RAIS
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amesema kwamba
Jeshi la Polisi nchini sharia zao zilizotungwa ni sheria za udhibiti ,
hivyo jeshi hilo lijielekeze zaidi katika kudhibiti makosa badala
kutumia sheria zilizopo kuzigeuza kuwa kitega uchumi.
Amesisitiza
sheria zilizopo zaidi zitumike kudhibiti kuliko kujikita kwenye
ukusanyaji fedha na tozo nyingine huku akitumia nafasi hiyo kusisitiza
umuhimu wa jeshi la polisi kutoa elimu inayohusu usalama barabarani
pamoja na usalama wa mali zao.
Rais Samia amesema hayo leo baada
ya kuzindua kiwanda cha Ushonaji cha Jeshi la Polisi jijini Dar es
Salaam ambapo wakati akitoa hotuba yake amezungumzia masuala mbalimbali
yanayohusu jeshi hilo, hivyo ametumia nafasi hiyo kueleza anawashakuru
Polisi kwa vipindi vyao vya kutoa elimu kwa umma kuhusu mambo yanayohusu
usalama barabarani na usalama wa raia.
“Ninawashukuru sana kwa
vipindi vile kwa kuwa elimu inatoka lakini naomba muongeze jitihada ili
wananchi wengi zaidi waweze kuwasikia ili kupunguza hayo, ni vema na
najua kiwanda hiki pengine kimejengwa kwa fedha hizo ,lakini ni vema
kama tukajielekeza kwenye kutoa elimu zaidi kuliko kutumia sheria kama
vitega uchumi.
Aidha Rais Samia ametumia nafasi hiyo kueleza
kwamba pamoja na pongezi ambazo amezitoa kwa Jeshi la Polisi katika
kukabiliana na uhalifu lakini bado kuna changamoto za kiusalama.”Kama
nilivyowahi kusema nikiwa Mlimani City wanaojihusisha na vitendo vya
ujambazi na uhalifu wasijaribu kupima kina cha maji kwa kutaka kurejesha
vitendo vya vitendo vya ujambazi hapa nchini.
“Nakupongeza IGP
Sirro baada ya kauli yangu ile pale Mliman City, Mei 8 mwaka huu
ulikutana na Jeshi la Polisi ili kuweka mikakati ya kupambana na hali
hiyo, ni matumaini yangu kuwa tutaona matunda ya mkutano huo ingawa bado
tunasikia vijitaarifa taarifa hawa watu wanaendelea kubonyeza.
"Naomba
muwe wagumu wanapobonyeza msibonyee, mliweza na hakuna sababu ya kurudi
nyuma sasa hivi.Naomba sana Jeshi la Polisi mjipange vizuri kukabiliana
na hao wanaotaka kuwajaribu na hii sio hapa Dar es Salaam ni nchi
nzima,”amesema Rais Samia.
Akifafanua zaidi amesema kwamba hivi
sasa hata katika kuteua au kutengua makanda wa Polisi wa mikoa, moja ya
kigezo ambacho atakitumia ni jinsi gani anayeteuliwa au anayetenguliwa
anaweza kukapabiliana na wahalifu nchini.”Na niwe mkweli miongoni mwa
vigezo ambavyo tutavitumia kuteua au kutengua makamanda wa mikoa ni
udhibiti wa vitendo vya ujambazi ikiwemo wa kutumia silaha.
“Hii
nayo itakuwa moja kati ya vigezo, najua IGP umeniletea majina kadhaa kwa
ajili ya zile Kamisheni mbili ya Fedha na Lojistiki na ile Kamisheni
nyingine lakini hiki kitakuwa moja ya kigezo ambacho nitatumia.”
Na Said Mwishehe, Michuzi TV
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...