Makamu wa Pili wa Rais wa
Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi wa Tatu kutoka Kushoto akizungumza na Uongozi wa
Chuo cha Muziki wa Nchi za Jahazi {DCMA} kilichopo Mtaa wa Mizingani pembezoni
mwa Fukwe ya Forodhan.
Mkurugenzi Mkuu wa Chuo cha
Muziki wa Nchi za Jahazi {DCMA} Bibi Alessia Lombardo Kushoto akimueleza Makamu
wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi muelekeo wa Chuo hicho wa hapo
baadae.
Mkufunzi wa Chuo cha Muziki wa
Nchi za Jahazi {DCMA} Kassim Ali Basalamu akimueleza Balozi Seif changamoto
zinazokikabili Chuo hicho kwa wakati huu.
Mwalimu Mkuu wa Chuo cha Muziki
wa Nchi za Jahazi {DCMA} Mohamed Othman akielezea Mfumo wa Chuo cha CDMA
kinavyotoa Mafunzo wa Watoto wenye mahitaji Maalumwa Skuli ya Kisiwandui.
Makamu wa Pili wa Rais wa
Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Kulia akiupongeza Uongozi wa DCMA Kwa juhudi
unazochukuwa wa kufinyanga Vijana katika Tasnia ya Muziki wa Taarab.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali
Iddi alisema Zanzibar itaendelea kupata umaarufu katika maeneo mbali mbali Duniani
kupitia Muziki wake wa Taarab ambao umekuwa na mvuto wa kipekee hasa kwa wale wanaoamua kuufuatilia ili kujiburudisha.
Alisema Taasisi zinazosimamia masuala ya Muziki
Nchini bado zina wajibu na jukumu la kuhakikisha Sanaa hiyo muhimu kwa Jamii
inalindwa, inakuzwa na kuendelezwa kwa vile mbali ya kuburudisha lakini pia husaidia
Taaluma kupitia Kazi hiyo muhimu inayotoa Ajira kwa kundi kubwa la Vijana.
Balozi Seif Ali Iddi alisema hayo wakati wa
mazungumzo yake na Uongozi wa Chuo cha Muziki wa Nchi za Jahazi {DCMA}
kilichopo Mtaa wa Mizingani pembezoni mwa Fukwe ya Forodhan alipokutana nao
Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.
Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
inafarajika kwa kuwa na Chuo kinachofundisha Muziki wa Taarab uliopata maarufu
tokea Karne ya 18 katika Mwambao wa Afrika ya Mashariki, Kusini na hata Ulimwenguni
kwa kutumia Lugha ya Kiswahili inayozidi kukuza Utamaduni wake.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliupongeza
Uongozi wa Chuo hicho cha Muziki wa Nchi za Jahazi {DCMA} kwa jitihada
unazochukuwa wa kufinyanga Vijana katika Tasnia hiyo ya Taarab ikiwa ni Tanuri
la kupata Ajira katika vikundi mbali mbali vya Muziki mara wamalizapo Mafunzo
yao.
“ Chuo cha Muziki cha Nchi za Jahazi kinastahiki
kuungwa mkono na Washirika wa Maendeleo kutokana na kuwa Tanuri la kuwafinyanga
Vijana ili kuingia katika Ajira kupitia Tasnia na Muziki wa Taarab”.
Alisisitiza Balozi Seif
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alizishauri na
kuziomba Taasisi na Washirika wa Maendeleo kukiunga mkono Chuo hicho wakati
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ikiangalia mazingira na kutafuta mbinu
zitakazosaidia kuzitafutia ufumbuzi
changamoto mbali mbali zinazokikabili Chuo hicho.
Mapema Mkurugenzi Mkuu wa Chuo cha Muziki wa Nchi za
Jahazi {DCMA} Bibi Alessia Lombardo alisema Wahitimu wapatao 170 humaliza
Mafunzo yao Kila Mwaka tokea kilipoanzishwa Chuo hicho
Mnamo Mwaka 2002 kikiwa na Miaka 18 sasa.
Bibi Alessia alisema Chuo hiko kimebarikiwa kupata
Wataalamu wa kujitolea kutoka Mashirika na Taasisi mbali mbali za Kitaifa na
Kimataifa ambao hutoa Mafunzo kwa Wafanyakazi na Wanafunzi wa chuo hicho.
Alisema Mwanafunzi anayepitia Mafunzo ya Chuo hicho
anapomaliza Taaluma yake lazima awe na ujuzi na uwezo kamili utakaomuwezesha kubadilishana mawazo na Msanii mwenzake
popote atakapoamua kwenda Duniani katika masuala ya Muziki.
Mkurugenzi Mkuu huyo wa Chuo cha Muziki wa Nchi za
Jahazi {DCMA} alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba uwezo huo
ndio uliyoonyesha wazi kwa Wasanii wa Chuo hicho kupata mialiko mbali mbali nje
ya Nchini wa kushiriki kwenye Warsha, Matamasha
pamoja na Maonyesho ya Muziki Kimataifa.
Bibi Alessia Lombardo alifahamisha katika muelekeo
wa baadae wa kukijengea uwezo zaidi wa Ufundishaji Chuo hicho umelenga kutoa
Mafunzo yake katika Ngazi ya Cheti na Stashahada kupitia Mfumo wa Baraza la
Taifa la Elimu ya Ufundi Tanzania {NACTE}.
Alisema Uongozi wa Chuo kupitia Bodi yake
umeshatayarisha Mitaala kamili itakayostahiki kufundishwa kwa mfumo huo wa
Nacte lakini kinachosubiriwa kwa wakati huu ni ukamilishwaji wa Taratibu
zinazohusika kwa ajili ya kuanza mfumo huo.
Nao kwa upande wao Mwalimu Mkuu wa Chuo hicho
Mohamed Othman pamoja na Wakufunzi wenzake Kassim Ali Basalamu na Hassan
Mahenge walisema kwa mbali ya jukumu lao chuoni hapo lakini pia hutenga muda wa
kutoa Mafunzo kwa Wanafunzi wenye mahitaji Maalum katka Skuli ya Msingi ya
Kisiwandui.
Walisema mafunzo hayo Maalum yalikwenda sambamba na
kuwapatia mafunzo ya Muziki wana Sanaa wa Kikundi cha Taraabu kilichopo Mahonda
Mkoa Kaskazini Unguja.
Hata hivyo Wakufunzi hao walimuomba Makamu wa Pili
wa Rais wa Zanzibar kutumia nafasi yake itakayowezesha kupatikana kwa Taasisi
na Mashirikia yatayokiunga Mkono Chuo hicho kutokana na kumalizika kwa zaidi ya
Mwaka Mmoja sasa ufadhili waliokuwa wakiutegemea.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...