Toleo la 20 la mbio za Kilimanjaro Premium Lager Marathon 2022 limezinduliwa mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro, ikiwa ni takribani mwezi mmoja kabla ya kufanyika mbio hizo na ambazo zinasubiriwa kwa hamu kubwa.

Hafla hiyo iliyowakutanisha wadau mbalimbali, iliandaliwa na Hoteli ya Kibo Palace – kampuni ambayo ni moja ya wadhamini wenza wa mbio za Kilimanjaro Premium Lager Marathon.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Stephen Kagaigai aliwapongeza wadhamini na waandaaji wa mashindano hayo kwa kuhakikisha mbio hizo muhimu katika kukuza sekta ya michezo na uchumi na ambazo zimekuwa kivutio kwa wadau wengi wa michezo yanakuweko kwa miaka 20 sasa.

Wadhamini katika hafla ya maadhimisho haya ya miaka 20 ni pamoja na Kilimanjaro Premium Lager (Mdhamini Mkuu) Tigo (21km) na Grand Malt (5km).

Wadhamini wa meza za maji ni pamoja na Absa Tanzania, Unilever Tanzania, TPC Sugar, Simba Cement na Kilimanjaro Water. Wasambazaji rasmi ni GardaWorld Security, Keys Hotel, Kibo Palace Hotel, CMC Automobiles na Surveyed Plots Company Ltd (SPC).

"Hili ni tukio kubwa ambalo linaunufaisha Mkoa ya Kilimanjaro, Mikoa jirani na Taifa kwa ujumla kwani kuna fedha nyingi za kigeni zinazopatikana kutokana na shughuli wanazofanya wageni wanaokuja nchini kabla na baada ya mbio za marathon", alisema Mkuu wa Mkoa.

Aliendelea kusema kuwa Serikali ya Mkoa itaendelea kushirikiana kwa karibu na waandaaji na wadhamini wa mbio hizo ili kuhakikisha tukio hili linaendelea kukua lengo kuu likiwa ni kuboresha utalii kupitia michezo hapa nchini, ambapo alitoa wito kwa wadau wengine wa michezo kuiga kazi nzuri zinazofanywa na wandaaji wa  mbio za Kilimanjaro Marathon.

"Tunawashukuru kwa jinsi mlivyojipanga sana kwani hii inatupa wakati rahisi kama Serikali kutoa ushirikiano wetu kutokana na ukweli ya kuwa mmejipanga vyema huku mkiishirikisha Serikali ya Mkoa; hili linatuweka katika nafasi nzuri na rahisi zaidi katika kuhakikisha kuna usalama wa uhakika kabla na baada ya mbio za Kilimanjaro Marathon”, alisema.

Kwa upande wake, Meneja wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, Irene Mutiganzi, ambaye pia ni Meneja wa Chapa ya Grand Malt, alisema maadhimisho ya 20 ya mbio za Kilimanjaro marathon ni mafanikio makubwa haswa ikitiliwa maanani ya kuwa Kilimanjaro premium lager imekuwa mdhamini mkuu wa mbio hizo tangu kuasisiwa kwake miaka 20 iliyopita.

“Mbali na kuwa mashindano ya kimataifa yaliyojijengea umaarufu mkubwa, sisi kama wadhamini wakuu pia tumehamasishwa kujitolea zaidi kutokana na mbio hizo kuchangia kwa kiasi kikubwa kukua kwa sekta ya utalii  na utamaduni wa Mtanzania kwa ujumla”, alisema.

Alisema wao kama wadhamini wakuu wamejipanga vyema kwa ajili ya maadhimisho ya miaka 20 ya Kilimanjaro Premium Lager Marathon ambayo yatahusisha matukio ya kusisimua katika wiki nzima ya kuelekea mbio hizo ambapo alisema jumla ya shilingi milioni zimetengwa kwa ajili zawadi.

Irene aliendelea kusema kuwa washindi wa kwanza kwa upande wa wanaume na wanawake kwa mbio za kilomita 42 watazawadiwa shilingi milioni 4 kila mmoja na kwamba Mtanzania mwanamume au mwanamke atakaeshika nafasi ya kwanza katika mbio za kilomita 42 atapata zawadi ya ziada ambayo alisema ni motisha ya Tsh 1.5 m kila mmoja.

Aidha alitoa wito kwa wanaotarajia kushiriki mbio hizo kuhakikisha wanajiandikisha mapema kupitia mtandano wa www.kilimanjaromarathon.com na kupitia TigoPesa kwa kupiga *149*20#.

Irene pia alitoa wito kwa washiriki wa mbio za 5km (Mbio za kujifurahisha) ili kuepuka kukosa fursa hiyo pale namba zitakapokwisha kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.

Akiongea katika hafla hiyo Mkurugenzi wa Tigo Kanda ya Kaskazini, Henry Kinabo alisema: “Sisi tukiwa ni wadhamini wa mbio za kilomita 21, maarufu kama Tigo Kili-Half marathon kwa zaidi ya miaka 7 sasa, tunatarajia mbio za mwaka huu zitakuwa ni za kusisimua, ambapo tunatarajia washiriki zaidi ya 5,000 kutoka ukanda mzima wa Bara la Afrika kutokana na kuongezwa kwa thamani ya zawadi za washindi”.

Kinabo aliwapongeza waratibu wa mbio hizo kwa mafanikio waliyopata kwa miaka 20 sasa, ambapo alitoa wito kwa wale wanaotarajia kushiriki mbio hizo kutumia mtandao wa Tigo Pesa kujiandikisha kwani jambo hilo limerahisisha mchakato mzima kujiandikisha kwa ajili ya ushiriki wa mbio hizo.

"Wanaotarajia kushiriki mbio hizo na ambao hawana laini za Tigo wanaweza kuwaomba marafiki zao ili wajiandikishe kwa ajili ushiriki wa mashindano hayo”, alisema.

Kwa upande wao, waandaji wa hafla hiyo walitoa wito kwa washiriki kujiandikisha mapema kabla zoezi la kujiandikisha kusitishwa ifikapo Februari 7, 2022 au tiketi zitakapokwisha, ambapo walisema uandikishaji wa mio za kilomita 5 utaendelea hadi februari 26, mwaka huu.

“Kutakuweko na vituo vya kuchukulia namba za ushiriki ambapo Dar es Salaam itakuwa ni eneo la Mlimani City, Arusha hoteli ya Kipo Palace na Moshi katika chuo kikuu cha ushirika Moshi (MoCU)”, ilisema taarifa ya waandaaji hao na kuongeza kuwa zoezi hilo litaanza mapema Februari, mwaka huu.

Kwa mujibu wa waandaaji hao, kwa mara ya kwanza kutakuweko na maonesho yanayojulikana kama Kili Expo (The People's Expo) ambapo wadhamini na wadau wengine wa mbio hizo watapata fursa ya siku tatu za kuonyesha bidhaa na huduma wanazotoa, maonyesho ambayo yanatarajiwa kufanyika kati ya Februari 24-26, 2022, katika viwanja vya MoCU.

"Maonyesho haya pia linakusudiwa kuwapa umma uzoefu wa muda mrefu wa mbio za Kili Marathon; pia kwa mwaka huu wanaotarajia kushiriki mbio hizo watapata fursa ya kuchukua namba zao za ushiriki eneo la chuo kikuu cha Ushirika badala ya eneo la hotel kama ilivyokuwa miaka ya nyuma”, ilisema taarifa hiyo ya wandaaji.

Mbio za Kilimanjaro Premium Lager Marathon, zinatarajiwa kufanyika Jumapili ya Februari 27, 2022, katika viwanja vya Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi (MoCU), ambapo zimeandaliwa na taasisi ya Kilimanjaro Company Limited na kuratibiwa na wadau wa hapa nchini kampuni ya Executive Solutions Limited.
Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Stephen Kigaigai (wa pili kushoto) na Meneja wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, Irene Mutiganzi wakikata utepe kuashiria uzinduzi wa mbio za 20 za Kilimanjaro Premium Lager Marathon –Moshi katika viwanja vya Kibo Palace Homes huku wadau wengine wakishuhudia.





Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...