Na Muhidin Amri,Tunduru

MKUU wa mkoa wa Ruvuma Balozi Wilbert Ibuge, amewataka wazazi na walezi katika wilaya ya Tunduru na mkoa wa Ruvuma kuchangamkia fursa ya  mafunzo ya ufundi yanayotolewa na chuo cha Nazareti  kilichopo kata ya Mbesa wilayani Tunduru badala ya kutumia muda mwingi kuwafundisha vijana mila potofu zinazorudisha nyuma maendeleo.

Balozi Ibuge, amesema hayo baada ya kutembelea chuo hicho kinachomilikiwa na Kanisa la Biblia Tanzania na kufurahishwa namna  kinavyotoa mafunzo kwa vijana na kwa weledi mkubwa pamoja na kuwa na vifaa vya kisasa vinavyotumika kufundisha.

Hata hivyo, amesikitishwa na idadi ndogo ya wanafunzi  waliopo licha ya uongozi wa chuo kutoa nafasi kubwa na upendeleo kwa kuweka gharama ndogo  hasa vijana wanaotoka ndani ya wilaya ya Tunduru.

Chuo cha Nazareti Mbesa wilaya ya Tunduru kinafundisha masomo mbalimbali ikiwemo  Useremala na ufundi wa magari kwa lengo la kuwapatia ujuzi vijana ili waweze kujitegemea mara baada ya kumaliza masomo yao.

Amesema,jambo la kusikitisha kuona kuna mwamko mdogo wa vijana hususani wa wilaya ya Tunduru kwenda kupata  ujuzi katika chuo hicho.

Aidha,  amewasisitiza viongozi wa kata ya Mbesa na wilaya ya Tunduru akiwemo Mbunge wa Jimbo la Tunduru Kusini Daimu Mpakate kufanya jitahada za makusudi  kuhamasisha vijana wengi ili kujiunga na chuo hicho kwa manufaa yao na jamii.

“nina fikiri kwa dhati kabisa mfanye jambo  na vitu vitakavyosaidia  chuo iki kuwa na vijana wengi zaidi, unajua kuna ule msemo unaosema kwenye miti mingi hakuna wajenzi  na miti ipo kwa hiyo lazima tuhamasishane ili tupate wajenzi wengi”

“Serikali haiwezi kuajiri vijana wote,kwani  ina uwezo wa kuajiri asilimia 3.1 tu sasa hawa wengine watakwenda wapi,kwa hiyo ni lazima wajiajiri wenyewe”amesema Balozi Ibuge.

Amesema,uhamasishaji kwa ajili ya kupata vijana ni mdogo kwani chuo kina uwezo wa kuchukua wanafunzi  96 na  bado kuna wengine ziada 50  wanaoweza kujiunga bila kuhitaji kulala,lakini bado  mwitikio  wa wanafunzi hasa wenyeji wa wilaya ya Tunduru kujiunga na chuo hicho ni mdogo.

“apa kuna chuo kinachoweza kutoa huduma kwa jamii kwa kiwango kikubwa lakini  bado kinatoa kwa kiwango cha chini sio kwa sababu hakitaki bali watu ndiyo hawataki”amesema.

Balozi Ibuge, ametaka uhamasishaji  huo  lazima uende kwenye kuondoa mawazo mgando ya kijamii tuliyonayo hasa kuhusu mtoto wa kike kwa kuwapa stadi za maisha yao na kuondokana na mila potofu.

Amesema, ana taarifa kwamba watoto kati ya miaka saba na minane  katika wilaya ya Tunduru wanafundishwa  namna ya kuishi na wanaume, wengine kuozeshwa wakiwa bado na umri mdogo jambo ambalo ni makosa makubwa.


Amesema,  jamii na viongozi wa wilaya hiyo wana wajibu wa kuwapeleka vijana shule na kuwapa stadi za maisha ili wapate elimu na baadaye kuwa viongozi watakao iongoza Nchi yetu badala ya kuwafundisha mila potofu.

Balozi Ibuge ambaye pia ni Mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama mkoa  amesisitiza kuwa, uhamasishaji na nguvu kubwa ujikite kuzungumzia tabia na mila zisizofaa zinazopoteza muda wa maendeleo.

Amesema, chuo cha ufundi na Hospitali  kinahitaji vijana wazawa na wazalendo watakaofanya kazi kwenye taasisi hizo kuliko wanaokuja kutoka nje ambapo  ameitaka jamii ya wana Tunduru  kuunganisha nguvu kwa kupata vijana wengi watakaojiunga na chuo hicho.

Kwa upande wake Mkuu wa chuo hicho Ezakiel Mapunda amesema, chuo kina uwezo wa kuchukua  vijana 96 kwa  wa fani za ufundi magari na useremala, hata hivyo waliopo kwa sasa hawafiki nusu ya uwezo wa chuo.

Amesema, chuo kilianzishwa kwa misingi ya kufundisha vijana wanaoishi kuzunguka maeneo hayo na wilaya ya Tunduru ili wapate ujuzi utakaowasaidia kujiajiri ,hata hivyo changamoto kubwa ni mwamko mdogo wa wazazi kupeleka  watoto kujiunga na chuo hicho.

Mkurugenzi wa Taasisi ya Mbesa Helga Amburste amesema,licha ya taasisi hiyo kutoa huduma mbalimbali za kijamii na zinazochangia maendeleo, lakini  tatizo ni kutopewa hati miliki ya eneo  lao.

Amemuomba Mkuu wa mkoa, kusaidia ili waweze kupata hati miliki ya ardhi yao ambayo wameiomba kwa muda mrefu.

,Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Balozi Wilbert Ibuge kulia,akimsikiliza mkuu wa chuo cha ufundi Nazareti  Mbesa Ezekiel Mapunda kushoto namna chuo hicho kinavyofanya kazi  ya kutoa mafunzo ya ufundi wa magari na useremala kwa vijana,katikati Mkuu wa wilaya ya Tunduru Julius Mtatiro. Picha na Muhidin Amri,

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...