*Ni kile kinachirushwa na Luninga ya Star TV
Na Chalila Kibuda,Michuzi Tv
MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imekisimamisha kwa muda wa miezi mitatu kipindi cha 'Efatha Ministries' kinachorushwa na Star Televisheni kwa kutoa taarifa za kupotosha umma zisizokuwa na uthibitisho wowote na kuleta sintofahamu kwa wananchi.
Mwenyekiti wa Kamati hiyo Habbi Gunze alitoa taarifa hiyo kwa waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.
Alisema Disemba 26 mwaka jana Star TV ilirusha matangazo ya moja kwa moja ya mahubiri ya Askofu Josephat Mwingira kutoka katika kanisa la Efatha lililopo eneo la Mwenge jijini Dar es Salaam.
Alisema wakati wa matangazo hayo ya moja kwa moja , Askofu Mwingira alitoa taarifa hizo zinazoweza kujenga chuki na kuleta taharuki miongoni mwa watanzania kinyume na kanuni za utangazaji.
Akimnukuu Mwingira alisema " Yaani kwa mfano mimi nipo kwenye hii nchi ya Tanzania leo hii nikimwambia Mungu wacha hawa watu wachapane kwa sababu wanaibiana kura watachapana damu itamwagika isiyo ya kawaida watachapana kweli kweli.
" Lakini huwa namwambia Bwana wee wacha hao wezi waibe mpaka siku utakapowakamata mwenyewe," alisema.
Alisema kitendo hicho cha kuutangazia umma Maudhui yenye taarifa za kupotosha zisizokuwa na uthibitisho wowote, zinaweza kujenga chuki na kuleta taharuki miongoni mwa watanzania, Star Televisheni inatuhumiwa kukiuka kifungu cha 11 ya kanuni za Mawasiliano ya kielektroniki na Posta.
Aidha Kamati hiyo imetoa onyo kali na kuitaka Televisheni ya Star TV kuwaomba radhi watazamaji wake na umma kwa ujumla kupitia kituo chake kilichotumika kurusha Maudhui hayo kwa Siku tatu mfululizo kuanzia leo hadi 27 Januari mwaka huu.
Awali Mwenyekiti huyo alitoa ushauri kwa Televisheni hiyo kuhakikisha inakuwa na usimamizi makini wa vipindi vyake vinarushwa kwa matangazo ya moja kwa moja.
Pia kuhakikisha inazingatia misingi, sheria, kanuni, maadili na weledi katika kusimamia, kuhariri na kutoa Maudhui katika kituo chao cha utangazaji ili kuepuka kutangaza Maudhui yasiyofaa.
Alivikumbusha vyombo vyote vya utangazaji kuzingatia usimamizi makini wa matangazo yao ya moja kwa moja kwa mujibu wa kanuni ya 37 ya kanuni za Mawasiliano ya kieletroniki na Posta.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...