Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amemuomba Rais wa Jamhuri ya Afrika Kusini, Mhe. Matamela Cyril Ramaphosa kuwahamasisha zaidi wafanyabiashara wa Afrika Kusini kuja kuwekeza hapa nchini kwa kuwa Tanzania inayo dhamira ya dhati ya kuongeza ushirikiano wake na nchi hiyo katika nyanja mbalimbali za kiuchumi.

Mhe. Rais Magufuli amesema hayo leo tarehe 15 Agosti, 2019 Ikulu Jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na wananchi kupitia vyombo vya habari muda mfupi baada ya kufanya mazungumzo na Mhe. Rais Ramaphosa ambaye amewasili hapa nchini jana jioni kwa Ziara ya Kitaifa ya siku 3 na baadaye kuhudhuria Mkutano wa 39 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) unaofanyika Jijini Dar es Salaam.

Katika mazungumzo hayo yaliyotanguliwa na mapokezi rasmi yaliyofanyika katika viwanja vya Ikulu, Mhe. Rais Magufuli amesema katika kutekeleza mipango yake ya maendeleo na dira ya kufikia uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025 Tanzania inawakaribisha wawekezaji mbalimbali, na kwa kuwa Afrika Kusini imepiga hatua kubwa katika viwanda amewaalika wafanyabiashara wa nchi hiyo kuja kujenga viwanda vya kuzalisha bidhaa mbalimbali zikiwemo dawa na vifaa tiba, kuchakata madini na kwamba Serikali itatoa ushirikiano wowote utakaohitajika.

Mhe. Rais Magufuli pia amemuomba Mhe. Rais Ramaphosa kuongeza ushirikiano na Tanzania katika utalii, hasa ikizingatiwa nchi hiyo inapokea watalii zaidi ya Milioni 10 kwa mwaka ikilinganishwa na Watalii Milioni 1.5 wanaoingia hapa nchini, na katika hilo ametoa wito kwa Afrika Kusini kuongeza safari za treni ya watalii na kwa wawekezaji wake kuja kuwekeza katika hoteli na fukwe za Tanzania.

Kwa upande wa biashara, Mhe. Rais Magufuli amesema Afrika Kusini ni nchi inayoongoza kwa kufanya biashara na Tanzania ikilinganishwa na nchi nyingine za SADC ambapo asilimia 70 ya bidhaa za Tanzania zinazokwenda SADC huenda Afrika Kusini na kwamba biashara kati ya Tanzania na Afrika Kusini imeendelea kukua ambapo katika mwaka 2018 ilikuwa na thamani ya shilingi Trilioni 2 na Bilioni 687 ikilinganishwa na mwaka 2017 ilipokuwa na thamani ya shilingi Trilioni 2 na Bilioni 528.

Amempongeza Mhe. Rais Ramaphosa kwa kuja na wafanyabiashara ambao wanajadiliana na wafanyabiashara wa Tanzania juu ya kushirikiana kibiashara, na amemhakikishia kuwa Tanzania itakuwa tayari kuhakikisha ushirikiano huo unafanikiwa.

“Sisi Tanzania tumeamua kuwa tunanunua bidhaa zetu Afrika Kusini badala ya kununua bidhaa hizo huko mbali, na kwa kuanzia pikipiki za kuongozea misafara ya viongozi tutakazotumia wakati huu wa Mkutano wa 39 wa SADC tumenunua Afrika Kusini” amesisitiza Mhe. Rais Magufuli.

Kwa upande wake Mhe. Rais Ramaphosa amemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa kumwalika kufanya Ziara ya Kitaifa hapa nchini na amemhakikishia kuwa wananchi Afrika Kusini wanaiona Tanzania ni nyumbani kwao na hivyo Serikali yake ipo tayari kuuendeleza na kuukuza uhusiano mzuri kati yake na Tanzania.

Mhe. Rais Ramaphosa ameelezea kufurahishwa kwake na kuwepo kwa kampuni 228 za Afrika Kusini zilizowekeza nchini Tanzania na kuajiri wa zaidi ya watu 21,000 na ameahidi kwenda kuwahimiza zaidi wafanyabiashara na wawekezaji wa Afrika Kusini kuja kuwekeza nchini Tanzania huku akiwakaribisha wawekezaji wa Tanzania kwenda kuwekeza Afrika Kusini.

Ameipongeza Tanzania kwa kuzalisha mazao mengi ya chakula na ameahidi kuwa Afrika Kusini itaendelea kununua mazao kutoka Tanzania.Aidha, Mhe. Rais Ramaphosa amesema Afrika Kusini ipo tayari kushirikiana na Tanzania katika nyanja nyingine mbalimbali zikiwemo afya, ulinzi na usalama, utalii na amekubaliana na mapendekezo ya Tanzania juu ya mpango wa kufundisha lugha ya Kiswahili nchini Afrika Kusini hasa wakati huu ambapo SADC inatarajia kuifanya kuwa lugha rasmi ya 4.
Katika ziara hii, Mhe. Rais Ramaphosa ameongozana na Mkewe Mhe. Dkt. Tshepo Motsepe ambaye wakati wa mazungumzo rasmi ya Waheshimiwa Marais amekuwa na mazungumzo na Mke wa Rais wa Tanzania Mhe. Mama Janeth Magufuli.
  
Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
15 Agosti, 2019

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...