Veronica Simba – Kagera
Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani amesema Serikali imedhamiria kupeleka umeme wa gridi ya Taifa katika Mkoa wote wa Kagera, awamu kwa awamu ikianza na Wilaya za Bukoba Vijijini, Muleba na Misenyi.

Amesema Wilaya hizo za awali zitaungwa kwenye gridi ya Taifa ndani ya kipindi cha mwezi mmoja kutoka sasa.

Waziri ameeleza hayo Februari 27 mwaka huu wakati akizungumza na Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Brigedia Generali Marco Gaguti, akiwa katika ziara ya kazi.

“Wataalamu wetu kutoka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), wataanza kujenga njia ya kusafirisha umeme wa kilovoti 33 kutoka Kanazi mpaka Itako na kutoka Itako mpaka Misenyi,” amefafanua.

Akieleza zaidi, amesema maeneo hayo yataanza kutumia umeme wa gridi ya Taifa inayotoka Geita mpaka maeneo ya Ngara, Biharamulo na baadaye Misenyi.

Hata hivyo, Waziri amesema maeneo ambayo hayatafikiwa katika awamu ya kwanza kikiwemo kiwanda cha sukari cha Kagera na mengine yote yatakayosalia, yataendelea kutumia umeme kutoka nchi jirani ya Uganda wakati wakisubiri awamu nyingine ya utekelezaji wa mpango huo.

Akielezea kuhusu kuyaunga maeneo hayo yatakayosalia, Waziri amesema zoezi hilo litafanyika baada tu ya kukamilika kwa miradi mikubwa ya umeme ya Kakono, Rusumo na Nyakanazi.

“Miradi hiyo ikikamilika, taratibu tutaweza kuwaondoa wale waliosalia kutoka kwenye gridi ya Taifa upande wa Uganda na kuwaunga kwenye gridi ya Taifa ya hapa nchini.”

Aidha, Waziri amebainisha kuwa, utekelezaji wa mpango huo ni sehemu ya mkakati wa serikali unaoendelea ukilenga kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika katika maeneo yote ya nchi yetu.

Ameeleza zaidi kuwa, mbali ya kuimarisha hali ya upatikanji umeme nchini, serikali pia inapanga kuwa na umeme mwingi utakaotosheleza mahitaji ya ndani na kuuza ziada kwa nchi jirani za Ukanda wa Afrika Mashariki.

“Leo sisi tunanunua umeme kutoka kwa jirani zetu. Tunataka nasi tuwauzie umeme hapo baadaye. Uhakika wa kufanya hivyo tunao kutokana na miradi mikubwa tunayoitekeleza ukiwemo ule wa kuzalisha umeme (megawati 2,115) wa Julius Nyerere huko Rufiji.”

Kwa upande wake, Brigedia Gaguti amepongeza uamuzi huo wa serikali kuunganisha umeme wa gridi ya Taifa katika Mkoa wote wa Kagera na kuahidi kutoa ushirikiano kadri utakavyohitajika katika kuhakikisha mradi huo unatekelezwa kikamilifu.

Katika ziara hiyo ya siku moja, Waziri na Ujumbe wake walitembelea maeneo mbalimbali ambayo yatahusika katika utekelezaji wa Mradi huo kikiwemo kituo cha kupoza umeme cha Kyaka kilichopo wilayani Misenyi.
 Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani (aliyeinua mkono), akitoa maelekezo mbalimbali kwa uongozi wa TANESCO, yanayohusu kuboresha huduma ya upatikanaji umeme kwa wananchi, alipotembelea Kituo cha kupoza umeme Kyaka, kilichopo wilayani Misenyi, Mkoa wa Kagera, Februari 27 mwaka huu. Wa kwanza kulia ni Mkuu wa Wilaya hiyo, Luteni Kanali Dennis Mwila.
  Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Brigedia Generali Marco Gaguti (kushoto), akimweleza jambo Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani (kulia). Waziri na Ujumbe wake walifika ofisini kwa Mkuu wa Mkoa kumweleza dhamira ya ziara yake mkoani humo, Februari 27 mwaka huu.
Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani na Ujumbe wake, wakikagua kituo cha kupoza umeme Kyaka, kilichopo wilayani Misenyi, Mkoa wa Kagera, alipokuwa katika ziara ya kazi Februari 27 mwaka huu.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...