Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira Dkt. Samuel Gwamaka amewataka watanzania kujifunza kuwa na tamaduni ya kutunza mazingira na siyo mpaka Rais atukumbushe, wajibu ni wetu na Kamati za Mazingira ambazo zimetamkwa kwa mujibu wa Sheria kutekeleza majukumu yake.
Ameyasema hayo alipokuwa kwenye mkutano wa waandishi wa habari ofisi za NEMC Makao Makuu jijini Dar es salaam na kusema kuwa katika utekelezaji wa agizo la mheshimiwa Rais kuhusu ulinzi wa vyanzo vya maji na mabadiliko ya tabianchi, Baraza litashirikiana na Wakuu wa Mikoa kusimamia vyanzo vya maji.
‘’NEMC tumepewa nguvu ya Kisheria ambayo tutaitumia kuhakikisha kwamba tunashirikiana na Wakuu wa Mikoa kutekeleza agizo la
Mheshimiwa Rais. Aidha, hatutasita kupendekeza kwenye mamlaka husika kuchukua hatua stahiki kwa wale ambao tutabaini kabisa kwamba hawatekelezi majukumu yao ya kimazingira kwenye maeneo ambayo wamepewa mamlaka, tutapendekeza.’’
Aidha amewataka wanaofanya shughuli zozote za maendelezo kwenye vyanzo vya mito, kwenye maeneo oevu na kama ni lazima sana basi wafanye Strategic Environmental Assessment (Tathmini ya Kimkakati ya Utunzaji wa Mazingira).
‘’Fanya Strategic Environmental Assessment (Tathmini ya Kimkakati ya Utunzaji wa Mazingira) ili tuweze kubaini athari utakayoisababisha kwenye mazingira ni kiasi gani na huo mradi wako una faida sana kuliko hiyo hifadhi ambayo tunaitaka ambayo inastawisha ustawi wa waTanzania wote? Tutakapopima inamaana mamlaka husika zitajirizisha.’’
Amemaliza kusema kuwa siyo nia ya Baraza kuendelea kukaa kimya kuona tunaendelea kupata athari ya upungufu ya maji, athari ya uharibifu wa mazingira au uchafuzi wa mazingira katika maeneo mbalimbali, Sheria zipo na tutahakikisha mazingira yanaenziwa.
‘’Sheria zipo na adhabu zipo ambazo zinatambulika Kisheria lakini sasa hivi tunachohitaji ni ushirikiano na Serikali za Mitaa, Kamati za Mazingira kwenye maeneo husika zifanye kazi yake, na moja ya majukumu ya Kamati za Mazingira ni pamoja na kuchukua hatua ya kumfungia mtu mradi wake au kumpiga faini lakini pia kufunguliwa mashitaka na kufungwa, yote yapo kwenye Sheria.’’
Mkurugenzi Mkuu wa
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira Dkt. Samuel Gwamaka
akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za NEMC Makao Makuu
jijini Dar es Salaam.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...