Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Manunuzi cha Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Josephat Msafiri (wa pili kulia) akiandika mambo mbalimbali yanayofundishwa na Mwezeshaji Kenneth Nnembuka kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA), katika mafunzo ya mfumo wa manunuzi kwa njia ya mtandao (TANePs), yanayoendelea kwenye ukumbi wa Mikutano wa Watu Mashuhuri wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (VIP -JNIA-TB2).
Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani cha Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Irene Sikumbili (wa tano kulia) akimsikiliza mwendeshaji wa mafunzo ya mfumo wa manunuzi kwa njia ya Mtandao (TANePs), yanayoendeshwa na Kenneth Nnembuka kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA). Mafunzo hayo yanafanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa Watu Mashuhuri wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Juluius Nyerere (JNIA_VIP).
Washiriki wa mafunzo ya siku tano ya Mfumo wa Manunuzi kwa njia ya Mtandao (TANePs) kutoka Makao Makuu ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) na wa Kiwanja cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), wakifuatilia kwa makini mafunzo hayo yanayofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa Watu Mashuhuri wa JNIA.
Kaimu Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), akimkabidhi cheti cha kufuzu mafunzo ya mfumo wa Manunuzi kwa njia ya Mtandao (TANEPs), Mkuu wa Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani wa Bi. Irene Sikumbili (wa pili kushoto). Mafunzo hayo yaliendeshwa na Mwezeshaji Kenneth Nnembuka kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA) (kulia)

Afisa Manunuzi na Ugavi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Honest Mushi (mwenye fulana) akipokea cheti cha kufuzu mafunzo ya mfumo wa Manunuzi kwa njia ya Mtandao (TANEPs), kutoka kwa Kaimu Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Bw. Abdul Mkwizu. Kulia ni Mwezeshaji wa Mafunzo hayo Bw. Kenneth Nnembuka kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA)
……………………………..

Na Bahati Mollel, TAA

KAIMU Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Abdi Mkwizu amewataka wahitimu wa mafunzo ya mfumo wa Manunuzi kwa njia ya mtandao (TANEPs), kuutumia vyema mfumo huo ili kuongeza ufanisi katika taratibu za ununuzi wa Umma kwa maslahi ya taasisi na Taifa kwa ujumla.

Akifunga mafunzo hayo ya siku tano jana yaliyokuwa yakifanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Watu Mashuhuri wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Bw. Mkwizu alisema tayari Mamlaka imeanza kutumia mfumo huu ulioagizwa na serikali kupitia Mamlaka ya udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA).

Mkufunzi wa mafunzo hayo Bw. Kenneth Nnembuka kutoka PPRA, aliwataka wahitimu kuanza haraka kutumia maarifa waliyoyapata ili wasije wakasahau. Pia aliwasihi kutosita kuomba msaada mara wapatapo mkwamo kuhusu mfumo huu mpya.

Naye Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Manunuzi na Ugavi cha TAA, Bw. Josephat Msafiri alishukuru uongozi wa juu wa TAA kukubali kufanyika kwa mafunzo hayo muhimu wenye lengo la kuongeza ufanisi wa utendaji wa ndani wa taasisi. Aliahidi kuendelea kutumika bila kuharibu kada hiyo.

Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Ukaguzi wa ndani ya Taasisi, Bi Irene Sikumbili aliweka msisitizo kwenye matumizi sahihi ya mfumo kwa mujibu wa miongozo, taratibu, kanuni na sheria za serikali.

Naye, Mkurugenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Bw. Paul Rwegasha, alisisitiza mapendekezo ya TAA na wadau mbalimbali kuhusu changamoto za kimfumo yafanyiwe kazi ili kuepusha uwezekano wa ukwamishaji wa huduma viwanjani.

Mratibu wa mafunzo hayo, Bw. Soud Saad naye amesema mafunzo hayo yalishirikisha watendaji wakuu wa TAA; Wakaguzi wa ndani; wataalam wa TEHAMA na Wataalam wa Ununuzi na Ugavi kutoka Makao Makuu na JNIA.

Alisema mfumo huo unafaida kubwa kwa taasisi na serikali kwa ujumla, ambapo unaongeza uwazi katika masuala ya zabuni na kupunguza dhana ya upendeleo; kuongeza ushindani na kupata washindi bora; pia tutapata bidhaa bora kwa gharama nafuu na halisi ya soko.

Pia kuongeza uwazi katika utendaji kazi kwa kuwa zabuni zinanunuliwa na kufunguliwa kwa njia ya mtandao, ambapo awali kulikuwa na shida ya utunzaji wa kumbukumbu, ila sasa kila kitu kinabaki katika mfumo na kusaidia kupata taarifa katika suala zima la ukaguzi; kuepuka gharama za matangazo katika magazeti na sasa inatangazwa moja kwa moja kwenye mtandao.

“Mfumo unaleta urahisi (flexibility) utaokoa muda kwani utendaji na ufuatiliaji wa michakato unafanyika popote pale ili mradi mtu awe na simu ya janja au komputa mpakato,” alisema.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...