Na Said Mwishehe, Michuzi TV
MAKADA wa Chama Cha Mapinduzi( CCM) wameendelea kuchukua fomu za kuwania nafasi ya Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwemo binti wa miaka 32 anayefahamika kwa jina la Ester Stephano Makazi anayeishi Wilaya ya Temeke mkoani Dar es Salaam.
Hadi jana Januari 12,2022 jumla ya waliokuwa wamechukua fomu ya kuwania nafasi hiyo walikuwa 30 na leo Januari 13 mwaka huu wameendelea kuchukua kwa ajili ya kuomba ridhaa ndani ya CCM kupitishwa na hatimaye kupigiwa kura na wabunge.
Akizungumza leo baada ya kuchukua fomu ya kuwania U-Spika Ester Makazi amesema amejitosa kuwa nafasi hiyo kwa kuamini anao uwezo wa kutosha huku akielezea uwezo wake wa muda mrefu wa kukitumikia Chama hicho ,hivyo anaomba ridhaa ya Chama chake.
"Nimejitafakari na nimeona ninatosha kukalia kiti hicho , mimi ni binti, ni msichana lakini najiamini na bahati nzuri wanawake ambao wapo kwenye uongozi wameonesha uwezo mkubwa wa kuongeza.Mama yetu Rais Samia Suluhu Hassan ni mfano kwetu, na ni wazi wanawake tunaweza,"amesema.
Kuhusu uzoefu wake ameeleza katika chama amemewahi kuwa mjumbe katika Tawi langu la Toangoma na kufanya shughuli za kichama na maendeleo hivyo amejipima akaona anaweza kugombea nafasi hiyo."Kuhusu elimu nina Shahada ya Sheria Chuo cha Tumaini."
Kwa upande wake Mohammed Mmanga, ambaye ni Mjumbe wa Kamati Kuu Wilaya ya Temeke mkoani Dar es Salaam amechukua fomu ya kuwania nafasi hiyo huku akieleza kuwa anao uzoefu wa muda mrefu kwani ameanzia chipukizi na ameendelea kukua akiwa ndani ya Chama.
Mmanga amesema endapo atafanikiwa kuchaguliwa kuwa Spika atatumia kila aina ya maarifa aliyonayo kuhakikisha anasimamia maslahi ya Chama, Serikali na Taifa kwa ujumla.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...