Jaji
Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akimkabidhi Mkuu wa
Wilaya ya Nkasi, Said Mohamed Mtanda kitabu kinachoonyesha Mpango wa
ujenzi wa majengo ya Mahakama ya Tanzania alipofika ofisini kwake
kumtembelea akiwa katika ziara ya kikazi mkoa wa Rukwa.
Jaji
Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim
Hamis Juma akiwa katika picha ya pamoja na kamati ya ulinzi na usalama
ya wilaya ya Nkasi alipomtembelea Mkuu wa wilaya hiyo ofisini kwake
akiwa katika ziara ya
kikazi mkoa wa Rukwa.
Watumishi wa Mahakama ya wilaya ya Nkasi wakimsikiliza Jaji Mkuu.
Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim
Hamis Juma akiwa katika picha ya pamoja na wananchi wa wilaya ya Nkasi waliofika Mahakamani kupata huduma za kimahakama.
Na
Lydia Churi-Mahakama Rukwa
Jaji Mkuu wa Tanzania
Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewataka Mahakimu nchini kuanza kuzipitia Sheria
na kanuni zinazohusu uchaguzi ili kujiandaa kusikiliza kesi za uchaguzi.
Akizungumza na
Watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Nkasi wakiwemo Mahakimu, Jaji Mkuu amewataka
Mahakimu kuanza kujiandaa kusikiliza kesi za uchaguzi kwa kuwa mwaka huu nchi
itafanya uchaguzi wa Serikali za mitaana baadaye mwakani uchaguzi mkuu.
Aidha, Jaji Mkuu pia
ameagiza Mahakimu kutochelewesha kesi za uchaguzi kwani alisema kwa kufanya
hivyo wataweza kuiingiza Mahakama kwenye migogoro. Aliongeza kuwa endapo kesi
hizo zitasikilizwa kwa mujibu wa sheria na kumalizika kwa wakati zitasaidia kuifanya
Mahakama kuendelea kuaminiwa zaidi na wananchi.
Alisema endapo Mahakimu
watazipitia sheria na kujiandaa vema kusilikilza kesi hizo kni wazi kuwa
hawatababaishwa mahakamani. “Hakimu anayefahamu sheria na taratibu hawezi
kubabaishwa awapo Mahakamani”, alisema Jaji Mkuu.
Jaji Mkuu pia amewataka
Mahakimu kutojihusisha na masuala ya siasa ili waweze kuwa huru katika kutatua
migogoro mbalimbali itakayoletwa kwao. Alifafanua kuwa Sheria inamkataza Jaji,
Msajili, na Hakimu kujiunga na chama chochote cha siasa ili waweze kutatua
migogoro inayoletwa kwao.
Awali akizungumza na
Mkuu wa wilaya ya Nkasi, Said Mohamed Mtanda, Jaji Mkuu amesema Mahakama ya
Tanzania inao mpango wa kuwa na mahakama za Mwanzo za kisasa kwenye kwenye kila
tarafa kwa nchi nzima ili kusogeza huduma zake karibu zaidi na wananchi.
“Tutahakikisha
tunajenga Majengo ya kisasa ili endapo tarafa husika itakuwa wilaya basi
majengo hayo yawe na hadhi ya kuwa Mahakama za wilaya”, alisema Jaji Mkuu. Alisema
Mahakama itaiomba Serikali Kuu kupeleka fedha za ujenzi wa majengo hayo kwenye
halmashauri ili halmashauri zijenge.
“Sisi tutatoa ramani za majengo, tutatafuta na
fedha ili halmashauri zijenge kwa kuwa tayari zinao uzoefu katika kujenga vituo
vya afya hivyo na jukumu la kujenga Mahakama za Mwanzo mlibebe.”
Awali akizungumza na
Mkuu wa wilaya ya Nkasi, Said Mohamed Mtanda alipomtembelea ofisini kwake,
Prof. Juma alihimiza ushirikiano wa Mahakama na mihimili mingine kwa kuwa Katiba
ya nchi pia inatambua na imegawa majukumu kwa kila mhimili ambapo mihimili yote
humtumikia mwananchi.
Naye Mkuu wa wilaya ya
Nkasi, Said Mohamed Mtanda amesema Serikali wilayani humo itashirikiana na
Mahakama ya Tanzania kwa karibu ili kuhakikisha wananchi wa wilaya hiyo
wanapata huduma zote muhimu zikiwezo huduma za mahakama.
Jaji Mkuu anaendelea na
ziara yake ya kikazi katika mkoa wa Rukwa ambapo leo alitembelea Mahakama za
wilaya ya Nkasi na Namtumbo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...