Jamii
mkoani Njombe na Tanzania kwa ujumla wametakiwa kuwa na utamaduni wa
kufanya vipimo vya hali ya lishe angalau mara mbili au tatu kwa mwaka
ili kufahamu hali yake ya lishe na kumsaidia kufuata njia bora za lishe
ili kuepuka utapiamlo.
Hayo yamebainishwa na Afisa Mtafiti
Mwandamizi-Lishe kutoka Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania (TFNC)
Bi.Maria Ngilisho kwenye mwendelezo wa maonesho ya Wiki ya Chakula
Duniani iliyozinduliwa rasmi tarehe 10/10/2020 ambapo Kitaifa
maadhimisho haya yanafanyika Mkoani Njombe na yatahitimishwa 16/10/2020.
Bi.Ngilisho
amesema, moja ya vipimo vinavyoweza kutoa tafsiri ya kuwa na hali nzuri
ya lishe ni kipimo cha uwiano kati uzito na kimo/urefu ili kupata
farihisi (Body Mass Index - BMI).
Amesema, kabla ya kufanya
vipimo vya hali ya lishe katika banda lao, mteja anaeleweshwa namna ya
kupanda kwenye mizani (kuvua viatu, kutoa vitu mfukoni kama vile
funguo, simu na vitu vingine ambayo vinaweza kuongeza uzito wake kama
vile saa) na kusimama kwenye ubao wa kupimia kimo/urefu (kuvua viatu;
mgongo kuwa sambamba na ubao; makalio, mabega na kisogo viguse ubao;
kusimama wima na kuangalia mbele)", alisema Bi. Ngilisho.
Aliendelea
kwa kusema, baada ya vipimo kuchukuliwa, vinaoanishwa kwa kutumia kadi
ya farihisi ili kupata tafsiri ya hali yake ya lishe na kupewa ushauri
stahiki kufuatana na matokeo ya vipimo vyake.
Aidha Bi. Ngilisho
alisema, katika kurahisisha uelimishaji wa njia sahihi ya kupanga mlo
kamili kwa jamii ni kutumia dhana ya pitamidi ya chakula (muundo wa
kabati iliyotenganishwa katika vyumba vitano, chumba kikubwa kikiwa
chini na kidogo kabisa kikiwa juu). Kila chumba katika piramidi hii kina
wakilisha kundi moja la chakula, ili kupata/ kuandaa mlo kamilo
inatakiwa kuchukua angalau chakula kimoja kutoka kwenye kila
kundi/chumba.
"Kundi la kwanza lina vyakula vya nafaka (mahindi,
ngano, ulezi, mtama, uwele, nk.), mizizi (mihigo, viazi vitamu, viazi
mvitingo, magimbi, nk.) na ndizi (ndizi mbichi).Kundi la pili lina
vyakula vya asili ya wanyama (nyama ya ng'ombe, kuku, mbuzi, nk.,
maziwa, mayai, dagaa, samaki na wadudu waliwao kama senene na
kumbikumbi. Jamii ya mikunde ni kama maharage, njegere, mbaazi, kunde,
choroko, soya, nk.).
Kundi la tatu ni la mboga za majani (mchicha,
spinachi, chinise, figiri, tembele, nk.) na mboga-mboga (pilipili hoho,
karoti, vitunguu, nyanya, bamia, biringanya, nyanya chungu, matango,
nk.), bila kusahau mboga za asili na porini. Kundi la nne ni la matunda
ya aina mbalimbali kama machungwa, maembe, mananasi, ndizi mbivu, limao,
fenesi, parachichi, machenza, nk., ukijumuisha pia matunda ya asili na
matunda ya porini. Kundi la tano la tano linajumuisha vyakula kama
sukari, mafuta, karanga, ufuta, korosho, mbegu mbalimbali kama vile
mbegu za alizeti, maboga na nazi" Alisema Bi.Ngilisho.
Nae afisa
lishe mtafiti kutoka taasisi hiyo, Elizabeth Lyimo, alielezea kuhusu
mchezo wa karata za mlo kamili ambao lengo lake ni kuboresha uelewa wa
wananchi kuhusu mlo kamili kwa njia shirikishi na ya kufurahisha ili
kuvutia washiriki kujifunza.
"Mtu yeyote anaweza kucheza mchezo
wa karata za mlo kamili. Masuala ya chakula katika ngazi ya kaya
yanatekelezwa kwa asilimia kubwa na wanawake, wanaume wamekuwa
wakishiriki kwa kiwango kidogo hivyo basi mchezo huu unawalenga zaidi
wanaume wa rika zote ili wapate uelewaa wa kupanga mlo iwe katika
kununua vyakula au kuandaa mlo kwa ajili ya familia. " Alisema
Elizabeth.
Aidha Mteknolojia Mwandamizi wa Maabara kutoka taasisi ya chakula na lishe Juvenary Mushumbusi alisema taasisi ina Maabara
mahususi kwa ajili ya kufanya uchunguzi wa
kimaabara ili kuiwezesha Taasisi kutekeleza na kufanikisha majukumu yake.
Maabara hii ina vitengo vitatu, ambayo ni;
• Mabara ya Kemia ya Chakula (Food Chemistry
Laboratory)
Kazi kuu ya maabara hii ni kufanya uchunguzi wa
sampuli za chakula ili kubaini uwepo na wingi wa viinilishe
kama
vile, protini, wanga, mafuta, vitamini, madini na phytochemicals. Pia
kitengo hiki hufanya uchunguzi wa kubaini ubora na usalama wa chakula
Kama vile uwepo na wingi wa sumukuvu, madini tembo, sumu kwenye
mihogo (cyanide) na vikolezo (food additives)
• Maabara ya Baiokemia (Biochemistry
Laboratory)
Kazi
kuu ya maabara hii ni kufanya uchunguzi wa sampuli zinazochukuliwa
kutoka kwenye mwili wa binadamu ili kubaini viwango vya virutubishi au
viashiria lishe mwilini (Nutritional Biomarkers) mwilini; kwa mfano,
vitamin, madini na elementi mbalimbali, mafuta na wingi wa damu
• Maabara ya Maikrobiolojia (Microbiology
Laboratory)
Kazi
kubwa ya maabara hii ni kufanya vipimo maalumu vya kilishe Kama vile
folate na amino asidi kwa kutumia mbinu za maikrobiolojia.
Pia
maabara hii hupima vimelea vinavyo patikana kwenye chakula ili kubaini
usalama na ubora wake kimikrobiolojia km vile uwepo wa vijidudu
vinavyosabisha magonjwa kwa mtumiaji wa chakula au vile vinavyoashiria
kuharibika kwa chakula au vinavyoashiria hali ya usa lama wa
maeneo/mazingira yanayuhusika na utayarishaji/usindikaji wa chakula
husika. Baadhi ya vimelea hivi ni kama Salmonella, E-coli,Shigella na
S.aureus
Juvenali Msumbusi ni mtekinolojia mwandamizi wa maabara
kutoka taasisi ya chakula na lishe taifa,amesema kulingana na maeneo ya
nyanda za juu kusini mimea kukosa virutubishi,serikali imekuja na mpango
wa kuongezea virutubishi kwenye chakula.
"Serikali saizi imekuja
na mpango mwingine wa kuongezea virubishi kwenye vyakula kama unga wa
mahindi na ngano na virutubishi hivi havibadilishi rangi wala radha na
kwenye upande wa vitamini A tunaongeza virubishi kwenye mafuta ya
kura"alisema Juvenali Msumbusi
Aidha amewata wananchi kufika na
kupata elimu katika taasisi hiyo licha ya wao kutumia njia mbali mbali
ili kumalizana na tatizo la udumavu ikiwemo kwa watoto wadogo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...