Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha ACT Wazalendo, Mhe. Othman Masoud Othman, amewahimiza wanachama wa chama hicho kuendelea kuunga mkono juhudi za viongozi wao ili waweze kufikia dhamira yao.

Ameyasema hayo katika kikao maalumu pamoja na viongozi wa ACT Wazalendo wa mikoa yote saba ya kichama ya kisiwani Unguja kilichofanyika kwenye Ukumbi Wa Majid Hall, uliopo Kiembe Samaki, Magharibi 'B' Unguja.

“Kwa kweli, nafasi pekee ya  kukifikisha chama chetu katika dhamira yake ni kwa wanachama kuendelea kuunga nguvu moja katika utafutaji wa haki pamoja na kuwa na umoja wa dhati na mshikamano”, alisema Mhe. Othman, ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar.

Aidha, amesema ni muhimu kuendelea kujenga hoja madhubuti, nidhamu pamoja na uwajibikaji kama misingi ya  kukiendeleza chama hicho.

Amesisitiza kuwa misingi bora iliyoachwa na aliyekuwa mwenyekiti wa chama hicho, Marehemu Maalim Seif Sharif Hamad, imekuwa ni fursa kwa chama kuendelea kuungwa mkono na wananchi walio wengi nchini, jambo linalotoa taswira mpya katika kufikia dhamira yao.

“Heshima aliyotuwachia Mzee wetu ndiyo ambayo hadi leo inatubeba na kutuweka mbele ya wengine na hivyo lazima kwetu kuendelea kuienzi,” alisema.

Sambamba na hayo, amewakumbusha wanachama hao kuendelea kudumisha amani ya kweli na uwajibikaji kwa lengo la kuinua maendeleo ya Zanzibar.

Mapema Kiongozi wa ACT Wazalendo, Ndugu Zitto Zubeir Kabwe, amesema Chama hicho kitaendelea kuhakikisha makubaliano  yaliyopo baina yao na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yanatekelezwa ikiwemo suala la uchunguzi juu ya waathirika wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2020, uwepo wa tume ya maridhiano itakayotoa haki sawa kwa raia wote pamoja na kuwepo kwa chaguzi za haki nchini.

Ameongeza kuwa kuwepo kwa Katiba Mpya ni miongoni mwa fursa pekee itakayoiinua Zanzibar kimaendeleo pamoja na kuondosha matatizo mbalimbali yanayojitokezaa katika kila chaguzi zitakazofanyika nchini.

Kikao hicho kimekamilisha ziara ya viongozi wa chama hicho iliyoanza tarehe 9 Agosti huko kisiwani Pemba, ambapo kwa ujumla wamekutana na viongozi wa Mikoa 11 ya  kichama, Majimbo 50 pamoja na Matawi 682 ya chama hicho kwa Unguja na Pemba.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...