Na Farida Saidy, Michuzi TV
KAIMU Kamishna wa Uhifadhi wanyamapori (TAWA,) Mabula Misungwi Nyanda, Amefanya kikao na watumishi wanaosimamia eneo la mfumo wa ikolojia wa Ziwa Natron, Mto wa Mbu na Longido na kuwaagiza watumishi wa eneo hilo kufanya kazi kwa bidii na ushirikiano kwani eneo wanalosimamia ni eneo la kimkakati katika kukusanya mapato ya Serikali.
Akizungumza katika kikao hicho kilichowakutanisha viongozi mbalimbali kutoka wizara ya maliasili na utalii Kamishna amewaeleza watumishi kuwa uongozi unatambua changamoto zilizopo kwenye eneo hilo na kuwaasa wasikate tamaa kwa kuwa changamoto hizo zinashughulikwa.
Aidha, amefafanua mabadiliko mbalimbali yaliyofanywa na Serikali kwa lengo la kuboresha utendaji ikiwemo mabadiliko ya majukumu ya kukusanya maduhuli ambayo yamehamishiwa kwa Mamlaka ya Mapato (TRA) pamoja na taratibu za utekelezaji wa Jeshi USU kuanzia ngazi ya Wizara hadi kwenye Taasisi za uhifadhi zilizopo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii.
Pia baadhi ya watumishi wameipongeza Menejimenti ya TAWA kwa jitihada mbalimbali zinazofanywa na mamlaka hiyo ambazo zimeanza kuleta mabadiliko chanya katika utendaji wao wa kazi.
Kwa upande wake Naibu Kamishna wa Huduma za Utalii na Biashara Imani Nkuwi, Amewapongeza watumishi wa TAWA kwa juhudi zao za kusimamia rasilimali za wanyamapori pamoja na changamoto zilizopo.
Vilevile Mkurugenzi wa Sheria kutoka Wizara ya Maliasili amewaeleza watumishi mabadiliko ya Sheria yaliyofanyika na kusema kuwa Wizara inaandaa kanuni na miongozo mbalimbali kwa ajili ya kuwezesha utekelezaji wa Sheria hiyo.
Kikao hicho kilihudhuriwa na Naibu Kamishna wa Huduma za Utalii na Biashara Imani R. Nkuwi, Mkurugenzi wa Sheria (DLS,) Lucy Seleko kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii ,Kaimu Kamishna Msaididizi Mwandamizi Kanda ya Kaskazini Mbanjoko Peter, Afisa Mfawidhi wa Kituo cha Matumizi Endelevu ya Wanyamapori Bi. Segorine Tarimo na Afisa wa Sheria kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii Happiness Salago.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...