Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akihutubia wakati alipofungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Jumuiya ya Wanafunzi wa Taasisi za Elimu ya Juu (TAHLISO) katika Ukumbi wa Nkrumah uliopo Chuo Kikuu cha Dar es salaam, Agosti 10, 2019. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisoma hati ya kiwanja ambacho kitajengwa Ofisi ya Jumuiya ya Wanafunzi wa Taasisi za Elimu ya Juu Tanzania (TAHLISO) kilichopo eneo la Mtumba jijini Dodoma kilichotolewa na Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Patrobas Katambi (kushoto) Agosti 10, 2019 wakati Waziri Mkuu alipofungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa TAHLISO katika Ukumbi wa Nkuruma uliopo Chuo Kikuu cha Dar es salaam. Kulia ni Waziri wa Elimu, Sayansi na Tekinolojia, Profesa Joyce Ndalichako na wa pili kushoto ni Mwenyekiti wa TAHLISO, Peter Niboye.
Baadhi ya washiriki wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Jumuiya ya Wanafunzi wa Taasisi za Elimu ya Juu (TAHLISO) wakimsikiliza Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wakati alipofungua Mkutano huo katika Ukumbi wa Nkrumah uliopo Chuo Kikuu cha Dar es salaam, Agosti 10, 2019.



Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisalimiana na Waziri wa Elimu, Sayansi na Tekinolojia, Profesa Joyce Ndalichako wakati alipowasili katika Ukumbi wa Nkrumah uliopo Chuo Kikuu cha Dar es salaam kufungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Jumuiya ya Wanafunzi wa Taasisi za Elimu ya Juu Tanzania (TAHLISO), Agosti 10, 2019.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiongozana na Waziri wa Elimu, Sayansi na Tekinolojia, Profesa, Joyce Ndalichako (kulia) na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es salam, Utawala, Profesa David Mfinanga (kushoto) wakati alipoingia katika Ukumbi wa Nkrumah uliopo Chuo Kikuu cha Dar es salaam kufungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Jumuiya ya Wanafunzi wa Taasisi za Elimu ya Juu Tanzania (TAHLISO), Agosti 10, 2019. Wa pili kulia ni Mwenyekiti wa TAHLISO, Peter Niboye

………………

WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa ameutaka uongozi wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) kutafakari namna ya kurekebisha baadhi ya dosari zilizopo likiwemo suala la kuwanyima mikopo wanafunzi kwa kutumia kigezo cha kusoma katika shule binafsi.

Amesema kuna baadhi ya wanafunzi ambao wamefaulu vizuri kidato cha nne na wamekosa nafasi katika shule za Serikali na wanatoka katika familia zisizokuwa na uwezo, hivyo wanatafuta wafadhili ambao wanawasomesha kwenye shule binafsi.

Waziri Mkuu ametoa agizo hilo leo (Jumamosi, Agosti 10, 2019) wakati akifungua mkutano Mkuu wa Mwaka wa Jumuiya ya Wanafunzi wa Taasisi za Elimu ya Juu Tanzania (TAHLISO) kwenye ukumbi wa Nkrumah, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).

Amesema kitendo cha bodi hiyo kuwanyima mikopo baadhi ya wanafunzi kwa kigezo cha kusoma katika shule binafsi bila ya kujiridhisha kama wanatoka kwenye familia zenye uwezo au zisizokuwa na uwezo kinawanyima wanafunzi hao fursa za kuendelea na masomo.

Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwaonya wakuu wa vyuo vikuu ambao wanatumia vibaya fedha za mikopo ya wanafunzi kwa kuzipeleka katika miradi mbalimbali baada ya kuzipokea kutoka HESLB na kuwacheleweshea wanafunzi stahiki yao.

Wakati huo huo, Waziri Mkuu amewaagiza viongozi wa vyuo vikuu kuimarisha mafunzo kwa njia ya vitendo kwani tafiti nyingi zinazohusu mambo ya ajira zimebainisha umuhimu wa mafunzo ya vitendo katika kumuwezesha mhitimu kuwa na uelewa na ujuzi mpana wa kile alichokisoma kwa njia ya nadharia.

“Vyuo viongeze umakini na ufuatiliaji wa karibu wa vijana wetu wanapokuwa kwenye elimu kwa vitendo ili kuhakikisha kwamba wanapata maarifa na ujuzi uliokusudiwa katika mitaala yao. Pia natoa wito kwa waajiri wa sekta ya umma na binafsi watoe ushirikiano wa dhati kwa wanafunzi wanaotafuta nafasi za kufanya mafunzo kwa njia ya vitendo kwenye taasisi zao.” 

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TAHLISO, Bw. Peter Niboye amesema miongoni mwa changamoto zinazowakabili wanafunzi wa elimu ya juu ni ucheleweshwaji wa mikopo kwa baadhi ya vyuo licha ya HESLB kuwasilisha fedha hizo mapema, hivyo ameiomba Serikali kuwasaidia katika kutatua tatizo hilo.

Kadhalika, Mwenyekiti huyo wa TAHLISO, ameishukuru Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli kwa ushirikiano mkubwa inaoipatia jumuiya hiyo hivyo kurahisisha utendaji wake.

Awali, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Bw. Patrobas Katambi alimkabidhi Waziri Mkuu hati ya kiwanja kilichoko katika eneo la Mtumba jijini Dodoma kwa ajili ya ujenzi wa ofisi za TAHLISO, ambapo baada ya kupokea hati hiyo, Waziri Mkuu aliikabidhi kwa Mkwenyekiti wa jumuiya hiyo Bw. Niboye.

Mkutano huo umehudhuriwa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Bw. Paul Makonda, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Bw. Godfrey Chongolo, Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Bw. Kisare Makori pamoja na viongozi kutoka vyuo mbalimbali nchini vinavyounda TAHLISO.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...