Charles James, Michuzi TV
MBUNGE wa Jimbo la Mlimba Godwin Kunambi amesema moja kati ya malengo yake katika kukuza ajira kwa vijana wa Jimbo lake ni kuanzisha Timu ya Soka ya Mlimba ambayo watapambana kuhakikisha inafika Ligi Kuu Tanzania Bara.
Kunambi ametoa kauli hiyo wakati wa ziara yake ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa jimboni kwake ikiwa ni pamoja na kuzungumza na viongozi wa Chama Cha Mapinduzi na Watendaji wa Serikali.
Amesema mchezo wa mpira wa miguu umekua sehemu ya ajira kwa vijana wengi nchini ambapo wamepata mafanikio kutokana na vipaji vyao.
"Mkoa wetu wa Morogoro na hasa Jimbo letu la Mlimba lina vijana wengi ambao ni mahiri katika kusakata kabumbu, ni kiu yangu kuona tunaanzisha Timu yetu ya Jimbo ambayo itashiriki Ligi za madaraja na kwa pamoja tuifikishe Ligi Kuu, kama nikiwa Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma nilifanikiwa kuipeleka Dodoma Jiji Ligi Kuu basi naamini hata hapa Mlimba tutaweza.
Hivyo natoa maelekezo kwa Madiwani wote wa Jimbo hili katika Kata 16 kuhakikisha wanaanzisha Ligi za Kata ambapo baadae washindi wa kila Kata wataenda kucheza Ligi ya Jimbo ambayo nitaianzisha ambapo kupitia Ligi hiyo tutapata wachezaji bora watakaounda Timu yetu ya Mlimba," Amesema Kunambi.
Mbunge huyo amekabidhi mipira ya mazoezi kwenye kata hizo ambapo amesema Madiwani wakishaanzisha Ligi za Kata atawaletea mipira, jezi na vifaa vingine vya michezo ili kufanikisha Ligi hiyo.
Viongozi wa Kata ya Mofu wakipokea mipira kutoka kwa Mbunge wa Jimbo la Mlimba, Godwin Kunambi (kulia) ikiwa ni mkakati wake wa kuanzisha Ligi za Kata lengo likiwa kuanzisha Ligi ya Jimbo itakayowezesha kupatikana kwa Timu ya Mlimba.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...