Na. Edward Kondela

Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) imefanikiwa kukodisha maeneo kwa ajili ya wafugaji kufuga mifugo yao hali iliyochangia kupunguza migogoro baina ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi, huku ikiahidi kuendelea kushirikiana na wawekezaji wanaotaka kuwekeza katika ranchi hizo.

Akizungumza (13.10.2021) wakati wa kikao cha mwisho cha bodi ya wakurugenzi ya NARCO, mwenyekiti wa bodi hiyo Bw. Paul Kimiti amesema bodi hiyo ambayo imemaliza muda wake baada ya kukaa madarakani kwa miaka mitatu imeweza kwa kiasi kikubwa kusimamia na kuhakikisha wafugaji nchini ambao wana mifugo mingi wanapatiwa maeneo kwa mikataba katika ranchi hizo ili waweze kufuga mifugo yao na kukuza sekta ya mifugo nchini.

“Tumegawa maeneo ya ranchi takriban asilimia 75 na kubakiza asilimia 25 kwa kuwa wafugaji nchini wamekuwa na mifugo mingi na wanahitaji maeneo kwa ajili ya kufuga mifugo yao.” Amesema Bw. Kimiti

Aidha amesema katika kipindi cha miaka mitatu bodi ya wakurugenzi ya NARCO imeweza kuhakikisha maeneo ya ranchi za taifa yanawekewa mipaka ili kuzuia uvamizi wa maeneo hayo na kwamba zoezi hilo linaendelea katika maeneo mengine ambayo bado hayajawekewa alama hizo.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa NARCO Prof. Peter Msoffe amesema bodi ya wakurugenzi ya NARCO ambayo imemaliza muda wake imeweka misingi sahihi katika kufuatilia ukubwa wa maeneo ya ranchi, madeni na mashauri mbalimbali ambayo kwa kiasi kikubwa yameiwezesha NARCO kupata mafanikio zaidi.

Ameongeza kuwa bodi imekuwa ikitoa maelekezo kwa NARCO kuhakikisha inakaa na wawekezaji ambao wamepatiwa vitalu katika ranchi za NARCO na kuona namna ya kuboresha mikataba ili iweze kuzinufaisha pande zote mbili lengo ni kuhakikisha wafugaji wanapata fursa ya kupatiwa vitalu ili kufuga mifugo yao na kulima malisho ya mifugo.

Kwa upande wao baadhi ya wakurugenzi wa bodi ya wakurugenzi ya NARCO ambayo imemaliza muda wake wamesema kampuni hiyo imeweza kutatua kwa kiasi kikubwa migogoro baina ya wafugaji na watumiaje wengine wa ardhi kwa kuamua kukodisha vitalu kwenye ranchi za NARCO ili wafugaji waweze kufuga mifugo yao.

Wameongeza kuwa NARCO imekuwa ikifuga mifugo bora ambapo wananchi wanakaribishwa kwenda kununua mifugo hiyo ikiwemo ng’ombe na mbuzi ili kuwa na aina bora ya mifugo inayozalishwa katika ranchi hizo.

Pia wamewaalika wawekezaji kuwekeza katika ranchi za NARCO kwa ajili ya kulima malisho, kujenga majosho na miundombinu mbalimbali ili mifugo inayozalishwa katika ranchi hizo kuongezewa thamani.

  Mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi ya Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) Bw. Paul Kimiti akifafanua jambo kwa wakurugenzi wa bodi hiyo iliyokaa madarakani kwa miaka mitatu namna ilivyoweza kukodisha maeneo kwa ajili ya wafugaji kufuga mifugo yao hali iliyochangia kupunguza migogoro baina ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi. Kikao hicho kimefanyika katika makao makuu ya NARCO jijini Dodoma. (Picha na Edward Kondela, Afisa Habari - Wizara ya Mifugo na Uvuvi).


Wakurugenzi wa bodi ya wakurugenzi ya Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) wakiongozwa na mwenyekiti wa bodi hiyo Bw. Paul Kimiti wakiwa kwenye kikao cha mwisho cha bodi ambayo imekaa madarakani kwa kipindi cha miaka  mitatu. Kikao hicho kimefanyika katika makao makuu ya NARCO jijini Dodoma. (Picha na Edward Kondela, Afisa Habari - Wizara ya Mifugo na Uvuvi).

 

Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) Prof. Peter Msoffe akizungumza kando ya kikao cha mwisho cha bodi ya NARCO namna bodi ilivyoweka misingi sahihi ya kufuatilia ukubwa wa maeneo ya ranchi, madeni na mashauri mbalimbali ambayo kwa kiasi kikubwa yameiwezesha NARCO kupata mafanikio zaidi. (Picha na Edward Kondela, Afisa Habari - Wizara ya Mifugo na Uvuvi).

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...