TAMASHA la 11 la muziki wa Cigogo linaanza kurindima leo kwenye viwanja vya Chamwino Ikulu jijini Dodoma ikiwa ni muendelezo wa kukuza na kuendeleza sanaa ya Tanzania.

Tamasha hilo linaanza leo kwa makundi mbalimbali ya ngoma za asili yakitoa elimu kwa jamii kupitia nyimbo zao huku kesho ndio uzinduzi rasmi ambao, mgeni rasmi atakuwa Naibu Waziri Ofisi ya Rais anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye ulemavu Anthony Mavunde.

Mavunde katika tamasha hilo ataongozana na watendaji wengine wa ofisi za serikali wanaotumikia Sanaa, lengo likiwa ni kufikisha ujumbe wa jamii kupitia wasanii.

Kwa kuwa tamasha la Cigogo ni mojawapo ya sehemu ambayo inabeba urithi wa utamaduni wa mtanzania kwa sababu ya kukusanya idadi kubwa ya wadau wa sanaa, watanzania wanakaribishwa kwa wingi kujipatia ujumbe ambao ni sehemu ya elimu.

Ingawa hivi sasa Tanzania kuna utitiri wa matamasha lakini umuhimu wa tamasha hilo ni wa kupigiwa mfano kutokana na shughuli zinazofanyika kwenye wiki ya tukio hilo.

Kwani mshindo wa tamasha hilo umefika mbali zaidi ambao umevuka mipaka ya nchi na kutokomea katika mabara ya Ulaya, Amerika na Asia ambayo huchota busara na urithi wa sanaa za Tanzania.

Yaliyomo ndani ya tamasha hilo ni kiota ambacho kimebeba dhamira na taratibu nzima za sanaa kwa sababu anayelisimamia tamasha hilo ni mwanazuoni mbobevu anayefanya kazi hizo na kuzifundisha ikiwa ni eneo la elimu, burudani na taratibu nyingine ambazo ni sehemu ya jamii.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa tamasha hilo Dk Kedmon Mapana vumbi limeanza kufuka leo katika viwanja vya Chamwino lilipo lango la kuingilia Ikulu ambalo litafikia tamati Jumapili.

Anasema tamasha hilo lililoasisiwa mwaka 2005 kijijini hapo na Kituo cha Sanaa cha Chamwino (CAC) kwa lengo la kuenzi na kuuendeleza muziki wa asili ya Kigogo.

Dk Mapana anasema ubora wake umezidi kukua kwa sababu ya matukio ambayo yanaendana na kasi ya maendeleo ya sanaa duniani.

Mapana anasema kadri siku zinavyokwenda mbele ndivyo linavyozidi kupiga hatua kwa matukio ambayo ni sehemu ya maendeleo ya sanaa.

“Kwa kuwa sanaa ni eneo ambalo ninaishi, kila mwaka matukio yanabadilika kuendana na wakati, hivyo ni nafasi ya mashabiki wa sanaa na utamaduni kujitokeza kwa wingi kujionea jinsi makundi ya sanaa yanavyoendeleza utamaduni wa mtanzania,” alisema Dk Mapana.

Dk Mapana ambaye ni Mkuu wa kitengo cha Sanaa za Ubunifu Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) anasema kutakuwa na matukio mbalimbali ambayo ni njia ya kufikia malengo yanayokusudiwa.

Anasema katika makundi shiriki huwa wanapewa nafasi ya kuibua vionjo vya asili kama vile aina ya ngoma, uchezaji wake na hata maleba. Makundi shiriki

Anasema tamasha la mwaka huu linatarajia kushirikisha makundi 31 ya hapa nchini ambayo yatabadilishana utamaduni.

Ingawa kutakuwa na wadau zaidi ya 20 kutoka nje ya Tanzania ambao wanakuja kujifunza na kushuhudia utamaduni wa Mtanzania kupitia tamasha hilo.

Anaweka bayana wadau hao kutoka nje ya Tanzania ni Afrika Kusini (4), Bulgaria (4) Amerika (4), Argentina (2) na Thailand (15) na Uganda (1).

Dk. Mapana anasema wafadhili wakubwa wa tamasha la Muziki wa Cigogo ni wasanii wenyewe ambao huwa wanajitoa kwa asilimia kubwa. Tamasha hilo limejijenga kutokuwa tegemezi, yaani hatusubiri wafadhili kuuenzi utamaduni wetu kwani hatusubiri tulipwe pesa.

“Sasa ukionyesha ulichonacho huwezi jua nani atakipenda na atakinunua kwa gharama gani, lakini pia Tamasha hili limejikika katika kufundisha watoto na vijana kuendelea kutambua mila na desturi zao,” alisema.

Kazi kubwa ya Kituo cha Utamaduni Chamwino ni kutafuta fedha ya kuhakikisha wasanii wanakula vizuri.

Anaweka bayana wafadhili wengine wa tamasha hilo ni serikali ya kijiji cha Chamwino ambacho kinatoa maeneo ya kufanyia tamasha hilo bila gharama yoyote pamoja na Shirika lisilo la Kiserikali la Chamwino Connect lililoko Marekani.

Anasema katika makundi shiriki huwa wanapewa nafasi ya kuibua vionjo vya asili kama vile aina ya ngoma, uchezaji wake,na hata maleba.

Kutolewa semina mbalimbali
Mojawapo ya matukio yatakayofanikisha tamasha la 11 ni semina mbalimbali zitakazotolewa na serikali kwa maeneo kama Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), Bodi ya Filamu, Chama cha Hakimiliki Tanzania (COSOTA), Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).

Dk Mapana anasema semina hizo si mara ya kwanza kufanyika tangu kuasisiwa kwa tamasha hilo ambalo linazidi kukua kadri siku zinavyokwenda mbele.

Msanii Dito ndani ya nyumba
Anasema kama ilivyokuwa mwaka jana, msanii wa muziki wa kizazi kipya, Lameck Dito ni mmoja wa wasanii washereheshaji wa tamasha la 11.

Ditto kwenye tamasha hilo akiiwakilisha taasisi ya Tulia Trust ukiwa ni ushirikiano kati ya CAC na taasisi ya Tulia.

Wanafunzi UDSM kujifunza zaidi
Dk Mapana anasema kama ilivyo ada ya tamasha hilo, wanafunzi wa sanaa wa UDSM hupata nafasi ya kujifunza kwa vitendo uandaaji wa Filamu (Film Documentary), namna ya kuandaa matamasha na matukio mengine ya sanaa.

“Huwa tunalitumia tamasha la Chamwino kama sehemu ya wanafunzi wetu kujifunza kwa vitendo yale ambayo tunayowafundisha darasani,” alisema Dk Mapana.

Kubwa zaidi katika tamasha
Dk Mapana anasema katika tamasha la mwaka huu kutakuwa na mchezo wa kuigiza ulioongozwa na wataalam kutoka Bulgaria ambao utachezwa na wanafunzi wa Shule ya Msingi Chamwino.

Anasema malengo makubwa ya mchezo huo ni kuibua na kuendeleza vipaji kwa watoto ukiwa ni mpango wa CAC.
 Katibu Mkuu Wizara ya Habari Sanaa Utamaduni na Michezo, Suzan Mlawi akiwasilisha neno kwenye tamasha la kwa jana, kulia kwake ni Dk Mapana
 Katibu Mkuu Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Suzan Mlawi akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wengine wa sanaa wa kada mbalimbali.
 Katibu Mtendaji wa Basata, Godfrey Mngereza na Dk Mapana wakicheza ngoma na kikundi cha watoto cha Ndagwa
 Katibu wa Basata Godfrey Mngereza akipigamarimba kwenye tamasha la Cigogo 2018
 Kundi la Iman Membe likitoa burudani kwenye tamasha la mwaka jana
Wakiserebuka tamashani

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...