Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amemuomba
Rais wa Jamhuri ya Afrika Kusini, Mhe. Matamela Cyril Ramaphosa kuwahamasisha
zaidi wafanyabiashara wa Afrika Kusini kuja kuwekeza hapa nchini kwa kuwa
Tanzania inayo dhamira ya dhati ya kuongeza ushirikiano wake na nchi hiyo
katika nyanja mbalimbali za kiuchumi.
Mhe.
Rais Magufuli amesema hayo leo tarehe 15 Agosti, 2019 Ikulu Jijini Dar es
Salaam wakati akizungumza na wananchi kupitia vyombo vya habari muda mfupi
baada ya kufanya mazungumzo na Mhe. Rais Ramaphosa ambaye amewasili hapa nchini
jana jioni kwa Ziara ya Kitaifa ya siku 3 na baadaye kuhudhuria Mkutano wa 39 wa
Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) unaofanyika
Jijini Dar es Salaam.
Katika
mazungumzo hayo yaliyotanguliwa na mapokezi rasmi yaliyofanyika katika viwanja
vya Ikulu, Mhe. Rais Magufuli amesema katika kutekeleza mipango yake ya
maendeleo na dira ya kufikia uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025 Tanzania
inawakaribisha wawekezaji mbalimbali, na kwa kuwa Afrika Kusini imepiga hatua
kubwa katika viwanda amewaalika wafanyabiashara wa nchi hiyo kuja kujenga
viwanda vya kuzalisha bidhaa mbalimbali zikiwemo dawa na vifaa tiba, kuchakata
madini na kwamba Serikali itatoa ushirikiano wowote utakaohitajika.
Mhe.
Rais Magufuli pia amemuomba Mhe. Rais Ramaphosa kuongeza ushirikiano na
Tanzania katika utalii, hasa ikizingatiwa nchi hiyo inapokea watalii zaidi ya
Milioni 10 kwa mwaka ikilinganishwa na Watalii Milioni 1.5 wanaoingia hapa
nchini, na katika hilo ametoa wito kwa Afrika Kusini kuongeza safari za treni
ya watalii na kwa wawekezaji wake kuja kuwekeza katika hoteli na fukwe za
Tanzania.
Kwa
upande wa biashara, Mhe. Rais Magufuli amesema Afrika Kusini ni nchi
inayoongoza kwa kufanya biashara na Tanzania ikilinganishwa na nchi nyingine za
SADC ambapo asilimia 70 ya bidhaa za Tanzania zinazokwenda SADC huenda Afrika
Kusini na kwamba biashara kati ya Tanzania na Afrika Kusini imeendelea kukua
ambapo katika mwaka 2018 ilikuwa na thamani ya shilingi Trilioni 2 na Bilioni
687 ikilinganishwa na mwaka 2017 ilipokuwa na thamani ya shilingi Trilioni 2 na
Bilioni 528.
Amempongeza
Mhe. Rais Ramaphosa kwa kuja na wafanyabiashara ambao wanajadiliana na
wafanyabiashara wa Tanzania juu ya kushirikiana kibiashara, na amemhakikishia
kuwa Tanzania itakuwa tayari kuhakikisha ushirikiano huo unafanikiwa.
“Sisi
Tanzania tumeamua kuwa tunanunua bidhaa zetu Afrika Kusini badala ya kununua
bidhaa hizo huko mbali, na kwa kuanzia pikipiki za kuongozea misafara ya
viongozi tutakazotumia wakati huu wa Mkutano wa 39 wa SADC tumenunua Afrika
Kusini” amesisitiza Mhe. Rais Magufuli.
Kwa
upande wake Mhe. Rais Ramaphosa amemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa kumwalika
kufanya Ziara ya Kitaifa hapa nchini na amemhakikishia kuwa wananchi Afrika
Kusini wanaiona Tanzania ni nyumbani kwao na hivyo Serikali yake ipo tayari
kuuendeleza na kuukuza uhusiano mzuri kati yake na Tanzania.
Mhe.
Rais Ramaphosa ameelezea kufurahishwa kwake na kuwepo kwa kampuni 228 za Afrika
Kusini zilizowekeza nchini Tanzania na kuajiri wa zaidi ya watu 21,000 na
ameahidi kwenda kuwahimiza zaidi wafanyabiashara na wawekezaji wa Afrika Kusini
kuja kuwekeza nchini Tanzania huku akiwakaribisha wawekezaji wa Tanzania kwenda
kuwekeza Afrika Kusini.
Ameipongeza
Tanzania kwa kuzalisha mazao mengi ya chakula na ameahidi kuwa Afrika Kusini
itaendelea kununua mazao kutoka Tanzania.Aidha,
Mhe. Rais Ramaphosa amesema Afrika Kusini ipo tayari kushirikiana na Tanzania
katika nyanja nyingine mbalimbali zikiwemo afya, ulinzi na usalama, utalii na
amekubaliana na mapendekezo ya Tanzania juu ya mpango wa kufundisha lugha ya
Kiswahili nchini Afrika Kusini hasa wakati huu ambapo SADC inatarajia kuifanya
kuwa lugha rasmi ya 4.
Katika
ziara hii, Mhe. Rais Ramaphosa ameongozana na Mkewe Mhe. Dkt. Tshepo Motsepe
ambaye wakati wa mazungumzo rasmi ya Waheshimiwa Marais amekuwa na mazungumzo
na Mke wa Rais wa Tanzania Mhe. Mama Janeth Magufuli.
Gerson
Msigwa
Mkurugenzi
wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar
es Salaam
15
Agosti, 2019
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...