* Wampongeza Dk. Rweikiza kwa uwekezaji
WAZAZI na walezi wamepongeza Mkurugenzi wa shule za St Anne Marie Academy, dk. Jasson Rweikiza kwa uwekezaji kwenye elimu huku wakipongeza pia mafanikio ya shule ya St. Anne Marie Academy kwenye matokeo mbalimbali ya mitihani ya kitaifa na kuwataka walimu wasibweteke.
Wametoa pongezi hizo mwishoni mwa wiki wakati wa mahafali ya 17 ya kidato cha nne, yaliyofanyika shuleni hapo Mbezi Kimara kwa Msuguri jijini Dar es Salaam.
Akizungumza kwa niaba ya wazazi wengine, Anitha Umbula amesema wazazi wamefurahia maendeleo mazuri ya kitaaluma ya shule hiyo na mazingira mazuri ya shule hiyo huku akiwataka walimu wasibweteke.
Amesema kwa miaka karibu saba mfululizo shule hiyo imekuwa ikifanya vizuri kwenye mitihani ya kitaifa na kuingia kwenye kumi bora kitaifa na kuipelekea kuongoza Mkoa wa Dar es Salaam na Wilaya ya Ubungo.
“Haya si mafanikio madogo ni makubwa sana lazima tuwapongeze walimu na Dk. Rweikiza kwa uwekezaji mkubwa mnaoufanya kwenye shule hii lakini msibweteke kwa mafanikio haya endeleeni kuwania zaidi wanafunzi bila kuchoka,” amesema.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa shule hiyo ambaye pia ni Mbunge wa Bukoba Vijijini (CCM), Dk. Jasson Rweikiza ameomba wazazi waendelee kuiamini shule hiyo na kwamba sasa wamekuwa wakifanya maboresho makubwa kila mwaka lengo likiwa ni kuhakikisha wanafunzi wanaopitia shule hiyo wanapata matokeo mazuri kitaifa.
Amesema wana maktaba zilizosheheni vitabu ikiwa na kiyoyozi, maabara zenye vifaa kwa ajili ya sayansi kwa vitendo, kitengo cha udhibiti ubora cha ndani na bodi ya mitihani inayoratibu mitihani ya ndani ya shule.
Naye,Gladius Ndyetabula ambaye ni Mkuu wa shule hiyo, amesema kwenye matokeo ya darasa la saba mwaka 2017, wanafunzi wote 43 walioata wastani wa alama A na kuipelekea shule kuwa ya kwanza Wilaya ya Ubungo, ya pili Mkoa wa Dar es Salaam na ya nane kitaifa.
Amesema mwaka 2018 wanafunzi wote 59 walipata alama A na shule kuwa ya kwanza Wilaya ya Ubungo, ya kwanza Mkoa wa Dar es Salaam na ya sita kitaifa.
Ndiyetabura amesema kwenye matokeo ya kitaifa mwaka 2019 wanafunzi wote 99 walipata wastani wa alama A, na shule kuwa ya kwanza Wilaya ya Ubungo, ya kwanza Mkoa wa Dar es salaam na ya13 kitaifa.
Kwa mwaka jana wa 2020, wanafunzi wote 129 walipata alama A, ikawa ya kwanza Wilaya ya Ubungo, ya kwanza Mkoa wa Dar es Salaam na ya nane kitaifa.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...