WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan imedhamiria kutekeleza dhana ya uchumi jumuishi kwa vitendo kwa kuweka vipaumbele vitakavyowawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi.
Ameyasema hayo leo (Jumatatu, Oktoba 4, 2021) wakati wa ufunguzi wa Kongamano la Tano la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, jijini Dodoma. Amesema kuwa vipaumbele katika mipango ya Serikali vimekuwa katika utekelezaji wa shughuli za kiuchumi zinazowajumuisha moja kwa moja wananchi.
Waziri Mkuu ametaja baadhi ya vipaumbele hivyo kuwa ni pamoja na uimarishaji wa huduma za afya, hifadhi ya jamii, maji, umeme na utekelezaji wa mpango wa elimumsingi bila ada “Mtanzania mwenye afya, aliyeelimika na miundombinu wezeshi ni chachu kwa ukuaji uchumi wa nchi yetu.”
Amesema uwezeshaji wa uchumi jumuishi ni msingi wa kuhakikisha kunakuwa na ustawi endelevu kwa watu wote, ambapo Serikali imeandaa Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2025 ambayo pamoja na mambo mengine imeainisha mazingira wezeshi yatakayowezesha nchi kunufaika kiuchumi, kijamii, kisiasa na kiutamaduni.
Mheshimiwa Majaliwa amesema Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2025 pia imelenga kuhakikisha kunakuwa na viwango vya juu vya maisha, amani na umoja, utawala bora na uchumi ulioimarika wenye ushindani katika jamii.
Pia, Waziri Mkuu amesema Serikali imeandaa sera mbalimbali ambazo zimelenga kuhakikisha kunakuwa na maendeleo endelevu na uchumi jumuishi. “Kati ya Sera hizo ni Sera ya Taifa ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ya mwaka 2004 ambayo ni Sera kiongozi kwenye masuala ya kuwezesha wananchi kiuchumi, sera hiyo imeweka mikakati inayolenga kuhakikisha kwamba Watanzania wanashiriki kikamilifu katika uchumi wa nchi”
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...