

KAIMU Mkurugenzi wa Idara ya Miliki Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) Said Mndeme ameridhishwa na kasi ya ujenzi wa mradi wa nyumba 3500 na nyumba 20 za viongozi zinazojengwa Jijini Dodoma na Wakala huo.
Akizungumza na Waandishi wa Habari leo Desemba 3,2021 Jijini Dodoma mara baada ya kukagua ujenzi wa nyumba hizo,Kaimu Mkurugenzi huyo ameridhishwa na jinsi Wakala huo ulivyojipanga kutekeleza miradi hiyo kwa kuwa na vifaa vya kutosha na vya uhakika.
“Tumeridhika kwa jinsi ambavyo wamejipanga tuna Cementi ya kutosha nondo za kutosha haya ni maono ya wakala,hatuna sababu ya kuwa na vikwazo vyovyote binafsi nimeridhika na nimefurahi katika kuhakikisha tunapunguza gharama na ubora unakuwa mzuri mashine ya kisasa ya kuchakata zege.
“Tumeona Kiwanda kingine cha uzalishaji wa tofali hii itatisaidia tofali zenye ubora tumeambiwa kiwanda kinauwezo wa kuzalisha tofali 6000,”amesema.
Amesema mradi wa Nzuguni unaenda kwa kasi ambapo zitajengwa nyumba 3500 ambapo amedai awamu ya kwanza zinajengwa nyumba 150 na kwamba nyumba 86 zimeanza kujengwa.
“Nyumba hizi 3500 zitakuwa ni za kisasa kutakuwa na ujenzi maghorofa 100 na nyumba kubwa 200 na nyumba za saizi ya kati 1400, maghorofa yatakuwa nyumba tofauti tofauti 800 na za size za chini nyumba 1000.
Aidha,amesema katika eneo hilo kutakuwa na huduma za kijamii ambapo kutajengwa shule za awali tano,nyumba za ibada misikiti na makanisa,Soko na kituo cha biashara.
Kuhusiana na nyumba 20 za viongozi katika eneo la Kisasa Jijini Dodoma,Kaimu Mkurugenzi huyo wa Miliki amesema zimeboreshwa na kuongezewa ubunifu ikiwa ni pamoja na vyumba vyote kuwa Master bedroom
“Lakini tumeona jitihada kubwa ambazo zimefanyika nyumba hizi zinajengwa katika nyumba 300 katika eneo la Kisasa lakini nyumba hizi sasa hivi zimeboreshwa kwa kiasi kikubwa Kwanza nyumba hizi muonekano ni tofauti na zile nyumba 300 ambazo zilijengwa za sasa hivi kila chumba kina choo,”amesema.
Kwa upande wake,Kaimu Meneja Maendeleo ya Miliki TBA,Suzan Ulula amesema wanaamini watafikia malengo ambayo wamejiwekea ikiwa ni pamoja na kukamilisha kwa wakati ujenzi wa nyumba hizo.
“Baada ya kutembelea Nzuguni na Kisasa tunaamini tutafikia malengo wakala ambayo imeyaweka kwa watumishi wa Serikali.Kwa mkoa wa Dodoma tunamaeneo mengine Iyumbu na katika Mikoa mbalimbali Arusha na Dar tunategemea tutaendelea na sehemu zingine,”amesema.
Naye,Msimamizi wa Mradi wa ujenzi wa nyumba 3500 Nzuguni Jijini Dodoma,Fedrick Jackson amesema ujenzi huo ulianza Oktoba 25,2021 ambapo amedai matarajio ni kwa nyumba zote 150 ziwe zimekamilika Septemba 30 mwakani.
“Kwa matarajio ya miezi mitatu mitatu kwa nyumba 50 lakini tunajaribu kukimbizana ili tuzikamilishe nyingi kwa wakati mmoja hizi nyumba 86 ambazo tumeanza nazo mwezi wa tatu mwishoni kuelekea wanne mwanzoni tunatakiwa tuwe tumeishazimaliza.
“Lakini wakati huo zile nyumba 64 ambazo zitatutimizia nyumba 150 zinatakiwa ziwe mpaka mwezi wa sita ziwe zimekamilika.Hapa kila kitu kimepimwa maabara na namna ujenzi unavyokuwa tunasimamia na kupitia mara kwa mara kwa maana kile cha maabara tunakipeleka kupimwa,”amesema.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...