KESHO KUTOA UAMUZI WA KUFUTA AU KUTOFUTA DHAMANA 

Na Karama Kenyunko, Globu ya Jami.


MAHAKAMA ya ya Hakimu Mkazi Kisutu kesho Novemba 20, mwaka 2019  inatarajia kutoa uamuzi wa kufuta au kutofuta dhamana ya  wabunge wanne wa Chadema  baada ya kukiuka masharti ya dhamana.

Wabunge hao ni Mbunge wa Tarime Vijijini John Heche, Mbunge wa Iringa Mjini Peter Msigwa,  Mbunge wa Kawe Halima Mdee na Mbunge wa Bunda Mjini Ester Bulaya ambao wamefika mahakamani hapo leo wakitokea katika kituo cha polisi  Osterbay jijini Dar es Salaam baada ya kujisalimisha kutokana na amri ya Mahakama ya kuamuru wakamatwe.

Hatua hiyo ya Mahakama imekuja bàada ya washtakiwa hao wote wanne kutoa sababu zao mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Thomas Simba zilizowafanya kushindwa kufika mahakamani hapo Novemba 15, saa tatu asubuhi kama Mahakama ilivyokuwa imepanga.

Wakitoa sababu kwa nini wasifutiwe dhamana, washtakiwa Heche, Msigwa na Mdee waliieleza Mahakama kuwa siku hiyo ya kesi walifika mahakamani hapo kwa kuchelewa kutokana na sababu mbali mbali.

Mshtakiwa  Msigwa na Heche walidai kuwa walipata ajali wakiwa njiani kufika mahakamani hapo huku Mdee yeye alidai aliugua ghafla akiwa njiani na kumlazimu kupitia Hospitali kitendo kilichopelekea wote kufika mahakamani kwa kuchelewa.

Kwa upande wake, mshtakiwa Ester Bulaya alidai kuwa  hakufika  mahakamani siku hiyo kwa kuwa alifiwa na mama yake Mdogo hivyo alikwenda Singida kwa ajili ya Maziko.

"Wakati kesi inaendelea siku ya mwisho nilijaribu kunyoosha mkono lakini haukuniona Hakimu,  mimi ni Mjumbe wa kamati ya Bunge ambapo baada ya kesi, nilikimbia  kwenda Dodoma alhamisi kwenye kikao ambacho kiliisha saa moja na nusu usiku niliondoka saa mbili na nusu usiku na kuingia Dar es Salaam saa mbili asubuhi. Kwenye akili yangu nilijua kesi ni saa nne na nusu hivyo sikuwa na wasiwasi kama nitachelewa lakini wakati nikiwa njiani kuja mahakamani nikiwa na Heche, tulipata ajali", amesema Msigwa.

"Mheshimiwa ninaheshimu Mahakama na siwezi kuidharau mahakama wala wewe binafsi,
Naomba Mahakama isinifutie dhamana yangu," alisema Msigwa.

Kwa upande wake Mdee ameiomba Mahakama isimfutie dhamana yake kwani anaiheshimu sana mahakamai ila siku hiyo wakati anakuja mahakamani aliugua ghafla akapitia Hosp lakini kwa kihofia kuchelewa alimpigia mdhamini wake ambae nae alifika kwa kuchelewa.

"Mimi ninakaa karibu kilometa 1600 kutoka hapa, hapa mjini sina familia wala mke, ila tangia kianza kwa kesi hii sijawahi kuchelewa mahakamani wala kuonywa, ila siku ya kesi tukiwa njianj na Msigwa, gari iligongwa, ikabidi tutafute pa kuiweka na kisha tukachukua boda boda lakini tulipofika mahakamani tukakutana na wenzetu ndio wanatoka" amesema Heche.

Wakati  Bulaya amesema, hawezi kuidharau mahakama, ila alifikwa na msiba wa mama yake mdogo huko Singida, hivyo aliwataarifu wadhamini wake ili siku ya kesi wafike, lakini nao walipofika walikuwa wamechelewa na kukuta kesi imeahirishwa.

Hata hivyo upande wa mashtaka kupitia wakili wa Serikali Salimu Msemo akiwasilisha hoja ya kutaka washtakiwa wafutiwe dhamana amedai, ni muhimu suala muda wa kuwepo mahakamani kuzingatiwa na ni dhahiri kuwa washtakiwa hawakuwepo mahakamani wakati kesi hiyo inaahirishwa.

Hivyo ninaiomba mahakama iwafutie dhamana washtakiwa hao wanne na kuwachukulia hatia stahiki wadhamini wao.Akijibu hoja hizo, Wakili wa utetezi Peter Kibatala amedai, hakuna sababu za kimazingira wala kisheria za kufuta dhamana, uamuzi wa kutoa dhamana ni mwepesi zaidi kuliko uamuzi wa kuifuta.

Hakuna ubishi kwamba wakati wa kesi hii washtakiwa walikuwa na rekodi bzuri ya kuhudhuria mahakamani na kwamba washtakiwa walitoa maelezo siku hiyo walikuja mahakamani.

Ni kweli kwamba kawaida kesi za jinai zinaanza saa tatu asubuhi lakini tangu waanze shauri hili awajawahi kuanza muda huo bali wamekuwa wakianza saa 4:30 asubuhi na kuendelea na kuongeza kuwa kuchelewa mahakamani sio na kutofika.

Mahakama sio mashine kwakuwa zipo sababu za kibinadamu na ndio maana kuna mahakimu au majaji wanaofanya maamuzi na kutafsiri sheria.

Wabunge watatu wa CHADEMA wanashikiliwa na Jeshi la Polisi baada ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kutoa amri ya wabunge wa 4 wa chama hicho wakamatwe kwa kukiuka masharti ya dhamana.

Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni,  Mwenyekiti wa Chadema Freeman Mbowe,  Naibu Katibu Mkuu Zanzibar Salum Mwalimu,  Naibu katibu Mkuu bara na Mbunge wa kibamba John Mnyika, katibu Mkuu wa Chama hicho, Dk Vincent Mashinji na Mbunge wa Tarime mjini Ester Matiko.

Katika Kesi hiyo Mbowe na wenzake wanakabiliwa na  mashtaka 13, ikiwemo kula njama,  kufanya mkusanyiko wenye ghasia na kuhamasisha hisia za chuki.

Pia, wanadaiwa kushawishi hali ya kutoridhika, uchochezi wa makosa yanayodaiwa kutendeka kati ya Februari 1 na 16, 2018, jijini Dar es Salaam. Hata hivyo watuhumiwa hao wanne wamepelekwa mahabusu hadi kesho uamuzi utakapotolewa.

Hata hivyo, pia Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe ameshindwa kufika mahakamani kwa sababu anaumwa na amelazwa katika Hospitali ya Aghakhan chumba 507. Taarifa ya kuumwa kwa Mbowe, imetolewa mahakamani hapo na Mdhamini wake, Grayson Selestine.






Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 1 mpaka sasa

  1. Naomba serikali iweze kuwalipa fidia wakazi wa Kifuru na Kibaga fidia kutokana na ujenzi wa umeme mkubwa utakatumika na reli ya kisasa ya SGR kwani mpaka sasa tingatinga liko site likiendelea kuchimba mitaro ya kusimika nguzo za umeme huo licha ya wananchi kutolipwa fidia.

    Naomba serikali iingilie kati suala hili maana ni mwaka sasa tangu tathmini ifanywe

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...