Na Muhidin Amri,Namtumbo
CHAMA Kikuu cha Ushirika cha wilaya ya Songea na Namtumbo(Sonamcu
Ltd)cha mkoani Ruvuma, kimefanya mnada wa tatu wa zao la mbaazi kupitia
mfumo wa stakabadhi ghalani huku wakulima wakifurahi bei nzuri
inayotolewa na wanunuzi.
Meneja wa Sonamcu Juma Mwanga amesema, Sonamcu imefanya minada mitatu na
hadi sasa kilo 1,327,513 zimeuzwa na Sh. Bilioni 1,727,765.879
zimelipwa kwa wakulima.
Amesema, katika mnada wa kwanza uliofanyika tarehe 11 Agosti, jumla ya
kilo 41,428 zimeuzwa kwa bei ya Sh.1,280 kwa kilo ambazo zimenunuliwa na
Kampuni ya Ginning Afrisian ambayo imelipa Sh. 53,027,840.00 na baada
ya tozo ya Sh.57 kwa kilo wakulima wameingiziwa jumla ya
Sh.50,666,444.00 kwenye akaunti zao.
Amesema, mnada wa pili umefanyika tarehe 18 Agosti na kilo 406,517
zimeuzwa kwa bei ya Sh. 1,320 kwa kilo moja na kufanya fedha zilizoingia
kwa mnada huo kufikia Sh.536,602,440.00.
Mwanga amesema,katika mnada huo makampuni matano yalijitokeza kwa ajili
ya kutaka kununua mbaazi,hata hivyo makampuni mawili ya Mohamed
Enterprises na Lenic Tanzania Ltd ndiyo yaliyoshinda na kupata fursa ya
kununua mbaazi zote zilizoingizwa mnadani.
Kwa mujibu wa Mwanga, katika minada hiyo miwili wanunuzi wamechangia
jumla ya Sh.16,126,020.00 kama ushuru kwa Halmashauri na wakulima
wamechangia Sh.895,890.00 katika mfuko wa maendeleo kwa Halmashauri ya
wilaya.
Mwanga amesema, Chama Kikuu cha Ushirika(Sonamcu Ltd)kimepata jumla ya
Sh.6,719,175.00 kama ushuru wa mauzo ya mbaazi kutokana na usimamizi na
uratibu wa shughuli nzima za minada katika wilaya ya Namtumbo.
Mbali na Sonamcu,vyama vya Msingi vya Ushirika(Amcos)vimepata jumla ya
Sh.15,678,075.00 kutokana na kuuza mbaazi za wanachama wake kupitia
mfumo wa stakabadhi ghalani.
Aidha amesema, katika mnada wa tatu uliofanyika tarehe 25 Agosti, kilo
879,568 zimeuzwa ambapo kampuni ya Lenic Tanzania Ltd imenunua mbaazi
zote kwa bei ya Sh. 1,380 kwa kilo moja, na kuwalipa wakulima jumla ya
Sh. 1,213,803,840.
Hata hivyo amesema, baada ya tozo ya Sh.57 kwa kilo wakulima wamelipwa
Sh. 1,323 na kufanya jumla ya fedha zilizoingia kwenye akaunti za
wakulima kutokana na mnada huo kufikia Sh. 1,163,668.
Mkulima wa mbaazi Ziaba Twaibu,ameishukuru Serikali kwa kusimamia vyema
mfumo wa stakabadhi ghalani hasa kwa zao la mbaazi ambalo siku za nyuma
halikuwa na thamani kutokana na kukosa wanunuzi.
Amesema, mfumo wa kuuza mazao kwa utaratibu wa stakabadhi ghalani licha
ya kumwezesha mkulima kupata soko la uhakika, umesaidia kurudisha
mahusiano ya familia na kuimarika kwa ndoa nying na kuhaidi kuongeza
uzalishaji wa zao hilo kwa msimu ujao.
Mkulima mwingine Hajali Ndimbo amesema, kwa ujumla zao la mbaazi
limeleta tija kubwa kwa wakulima na kukomesha vitendo vya dhuluma na
wizi vilivyokuwa vinafanywa na wafanyabiashara.
Hata hivyo,ameiomba Serikali kuendelea kusimamia mfumo wa stakabadhi
ghalani kwa mazao yote ya biashara na kuongeza wanunuzi wengi ambao
wataleta ushindani wa bei ya mazao.Mwenyekiti wa Sonamcu Ali Chemka, ametoa wito kwa wakulima ambao
hawajapeleka mbaazi zao kwenye maghala, wapeleka ili kuwahi bei na
msimu mpya wa kilimo .
Amesema, katika msimu wa mwaka huu hakuna changamoto ya kuchelewa malipo
ya wakulima,kwa hiyo ni vyema wakulima wakachangamkia fursa hiyo
iliyoletwa na Serikali, badala ya kuuza kwa wafanyabiashara wa mitaani
wanaonunua kwa bei ya chini.
Chemka amesema, minada ya mbaazi inayofanywa kupitia mfumo wa stakabadhi
ghalani imesaidia kuzuia vitendo vya wizi vinavyofanywa na
wafanyabiashara dhidi ya wakulima.
Pia,stakabadhi ghalani imevisaidia vyama vya Msingi vya Ushirika(Amcos)
na Chama Kikuu cha Ushirika(Sonamcu) kupata fedha za kujiendesha na
Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo kupata mapato.
Kwa upande wake Afisa Ushirika wa wilaya ya Namtumbo Emmanuel Gwao,
ameipongeza Serikali kwa kusimamia uuzaji wa mazao ya wakulima kwa mfumo
wa stakabadhi ghalani.
Amesema, mfumo huo umewaangalia zaidi wakulima ili wapate tija na
umesaidia kutoa ajira za muda kwa baadhi ya watu wakiwemo wachukuzi na
hata kufufua baadhi ya vyama vya Msingi vya ushirika vilivyopoteza
uwezo wa kutekeleza majukumu yake.
Baadhi ya wakulima wakifuatilia mnada wa mbaazi zinazouzwa kupitia mfumo wa stakabadhi ghalani katika wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma jana.
Baadhi ya vijana kutoka maeneo mbalimbali wa wilaya ya Namtumbo waliopata vibarua vya muda wakishusha shehena ya mbaazi wakati wa mnada wa tatu wa zao hilo uliofanyika Namtumbo. Picha na Muhidin Amri,
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...