Na Amiri Kilagalila,Njombe
MKUU wa mkoa wa Njombe Mhandisi Marwa Rubirya ametoa wito kwa wawekezaji wote wa ndani na nje ya mkoa huo waliowekeza kwenye uwekezaji wa kilimo cha Vanilla maarufu kama Vanilla Village uliopo katika kijiji cha Idunda halmashauri ya mji wa Njombe, kufika katika maeneo ya uwekezaji huo ili kuhakiki na kujiridhisha juu ya uwekezaji wao kama ni salama.
Rubirya ametoa wito huo katika mkutano wa sita wa baraza la biashara la mkoa wa Njombe uliofanyika leo kwenye ukumbi wa halmashauri ya mji wa Njombe.
“Serikali hatutarajii tufike mahala wananchi waanze kulalamika (Kuhusu uwekezaji wa Vannila Njombe) kama ambavyo tunaona kwenye vyombo vya habari,wote ambao wanadhani wana fedha zao huku wafike na kuhakiki ili kujiridhisha kuwa uwekezaji wao ni salama” Amesema Mhandisi Marwa Rubira
Mhandisi Rubirya amesema “Nitoe wito kuwataka wale wote waliowekeza fedha zao kwenye Vanilla,iwe wa hapa mkoani au walioko nje ya mkoa wetu,wafike Njombe ili kuhakiki vitalu nyumba vyao kuona kama fedha zao ziko salama.”
Aidha amesema serikali imesikia namna uwekezaji huo unavyohamasishwa kupitia vyombo vya habari lakini serikali inaendelea kulifanyia kazi zoezi la uwekezaji huo na kuja kutoa kauli hapo baadaye.
“Tumesikia hamasa kubwa ikiendelea kutangazwa kwenye kilimo cha Vanilla (Vanilla Village) Serikali ya mkoa inaendelea kulifanyia kazi hili hatuko kimya na mara baada ya kazi hii kukamilika,serikali itatoa kauli yake na hatua stahiki zitachukuliwa na mamlaka.” Amesema Rubirya
Kuhusu utaratibu wa uwekezaji,Rubirya amesema uongozi wa mkoa wa Njombe unawakaribisha wawekezaji wote wenye nia ya dhati ya kuwekeza kwa kuwa swala la uwekezaji ni fursa ambayo inatarajiwa kulete neema kwa muwekezaji na kwa mwananchi lakini uongozi hauta weza kuwavumilia wawekezaji ambao badala ya kuleta neema,uwekezaji wao unazua taharuki,hofu ama ulaghai.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...