NA SULEIMAN MSUYA

UTAFITI uliofanywa Shirika la Kuhifadhi Misitu ya Asili Tanzania (TFCG), chini ya ufadhili wa Mfuko wa Critical Ecosystem Partnership (CEPF) umebaini kuwa asilimia 89 ya upotevu wa misitu nchini unachangiwa na shughuli za kilimo.

Matokeo ya utafiti huo yametolewa na Mkurugenzi Msaidizi wa TFCG, Emmanuel Lyimo wakati akiwasilisha mada kuhusu sababu zinachangia upotevu wa misitu nchini kwa maofisa kutoka Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Serikali Kuu waliokutana mkoani Morogoro.

Lyimo alisema katika utafiti huo walishirikisha maeneo 120 katika wilaya 62 na mikoa 22 ambapo kila mahali kilimo kilionekana ni sehemu ya sababu kubwa ya upotevu wa misitu.

"Tumetumia miezi sita kuzunguka katika wilaya 62 mikoa 22 na maeneo 120 kuangalia kinachopelekea upotevu wa misitu na tumebaini asilimia 89 hali hiyo inasababishwa na shughuli za kilimo cha kuhamahama," alisema.

Alisema utafiti huo umeonesha uvunaji mkaa, uchomaji moto na ufugaji unachangia upotevu wa misitu kwa asilimia 7, uchomaji moto na ufugaji asilimia 3 na uanzishaji wa mashamba maypa ya miti asilimia 1.

Lyimo alisema utafiti ulibaini zao ambalo linalimwa zaidi katika maeneo ambayo misitu imevunwa ni mahindi, ufuta, kunde, mtama, mpunga, maharage, muhogo, alizeti na korosho.

Alisema iwapo hali hiyo itaendelea bila kuwepo mipango ya kuendeleza sekta ya misitu ni wazi rasilimali hiyo itapotea na kukosekana kwa mbao kwenye vijiji pia kukosekana kwa vyanzo vya maji, uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabia nchi.

"Pia uwezo wa kudhibiti uharibifu utakosekana hasa vijijini hivyo maofisa wanaohusika na usimamizi wa rasilimali misitu wanatakiwa kuongeza juhudi kukabiliana na hali hiyo," alisema.

Lyimo alisema ili maofisa hao kutoka Serikali za mitaa na serikali kuu kuweza  kukabiliana na hali hiyo wanapaswa kuanzisha Usimamizi wa Misitu ya Jamii (CBFM), jamii kunufaika moja kwa moja na rasilimali misitu na kuwepo kwa usawa katika maamuzi kuhusu matumizi ya ardhi kwa kushirisha wadau mbalimbali hasa kilimo, ardhi na misitu.

Kwa upande wake Ofisa Misitu Mkuu Idara ya Misitu na Nyuki Wizara ya Maliasili na Utalii, Seleboni John alisema Serikali imejipanga kikamilifu kusimamia sera ya misitu na sheria ili misitu iwe endelevu.

"Taarifa zinaonesha uharibifu wa misitu umeongezeka kutokana na kilimo, uchomaji mkaa na uvunaji wa mbao kinachohitajika ni wadau kushirikiana kudhibiti kama wanavyofanya TFCG, Mjumita na TaTEDO," alisema.

Mwakilishi wa Wakala wa Misitu Tanzania (TFS), Kanda ya Mashariki, Benadetta Kadala alisema wakala huo umejipanga kulinda misitu kwa kufuata sheria kanuni.Aidha, Kadala alisema TFS itahakikisha misitu ya vijiji inakuwa salama na endelevu kwa kusimamia uvunaji wa sheria.

Ofisa Misitu wa Mkoa wa Morogoro Joseph Chuwa alisema utafiti huo umeonesha hali halisi ya uharibifu hivyo wao kama maofisa misitu, maliasili, kilimo, ardhi na sheria hawana budi kujipanga upya kukabiliana na hali hiyo.

Chuwa alisema iwapo wao wataongeza jitihada ya usimamizi katika kulinda misitu ni dhahiri wafanya maamuzi wataungana nao kwenye kampeni hiyo.
Ofisa Misitu Mkuu wa Idara ya Misitu na Nyuki Wizara ya Maliasili na Utalii, Seleboni John akielezea mikakati ya Wizara hiyo katika kuendeleza misitu kwa maofisa serikali kutoka wilaya mbalimbali katika warsha iliyoandaliwa na Shirika la Uhifadhi Misitu ya Asili Tanzania (TFCG), Mtandao wa Jamii wa Usimamizi Misitu Tanzania (Mjumita) na Shirika la Kuendeleza Nishati ya Asili Tanzania (TaTEDO). Picha na Suleiman Msuya.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...