*Aruhusu bodaboda kuingia katikati ya Mji

Na Leandra Gabriel, Michuzi TV

MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda  amesema ataendelea kuchukua hatua za kila namna katika kuhakikisha anawalinda wakazi wa Dar es Salaam dhidi ya mlipuko wa virusi vya Corona na hiyo ni pamoja na  kupuliza madawa katika maeneo mbalimbali.

Akizungumza na wananchi katika kituo cha mabasi cha Makumbusho leo jijini Dar es Salaam Makonda amesema kuwa upuliziaji wa madawa katika maeneo mbalimbali unaendeleaje na kuna mpango wa kutumia helikopta katika zoezi hilo ili kuwaweka wakazi wa Mkoa huo salama zaidi.

Pia Makonda amesema kuwa kutokana na hali ya uchumi  wamiliki wa nyumba, vyumba na majengo ya biashara ni vyema wakapunguza kodi kwa asilimia 50 katika kipindi hiki cha mlipuko wa virusi vya Corona.

"Wananchi wa hali ya chini wanategemea biashara ambayo kwa sasa haiendi vizuri, ninawaomba wamiliki wa vyumba, nyumba na majengo ya biashara kushusha kodi kwa asilimia 50 ili kuwawezesha wananchi kubaki na fedha za kununua chakula katika kipindi hiki wanachoshauriwa kubaki ndani" ameeleza Makonda.

Aidha Makonda amewataka wazazi kuwalinda watoto ambao wapo majumbani baada ya shule kufungwa na kuwataka wale wote wasio na shughuli za msingi kusalia majumbani.

Wakati huo huo Makonda amewaruhusu waendesha wa pikipiki maarufu kama bodaboda kuingia katikati ya Mji na kubeba abiria ila kwa kuzingatia Sheria zilizopo ikiwemo kuvaa kofia ngumu (helmet) pamoja na kutopita kwenye barabara za mwendokasi.

"Mna ruhusa ya kuingia katikati ya Mji na kubeba abiria na zoezi hili litaendelea hadi pale amani, afya na Corona itakavyoondoka nchini" amesema.

Kuhusiana na wageni kuingia ndani ya nchi Makonda amesema kuwa utaratibu wa wageni hao kuwekwa karantini kwa siku kumi na nne unazingatiwa na kuwataka wale wote wenye ndugu wanawasili nchini kutokwenda kuwapokea na kuacha majukumu hayo kwa Serikali ya Mkoa na madaktari na kuwashauri wananchi wa Mkoa huo kwenda hospitali pindi watakapohisi kuwa na dalili za Corona.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...