kukadiri kodi, anakadiria vibata halafu Kamishna wa TRA upo kimya tu unamuangalia. Haiwezekani kodi ya ndani inashuka halafu unakaa kimya. 
"Kuna wafanyabiashara wanapakia mizigo wakidai inakwenda nje lakini wakifika mpakani wanagonga mhuri na kurudi nchini na TRA iko kila mahali, Kamishna yupo.TRA mnashikilia vifaa vya kuchimba dhahabu, vifaa vimekaa zaidi ya mwaka mzima. 
"Alikuwa anadaiwa sijui Sh.milioni moja wakamuongezea nyingine,Wanashindwa kufahamu kuwa muwekezaji anaweza kuongeza ajira, Siku ile ya wafanyabiashara nakuuliza na wewe(Kichere) halafu na wewe unaangalia mwingine,"amesema Rais Magufuli. 
Amesema ameamua kumteua kuwa Katibu Tawala na huko nako akishindwa nako anamuondoa na huo ndio ukweli. 
"Niliyekuteau kwenda TRA nenda kafanye kazi, najua watasema wamepita wengi na wewe utapita na kuna watu wako TRA wanajifanya hawagusiki, nenda kawaguse., nchi hii bila kodi haiende,"amesema Rais Magufuli. 
Ameongeza kuwa  wanajeshi wanahitaji  mshahara na asipowalipa atawakuta pale Ikulu, atawajibu nini. "Kwa hiyo usicheke na mtu, kuna uwezekano usiende mbinguni lakini Watanzania milioni 50 tutakusuma tu uende mbinguni, nenda kakusanye kodi kwa ajili ya Watanzania, bila kodi hakuna nchi. 
"Kuna wafanyabishara wazuri sana na ukienda watakupa ushirikiano, kuna wafanyabiashara walikuwa wanafoji na mazingira yalikuwa yanaruhusu kufanya hivyo, kaa nao waulize wanaweza kulipa ngapi. 
"Kuna watumishi wanafanya mambo ya hivyo na kusema wametumwa kutoka juu, usikubali kuendelea nao wakifanya mambo ya hovyo timua tu, hakuna ubaya kama unao watumishi 1000 halafu 200 ukawatimua kwa kushindwa kutekeleza majukumu yao,"amesema Rais Magufuli. 
Amemwambia Kamishna mpya wa TRA kuwa anajua siku atapoingia kazini watampelekea maua na hata ambao hawastahili kumuita bosi, watamuita bosi.
"Kwanza jana kuna ujumbe nimekutumia wa malalamiko nadhani umeupata au bado? kuna mipaka ambayo inafanya vizuri, Tunduma na Sirali hawafanyi vizuri , wale makamishna wa vituo hivyo fukuza. 
"Tena mnaowahamisha wengi mnawapeleka kodi , hawa ambao mtakuwa mnawaondoa peleka kwenye Wizara nyingine huko,wapeni hata umesenja wabebe mafaili na hata ofisi yangu ikiwezekana waleteni tu niwabebeshe mafaili,"amesema.


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...