Viongozi na baadhi ya watumishi wa Makumbusho ya Taifa wakimsikiliza
Afisa Utalii wa Jiji Benard Tahondi akieleza kuhusu chimbuko la mji wa
Dar es Salaam ndani ya jengo la Old Boma jijini Dar es Salaam.
Viongozi na baadhi ya viongozi wa
Makumbusho ya Taifa wakitembea mbele ya jengo la St, Joseph Cathedral
halimo pichani walipotembelea majengo ya kihistoria yaliko jijini Dar es
Salaam.Viongozi
na baadhi ya watumishi wa Makumbusho ya Taifa wakiwa katika picha ya
pamoja na maafisa wa utalii wa jiji mbele ya jengo mojawapo
linalohifadhiwa la Karimjee.
*************************************
Na Mwandishi Wetu
Viongo na baadhi ya watumishi wa
Makumbusho ya Taifa la Tanzania wametembelea maeneo na majengo ya
kihistoria yaliyoko kwenye eneo la hifadhi la jiji la Dar es Salaam kwa
lengo la kutalii, kujifunza na kuyaona baadhi ya majengo ya malikale
yaliyokasimishwa kwa Taasisi hiyo.
Katika ziara hiyo iliyoongozwa na
Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Taifa, Dkt. Noel Lwoga waliweza
kutembelea majengo zaidi ya 20 ambayo yamehifadhiwa kwa manufaa ya
kizazi cha sasa na kijacho.
Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya
Taifa anasema kuwa uhifadhi wa majengo na maeneo ya kihistoria ni muhimu
katika kutunza urithi wa asili na historia ya nchi yetu.
Dkt. Lwoga amesema kuwa Makumbusho
ya Taifa imekasimishwa zaidi ya majengo 40 katika jiji la Dar es Salaam
kwa ajili ya kutoa ushauri wa kitaalamu wa uhifadhi na utunzaji wa
maeneo/majengo hayo.
“Haya majengo yamejengwa siku
nyingi lakini yana maana kubwa kwa urithi wa nchi yetu kwa kizazi cha
sasa na kijacho, hivyo bila kuhifadhiwa tutapoteza historia na urithi wa
nchi yetu” alisema Dkt Lwoga.
Baadhi ya maeneo na majengo
yaliyotembelewa ambayo yako chini ya jiji la Dar es Salaam ni pamoja na
jengo la zamani kuliko yote jijini Dar es Salaam lililojengwa mwaka 1866
la Old Boma, jengo la Kanisa katoriki la St Joseph Cathedral, jengo la
shule ya Sekondari St, Joseph, jengo la White fathers (Atman), jengo la
Posta ya zamani, jengo la Karimjee Jivanjee, na bustani ya kumbukumbu ya
vita (War memorial garden) yaliyo kandokando ya Barabara ya Samora.
Mengine ni jengo la Kanisa la
Lutherani la Azania Front, jengo la Mahakama ya Rufaa, jengo la Mahakama
Kuu, jengo la Karimjee, jengo la hospitali ya Ocean Road, Bustani ya
jiji, mnara wa askari na mengineyo.
Akizungumza baada ya ziara hiyo,
Afisa Utalii wa Jiji, Daniel Kobelo amewashukuru viongozi wa Makumbusho
ya Taifa kwa kutembelea maeneo na majengo ya kihistoria na kusema kuwa
ilikuwa fursa nzuri kwao kupata uzoefu na utaalamu wa kimakumbusho.
“Kazi hii ni kweli tunaifanya
lakini tumejifunza mambo mengi kutoka kwenu siku ya leo kwa sababu ninyi
ni wataalam wa uhifadhi wa maeneo ya kihistoria,” alisema Bw. Kobelo.
Amesema uhifadhi ni jamba gumu kufanyika na taasisi moja hivyo, ameomba ushirikiano wa wadau mbalimbali.
“Hii inaweza ikawa mwanzo mzuri wa
ushirikiano wa Jiji na Makumbusho na wadau wengine wanaweza kujitokeza
katika kuhifadhi maeneo haya ya kihistoria na urithi kwa nchi yetu.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...