Hifadhi ya Taifa Serengeti imeshinda Tuzo ya kuwa Hifadhi Bora Barani Afrika kwa mwaka 2021. Tuzo hiyo imetangazwa na Taasisi ya World Travel Awards (WTA) ya nchini Marekani kwa njia ya mtandao.
Hii ni mara ya tatu kwa Serengeti kushinda katika kundi la Hifadhi zinazoongoza kwa ubora zaidi Barani Afrika baada ya kushinda tuzo hiyo mwaka 2019 na 2020.
Serengeti imeibuka na ushindi katika shindano hilo lililoshindanisha hifadhi za Central Kalahari ya Botswana, Etosha ya Namibia, Kidepo Valley ya Uganda, Kruger ya Afrika Kusini na Maasai Mara ya Kenya.
Hifadhi ya Taifa ya Serengeti yenye ukubwa wa Kilometa za mraba 14,763 inajivunia umaarufu wa kuwa na misafara wa nyumbu wahamao zaidi ya milioni moja na nusu, aina 70 za wanyamapori wakubwa , mimea na spishi mbalimbali za ndege zipatazo 500 zinazopatikana kwa wingi katika hifadhi hiyo, madhari nzuri ya kuvutia pamoja na shughuli mbalimbali za utalii zinazovutia watalii wengi.
Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) linaishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wananchi, Wadau wa Utalii pamoja na wote waliotumia muda wao kupiga kura na kuifanya Serengeti kuwa mshindi wa Hifadhi Bora zaidi kwa Bara la Afrika kwa mara ya tatu mwaka 2021.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...