Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mwita Waitara, akisisitiza jambo kwa uongozi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), namna ya kusimamia nidhamu na matumizi ya fedha alipokagua upanuzi wa Bandari ya Tanga.






NAIBU Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mwita Waitara, ametoa siku 14 kwa uongozi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), kumpa taarifa ya mradi wa upanuzi wa Bandari ya Tanga unaogharimu zaidi ya shilingi Bilioni 500.

Hatua hiyo imefikiwa baada ya Naibu Waziri huyo kutoridhishwa na maelezo ya namna kiasi cha shilingi Bilioni 172 zilivyotumika katika ujenzi wa kuongeza kina katika bandari hiyo ili kuziwezesha meli kubwa kutia nanga.

“Natoa siku 14 niwe nimepata taarifa ya kina kuhusu mradi huu na namna ya mchakato wa kumpata mkandarasi ulivyofanyika, nani alifanya upembuzi yakinifu, nani alishauri kutumiwa kwa hizo fedha, nani walihusika katika usimamizi wa huo mradi na tathimini ya fedha zilivyotumika ili kuiwezesha Serikali kuchukua hatua”, amesisitiza Naibu Waziri Waitara.

Amesema nia ya Serikali ni kuiona Bandari ya Tanga ikifanya kazi katika viwango vya juu na hivyo kuchangia kukuza uchumi wa Taifa na yoyote atakayebainika kukwamisha dhamira hiyo ya Serikali atachukuliwa hatua kali.

Amemtaka Mkurugenzi Mpya wa TPA, kupanga safu yake ya uongozi mapema iwezekanavyo ili kuendana na kasi na matarajio ya Serikali ya Awamu ya Sita.

Amewataka watumishi wa Taasisi zote zilizo chini ya Wizara yake kusoma mpango wa Maendeleo ya Taifa wa 2020 - 2025 ili kuweza kujua wanatakiwa wafanyeje na kwa namna gani katika kipindi hicho.

“Fanyeni kazi kwa weledi, acheni majivuno, hudumieni wananchi”, amesisitiza Naibu Waziri huyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa TPA, Bw. Erick Hamis, amesisitiza kwamba taarifa zinazotakiwa zitawasilishwa kwa wakati na miradi inayoendelea katika Bandari ya Tanga itakamilika katika kipindi cha miaka mitatu ijayo ili kuiwezesha Bandari hiyo kuhudumia tani milioni mbili za shehena toka tani laki saba zinazohudumiwa kwa sasa.

“Tutahakikisha uwepo wa reli na barabara za uhakika katika Mkoa wa Tanga kuelekea mikoa ya Kaskazini na katikati ya nchi kunawezesha bandari hii kufanya kazi kwa ufanisi”, amesema Bw. Hamis.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Waitara amekagua maendeleo ya ujenzi wa barabara ya Tanga – Pangani (KM 50) kwa kiwango cha lami na kumtaka mkandarasi M/S China Henan International kukamilisha barabara hiyo kwa wakati na Serikali haitakubali visingizio visivyo na tija.

Naye, Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Mkoa wa Tanga, Mhandisi Alfred Ndumbaro, amesema Serikali imetoa kiasi cha shilingi Bilioni 4 kwa ajili ya kulipa fidia  wananchi waliopisha ujenzi wa barabara hiyo na zoezi la kulipa fidia litaanza Mei 03, mwaka huu.

Amemhakikishia Naibu Waziri huyo kuwa atamsimamia kikamilifu mkandarasi ili kuhakikisha barabara hiyo inajengwa kwa viwango na kukamilika kwa wakati na hivyo kufungua ukanda wa Wilaya ya Pangani.

Naibu Waziri Waitara yupo mkoani Tanga kuendelea na ziara yake ya siku nne ya kukagua miundombinu ya Sekta ya Ujenzi na Uchukuzi ambapo pamoja na mambo mengine  amezungumza na watumishi ili kuwapa muelekeo wa Serikali na kusikiliza hoja zao.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...