Na Leandra Gabriel, Michuzi TV

JESHI la Magereza limeeleza kusikitishwa na kitendo cha viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kwa kushindwa kutii sheria bila shuruti na kuhatarisha usalama wa wafungwa, askari na mali za Jeshi la Magereza na hiyo ni baada ya watu wanaoaminika kuwa ni wafuasi na viongozi wa chama hicho wakiwa katika msururu ya magari binafsi na gari za kubeba abiria kufika katika eneo la gereza la Segerea na kutaka kuingia bila utaratibu.

Taarifa iliyotolewa na msemaji wa Jeshi la Magereza SSP Amina Kavirondo imeeleza kuwa Jana Machi 13, 2020  viongozi wa CHADEMA wakiwa na wafuasi wao walifika eneo la Magereza wakiwa na makundi ya watu na msururu wa magari binafsi na magari ya kubeba abiria na walipofika geti kuu walitaka kuingia ndani na magari yao jambo ambalo ni kinyume na taratibu za kiusalama katika eneo hilo ambalo limezuiliwa.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa Askari wa Jeshi la Magereza waliokuwa zamu walijaribu kuwasihi watu wao na kuwaeleza kuwa ni mtu mmoja tuu anayetakiwa kuingia ndani na kukamilisha utaratibu wa kumtoa mfungwa aliyelipiwa faini lakini jitihada hizo za kufafanua utaratibu hazikusaidia na watu hao walikaidi na kuendelea kuweka msongamano katika eneo hilo la kiusalama na kutoa maneno ya kashfa, matusi, vitisho na kumshambulia askari aliyekuwepo zamu na kumchania sare za Jeshi la Magereza.

Imeelezwa kuwa utaratibu wa kusimamia usalama wa eneo la Magereza na itifaki za kiusalama magerezani zilifuatwa na watu hao kuondolewa kwa nguvu ya wastani hadi nje ya eneo la Magereza.

Pia taarifa hiyo imeeleza umma wa watanzania kuwa utaratibu unaotumika kufika na kutembelea maeneo ya Magereza ikiwa ni kwa lengo la kuona wafungwa au kuwatoa wafungwa waliomaliza adhabu yao utaratibu huanzia mahakamani kwa kulipa faini  na mahakama kutoa hati ya uthibitisho wa kupokea malipo hayo hatimaye hati hiyo kukabidhiwa kwa mkuu wa gereza ambaye hufuata taratibu na itifaki ya gereza na kumtoa mfungwa aliyemaliza Kifungo.

Pia imeelezwa kuwa wananchi lazima wafuate kanuni na Sheria za maeneo hayo nyeti ya kiusalama yaliyozuiliwa kwa kutofanya mambo yaliyozuiliwa ikiwemo kutoingia na simu au kamera, kupiga picha, kupiga kelele na kuweka mikusanyiko.

Jeshi hilo limetoa Rai na onyo kali na kueleza kuwa halitovumilia vitendo vya mtu au kundi lolote litakalokaidi Sheria, kanuni na miongozo ya utendaji kazi wa jeshi  na limetoa pongezi kwa wananchi wote wanaotii sheria bila shuruti na kuwakaribisha kuendelea na kupata huduma ambazo jeshi la Magereza linatoa.
Msemaji wa Jeshi la Magereza SSP Amina Kavirondo

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...