Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) imetoa msaada wa mifuko ya saruji 920 (sawa na tani 46) yenye thamani ya sh mil 21 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni mawili katika shule ya Sekondari Kiriba iliyoko Halmashauri ya wilaya ya Musoma Mkoani Mara sambamba na msaada wa madawati 100 katika shule za Sekondari Libobe na Tangazo zilizopo Mkoani Mtwara ikiwa ni hatua ya benki hiyo katika kuunga mkono juhudi za serikali pamoja na wananchi katika kuboresha elimu hapa nchini.
Wakizungumza
kwenye hafla za kukabidhi misaada hiyo zilizofanyika mwishoni mwa wiki
katika shule hizo, Meneja wa benki ya NBC Tawi la Musoma Bi Sophia Lyimo
pamoja nae Meneja wa Benki ya NBC tawi la Mtwara Bi Editha Mwakatobe
walisema misaada hiyo inalenga kuunga mkono jitihada ambazo tayari
zinaendelea kuonyeshwa na serikali pamoja na wananchi katika maeneo
husika kwa kuboresha miundombinu ya elimu.
“Mifuko hii 920 ya
saruji tunayoikabidhi hii leo ni kwa ajili ya kusaidia ujenzi wa mabweni
mawili ya wasichana na wavulana katika Shule hii ya Sekondari Kiriba.
Wananchi na serikali wamefanikisha ujenzi wa maboma ya mabweni na sisi
tumeona tuwaunge mkono kwa kuwapatia saruji ili waweze kufanikisha
mpango huu muhimu unaolenga kuwasaidia wanafunzi wanaosoma hapa
wasitembee umbali mrefu kufuata elimu,’’ alisema Bi Lyimo.
Aliipongeza serikali kwa kutoa kiasi cha sh mil 60 kufanikisha ujenzi wa vyumba vya madarasa katika shule hiyo.
Akizungumza
kwenye hafla kama hiyo ya kukabidhi madawati 50 kwa ajili ya shule ya
sekondari ya Libobe iliyopo wilayani Mtwara, Meneja wa Benki ya NBC
tawi la Mtwara Bi Editha Mwakatobe alisema msaada ni sehemu ya msaada wa
madawati 100 unaotolewa na benki hiyo kwa shule hiyo Sekondari pamoja
na sekondari ya Tangazo iliyopo wilayani humo pia, lengo likiwa ni hilo
hilo la kuhakikisha wanasaidiana na serikali pamoja na wananchi katika
kuboresha mazingira ya elimu nchini.
“Lengo letu ni kuhakikisha
ndoto za watoto hawa kielimu zinafikiwa na pia kumuunga mkono Rais wetu
Mama Samia Suluhu Hassani katika utoaji wa elimu bora. Kwa hiyo
tunakabidhi madawati na viti hivi kwa ajili ya wanafunzi hawa kwa kuwa
ni furaha ya NBC kuona watoto wanaondokana na changamoto mbalimbali
zinazowakabili hasa katika swala la elimu” alisema Bi Mwakatobe.
Akizungumza
mara baada ya kupokea msaada wa viti na madawati kwa ajili ya Sekondari
ya Lipobe, Mkuu wa Wilaya ya Mtwara Bw Dunstan Kyobya pamoja na
kuishukuru benki hiyo kwa msaada huo alisema serikali imejipanga
kuhakikisha inamaliza changamoto za kielimu kwa kushirikiana na wadau
mbalimbali ikiwemo benki hiyo huku akitolea mfano shule hiyo ambayo
inaendelea na ujenzi wa madarasa mawili na ofisi ya walimu kupitia fedha
kiasi cha sh mil 40 zilizotolewa na serikali.
“Msaada huu
umekuja wakati muafaka kwasababu mahitaji ni viti na meza 72 kwa ajili
ya wanafunzi watakaonza masomo mapema mwakani…tunawashukuru sana benki
ya NBC kwa kutuunga mkono baada ya kuwapelekea maombi yetu na wao
hawakusita kutusaidia. Huu ni mwanzo tu kwa kuwa wiki ijayo Benki ya NBC
tena watatukabidhi msaaada kama huu kwa ajili ya Sekondari Tangazo,’’
alishukuru.
Zaidi Bw Kyobya aliiomba benki hiyo kuangalia
uwezekano wa kufungua tawi au huduma ya uwakala katika eneo hilo ili
kusaidia upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wananchi hao ambao licha
ya kupata fedha nyingi kupitia kilimo cha zao la korosho bado wamekuwa
wakibabiliwa na uhaba wa huduma za kifedha.
Kwa upande wao wakuu
wa shule hizo waliishukuru benki ya NBC kwa namna ilivyoguswa katika
kuchangia sekta ya elimu ikiwemo ujenzi na ukarabati wa vyumba vya
madarasa, mabweni na msaada wa madawati kwa kuwa jitihada hizo zimekuwa
zikisaidia kuongeza kasi ya serikali na wanachi wanaojitolea kuboresha
utoaji wa elimu hapa nchini.
“Binfasi nimefarijika sana kwa
msaada huu kutoka NBC na kwa kweli bado tunahitaji wadau wengine wajitoe
kusaidia kama walivyofanya benki hii. Tulituma maandiko ya kuomba
msaada kwao na tunashukuru waliyapokea na kuyafanyia kazi na matokeo
yake ndio haya tunayaona hii leo tunapokea msaada huu mkubwa wakilenga
kuunga mkono jitihada za wananchi na serikali yetu…asanteni sana NBC,’’
alisema Mtani Shadrack, Mkuu wa Shule ya Sekondari Kiriba, wilayani
Musoma.
Meneja wa Benki hiyo Kanda ya Kusini Bi Zubeider Haroun (wa kwanza kushoto) na Meneja wa Benki ya NBC tawi la Mtwara Bi Editha Mwakatobe (wa pili kushoto) wakikabidhi msaada wa madawati 50 kwa Mkuu wa Wilaya ya Mtwara Bw Dunstan Kyobya (wa tatu kulia) ikiwa ni sehemu ya msaada wa madawati 100 unaotolewa na benki hiyo kwa shule za sekondari Libobe na Tangazo zilizopo wilayani Mtwara kwa lengo la kuisaidia serikali pamoja na wananchi katika kuboresha mazingira ya elimu nchini wakati wa hafla ya makabidhiano hayo iliyofanyika Sekondari ya Libobe mwishoni mwa wiki. Wengine ni pamoja na Mkuu wa Shule ya Sekondari Libobe Bw Shadrack Nguvila (wa pili kulia) na Mwenyekiti wa Bodi ya shule hiyo Bw Ally Ngoda (Kulia)
Meneja wa benki ya NBC Tawi la Musoma Bi Sophia Lyimo (wanne kushoto) na maofisa wengine wa benki hiyo wakikabidhi sehemu ya msaada wa mifuko 920 (sawa na tani 46) ya saruji iliyotolewa na benki ya NBC kwa ajili ya kusaidia ujenzi wa mabweni mawili ya wasichana na wavulana katika Shule hiyo kwa uongozi wa shule ukiongozwa na Mkuu wa Shule hiyo Bw Mtani Shadrack (Katikati) wakati wa hafla ya makabidhiano iliyofanyika shuleni hapo mwishoni mwa wiki.Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Kiriba iliyoko Halmashauri ya wilaya ya Musoma Mkoani Mara sambamba na wafanyakazi wa Benki ya NBC tawi la Musoma na uongozi wa shule hiyo wakionesha sehemu ya msaada wa mifuko 920 (sawa na tani 46) ya saruji iliyotolewa na benki ya NBC kwa ajili ya kusaidia ujenzi wa mabweni mawili ya wasichana na wavulana katika Shule hiyo wakati wa hafla ya makabidhiano iliyofanyika shuleni hapo mwishoni mwa wiki.
Mkuu wa Wilaya ya Mtwara Bw Dunstan Kyobya (Kulia) sambamba na Meneja wa Benki hiyo Kanda ya Kusini Bi Zubeider Haroun (wa pili kushoto), Meneja wa Benki ya NBC Tawi la Lindi Bw Iovin Mapunda ( wa kwanza kushoto) pamoja na wanafunzi wa shule ya Sekondari Libobe iliyopo wilayani humo wakiwa wameketi kwenye madawati yaliyotolewa na Benki ya NBC kwa lengo la kuisaidia serikali pamoja na wananchi katika kuboresha mazingira ya elimu nchini wakati wa hafla ya makabidhiano hayo iliyofanyika shuleni hapo miwshoni mwa wiki.
Meneja wa Benki ya NBC Tawi la Lindi Bw Iovin Mapunda akizungumza pamoja na wanafunzi wa shule ya Sekondari Libobe iliyopo wilayani Mtwara wakati benki hiyo ilipokabidhi msaada wa madawati 50 kwa shule hiyo ikiwa ni sehemu ya msaada wa madawati 100 unaotolewa na benki hiyo kwa shule za sekondari Libobe na Tangazo zilizopo wilayani Mtwara kwa lengo la kuisaidia serikali pamoja na wananchi katika kuboresha mazingira ya elimu nchini. Anaemsikiliza pia ni Meneja wa Benki hiyo Kanda ya Kusini Bi Zubeider Haroun (Kushoto)
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...