Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwelwe, ametengua nafasi ya Meneja wa Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), mkoa wa Pwani na Lindi kutokana na kutoridhishwa na usimamizi na ufuatiliaji wa matumizi ya barabara ya Dar es Salaam - Kilwa - Lindi hadi Mingoyo yenye urefu takriban kilometa 450.
Aidha,
ameagiza Mameneja wapya wa mikoa hiyo na mameneja wa mikoa mingine kuhakikisha
wanaziba mashimo yote yaliyopo kwenye barabara zao ndani ya saa 48 kuanzia muda
wa shimo hilo linapojitokeza.
Mhandisi Kamwelwe, ametoa agizo hilo akiwa mkoani Lindi ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, baada ya kutoridhishwa na hali ya miundombinu ya barabara kuanzia Nangurukuru hadi Mbwemkuru wakati alipoikagua barabara hiyo siku chache zilizopita ambapo pamoja na mambo mengine amesema kuwa hadi sasa bilioni 10 zimeshatengwa kwa ajili ya zoezi la kuziba mashimo yote kabla hayajaleta athari zingine.
"Nimetengua nafasi za watendaji hawa wawili kwa makosa yaliyojitokeza katika barabara hizi zinazounganisha mkoa kwa mkoa na hadi kufikia mwishoni mwa mwezi huu nahitaji wananchi wawe wanapita salama katika barabara hii", amesema Waziri Kamwelwe.
Waziri huyo ameeleza kuwa sehemu kubwa ya barabara iliyoathirika ni kuanzia eneo la Muhoro mkoani Pwani hadi Mbwemkuru mkoani Lindi yenye jumla ya urefu wa kilometa 190 na zote zipo katika utaratibu wa kuanza kukarabatiwa.
Waziri Kamwelwe amebainisha kuwa ataendelea kusimamia muongozo wake alioutoa mwezi Juni mwaka huu kuwa barabara yoyote yenye mashimo katika barabara kuu na za mikoa basi huyo Mhandisi wa Mkoa ajiondoe mapema kwani hayuko tayari kufanya kazi na wataalamu wasio weledi na kushindwa kusimamia rasilimali fedha na watu vizuri.
Ameongeza kuwa hadi sasa Serikali imeshatoa kiasi cha fedha bilioni 40 kwa ajili ya matengenezo ya barabara zote nchini zilizoathriwa na maji ya mvua.
"Fedha zipo sasa sitarajii kuona barabara yoyote hapa nchini ina mashimo, huyo Meneja ambaye barabara zake zina mashimo tutamalizana hapo hapo", amesisitiza Mhandisi Kamwelwe.
Waziri
wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwelwe, akitoka kukagua
mzani wa Nangurukuru uliopo mkoani Lindi wakati alipowasili mkoani humo kwa
ajili ya utekelezaji wa agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano Tanzania Mhe. Dkt.
John Pombe Magufuli baada ya kukagua
barabara ya kutokea Lindi hadi Dar es Salaam na kutoridhishwa na hali ya
miundombinu ya barabara hiyo.
Naibu
waziri wa Ujenzi, Elias Kwandikwa, akitoa maelekezo kwa Katibu Mkuu wa
Wizara hiyo anayeshughulikia Sekta ya Ujenzi Arch. Elius Mwakalinga, kuhusu
ukarabati wa sehemu iliyoharibiwa na malori ya mizigo ya mawe katika barabara
ya Mtwara - Lindi - Dar es Salaam.
Viongozi
na Wataalam kutoka wizara ya Ujenzi,uchukuzi na mawasiliano (Sekta ya Ujenzi),
wakisikiliza maelezo kutoka kwa wasafirishaji wa mawe katika eneo la
Kilanjelanje mkoani Lindi tayari kwaajili ya kusafirishwa kuelekea jijini Dar
es Salaam.
Muonekano
wa sehemu ya barabara iliyoharibika kutokana usafirishaji wa mizigo kwa wingi
baada ya ongezeko kubwa la magari ya mizigo yanayotumia barabara hiyo ya Lindi
– Dar es Salaam na kupelekea kuharibu miundombinu ya barabara hiyo.
Lori la mizigo likipakia mawe katika eneo la Kilanjelanje mkoani Lindi tayari kwaajili ya kusafirishwa kuelekea jijini Dar es Salaam.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...