Benki Kuu ya Tanzania (BOT) imeipongeza benki ya Exim Tanzania kwa jitihada na mafanikio inayoyapata katika kujitanua ndani na nje ya nchi huku ikitoa wito kwa benki hiyo kuhakikisha inawekeza zaidi katika kutoa huduma maalumu na zenye ubunifu kwa wafanyabiashara wadogo na wa kati ili waongeze nguvu katika kuleta mabadiliko ya kiuchumi nchini.

Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam na Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT) Dk Bernard Kibesse wakati akifungua rasmi tawi jipya la benki ya Exim Tanzania lililopo katika mtaa wa Mkwepu jijini Dar es salaam ikiwa ni baada ya benki hiyo kukamilisha taratibu za umiliki wa iliyokuwa Benki ya UBL Tanzania. Katika uzinduzi huo, Dk Kibesse alimuwakilisha Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango.

“Ni fahari kwetu kuona benki ya kizalendo inafanya mambo makubwa kama haya. Mmekuwa mfano mzuri wa kuigwa kwa mabenki hapa nchini jinsi inavyojizatiti kujiimarisha ndani na nje ya mipaka ya nchi.Hatua hii ni sawa na kuitikia kilio cha wadau wa huduma za kifedha hapa nchini wanaohitaji huduma zinazokidhi mahitaji yao pia huduma zinazolingana na zile za kimataifa na kwenye mazingira yaliyobereshwa.’’ Alisema.

Alitoa wito kwa benki hiyo kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo wafanyabiashara wadogo na wa kati ili waweze kuongeza nguvu katika kuleta mabadiliko ya kiuchumi nchini ili kulisaidia taifa kufikia malengo yake ambayo ni pamoja na kufikia pato la kati ifikapo mwaka 2025.

Awali akizungumza kwenye hafla hiyo, Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Exim Tanzania Bw Jaffari Matundu alisema hatua hiyo inakwenda sambamba na msimamo wa Rais Dk John Magufuli ambae amekuwa akisisitiza juu ya umuhimu wa kuwa na benki kubwa zaidi na ndogo nchini kwa kuwa ni hatua muhimu kwa afya ya kifedha katika ukuaji wa uchumi hususani katika kutoa huduma kamili na zenye ubunifu kwa wateja.

“Aidha ufunguzi wa matawi mapya kama hili utasaidia kuimarisha uwepo wa Benki ya Exim kiushindani katika maeneo mbalimbali ili kutoa kwa urahisi huduma zetu kwa wakazi na wamiliki wa biashara wa maeneo haya’’

"Tunafurahi kuwakaribisha wateja wa Benki ya UBL, wafanyakazi na jamii yote ya UBL kwenye familia ya Benki ya Exim. Hatua hii si tu inaongeza uwepo wetu kwenye soko kubwa bali pia inatuongezea timu kubwa ya wafanyakazi wenye weledi katika masuala ya kibenki,’’ alisema.

Alisema Dar es salaam ni soko muhimu kwa Benki ya Exim na tawi hilo jipya la Mkwepu limeambatana na matumzi ya teknolojia mpya na muundo ambao utawasaidia wateja wa benki hiyo kuwasiliana na maafisa wa benki hiyo kwa njia inayowafaa na katika mazingira ambayo ni bora na salama zaidi.

Akielezea mpango wa benki hiyo Bwana Matundu alisema kuwa wanalenga kutoa kasi ya juu katika suala la utoaji huduma ili kuhakikisha kuwa wateja wanapata huduma haraka na zisizo na usumbufu kwa kuzingatia mahitaji ya wateja na hali ya soko.

Ikiwa na jumla ya matawi 33 kwasasa Benki ya Exim Tanzania ni moja wapo ya benki kubwa nchini. Katika kipindi kifupi cha zaidi ya miaka 22 ya uwepo wake benki hiyo imetoa huduma za kifedha kwa wateja wa wadogo, wa kati na wakubwa.
Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT) Dk Bernard Kibesse (Kulia) akipongeza na Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Exim Tanzania Bw Jaffari Matundu (Kushoto) wakati akifungua rasmi tawi jipya la benki ya Exim Tanzania lililopo katika mtaa wa Mkwepu jijini Dar es salaam baada ya benki hiyo kukamilisha taratibu za umiliki wa iliyokuwa Benki ya UBL Tanzania.


Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT) Dk Bernard Kibesse (Kulia) akijipongeza na Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Exim Tanzania Bw Jaffari Matundu (Kushoto) wakati akifungua rasmi tawi jipya la benki ya Exim Tanzania lililopo katika mtaa wa Mkwepu jijini Dar es salaam baada ya benki hiyo kukamilisha taratibu za umiliki wa iliyokuwa Benki ya UBL Tanzania. Wengine ni pamoja na maafisa waandamizi wa benki hiyo, wateja na wageni waalikwa.

Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT) Dk Bernard Kibesse akzungumza wakati wa hafla hiyo.
Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Exim Tanzania Bw Jaffari Matundu (katikati) akizungumza wakati wa hafla hiyo.
Mkuu wa Huduma ya Rejareja wa benki ya Exim, Bw. Andrew Lyimo akizungumza kwenye hafla hiyo.
Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT) Dk Bernard Kibesse (wa nne kulia) pamoja na na Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Exim Tanzania Bw Jaffari Matundu (katikati) wakiwa kwenye picha ya pamoja na maafisa waandamizi wa benki ya Exim, wateja na wageni waalikwa wakati wa hafla hiyo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...