…………………………………………………………………………………….
Na Mwandishi Wetu-MAELEZO
Msemaji Mkuu wa
Serikali, Dkt. Hassan Abbasi, ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya
Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, amekamilisha haki yake ya kikatiba
kwa kupiga kura katika eneo la Kilimani, jijini Dodoma.
Katika eneo hilo
ambapo pia awali na baadaye walionekana viongozi wengine mbalimbali wa
Serikali, Chama na taasisi binafsi, Dkt. Abbasi alikaa kwenye foleni
kama kawaida na wananchi wengine na alipomaliza kupiga kura akasisitiza:
“Nimekamilisha haki
yangu ya kikatiba kwa furaha sana kwa sababu tukiwa pale kwenye foleni
tunapiga stori za hapa na pale wananchi walikuwa wanasema sio wote
tuliopiga nao kura mwaka 2015 leo wamepata bahati tena kama hii kwa
maana ya uhai kushiriki nasi. Hivyo ni jambo si tu la kikatiba lakini
lenye hisia kubwa kibinadamu na kiroho mtu anapolitimiza.”
Dkt. Abbasi alieleza
kuridhishwa na hali ya utulivu kituoni hapo na kusisitiza ambao
hawajakamilisha haki yao wajitokeze kuwahi kabla ya muda uliowekwa na
Tume kukamilika.
“Kituoni kwetu hapa
na kwingine nilikopita hapa Dodoma hali ni shwari. Tume imejipanga hasa
utaratibu ni mzuri na wa uhakika kwani kila hatua unaelekezwa wasimamizi
na makarani wa uchaguzi na mawakala wa vyama wanajiridhisha kwa kila
jina linalotajwa.
“Ukiacha kelele za
baadhi ya wanasiasa wachache Watanzania wengi wameitikia wito wa amani
na wengi tuliopiga nao kura hapa kila mmoja anasema anarejea nyumbani au
kwenye shughuli zake kwa ajili ya kuendelea na masuala mengine
atasubiri matokeo kuanzia jioni,” alisema Dkt. Abbasi.
Dkt. Abbasi ametumia
muda huo pia kuvipongeza vyombo vya habari kwa kazi kubwa waliyoifanya
kuripoti kampeni za vyama mbalimbali na kuvitaka kumaliza vyema zoezi
hili la uchaguzi kwa kufuata taratibu za Tume hasa katika kutangaza
matokeo ya awali hadi yale ya mwisho.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...