MRATIBU wa mfuko wa Maendeleo ya jamii nchini(Tasaf)mkoa wa Ruvuma
Xsaveria Mlimira,amewaasa wanufaika wa mpango wa kunusuru kaya maskini
wanaopokea ruzuku ya fedha kutoka Tasaf kuanzisha miradi ya kimkakati
na biashara ndogo ndogo ili kuwaingizia kipato.
Mlimira ameyasema hayo kwa nyakati tofauti,wakati akizungumza na
wanufaika wa mpango huo katika kijiji cha Chikomo na Chiwana kata ya
Chiwana Halmashauri ya wilaya Tunduru mkoani humo.
Alisema, walengwa wakiwa na miradi ya kiuchumi kama ya ufugaji na mama
lishe wataweza kumudu maisha yao ya kila siku bila shida, hata pale
mpango wa kupokea fedha kutoka Serikalini utakapokoma(kumalizika).
Amewashauri kuanzisha vikundi vya kupeana na kukopeshana ambavyo vina
umuhimu mkubwa kwenye familia na jamii hasa yenye kipato cha chini
kupata fedha za kujikimu kimaisha na kufanya mambo mbalimbali ya
maendeleo.
Aidha,amewakumbusha kujiwekea akiba na kutumia fedha hizo kwa malengo,
badala ya kuzielekeza katika anasa ikiwamo ulevi na wanaume kuoa mke
zaidi ya mmoja kwani tabia hiyo inachangia kuongeza umaskini katika
jamii.
Alisema, malengo ya Serikali kutoa fedha kupitia Tasaf ni kuona kila
kaya ina uwezo wa kupata milo mitatu kwa siku,wananchi wapate huduma za
matibabu na watoto wanaosoma wapate mahitaji ya shule na mavazi.
Akizungumzia changamoto ya walengwa kukosa kadi za Bima ya afya licha ya
kuchangishwa fedha Mlimira, amewatoa hofu na kueleza kuwa tatizo hilo
litakwisha kwani liko ya chini ya uwezo wake na kuwataka kuendelea
kuchangia ili waweze kupata matibabu.
Baadhi ya wanufaika wa Tasaf, wameishukuru Serikali ya awamu ya sita
kwa kuona umuhimu wa kuendelea kutoa fedha ambazo zimesaidia kuboresha
maisha yao.
Hadija Hamis alisema, kupitia fedha za Tasaf amefanikiwa kujenga nyumba
ya matofari na kuezeka bati na kuanzisha biashara ya kufuga kuku ambao
unamwezesha kupata fedha za kujikimu na familia yake na kuiomba Serikali
kuendelea na mpango huo.
Hata hivyo mlengwa mwingine Said Mapepe alisema,walengwa wamekuwa
wakitoa fedha kwa ajili ya kujiunga na mfuko wa afya ya jamii(CHF)lakini
baadhi yao bado hawajapa kadi za matibabu hivyo kupata usumbufu pindi
wanapofika kwenye vituo vya kutolea huduma za afya.
“walengwa tunatoa fedha kwa ajili ya kujiunga na CHF,lakini tangu
tulipoanza kuchangia mwaka 2020 hatujapata kadi zetu za
matibabu”alisema Mapepe
Kwa upande wake Afisa Mtendaji wa kijiji cha Chiwana Issa Simba amekiri
kuwepo kwa tatizo hilo na kueleza kuwa,wanaohusika ni waratibu wa CHF
ngazi ya wilaya na mkoa ambao ndiyo wanaokusanya fedha kutoka kaya
maskini.
Simba,amewakumbusha wakazi wa kijiji hicho kuweka akiba ya chakula kwa
ajili ya matumizi ya familia zao ili kuepuka kukumbwa na janga la njaa.
Mratibu wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii Nchini(Tasaf)mkoani Ruvuma Xsaveria Mlimira kulia akimsikiliza mlengwa wa kaya maskini wa kijiji cha Chikomo kata ya Chiwana Halmashauri ya wilaya Tunduru Ali Wadali kuhusiana na changamoto mbalimbali inayowakabili walengwa wa mfuko huo ikiwamo kuchelewa kwa ruzuku na kukosekana kwa kadi za matibabu.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...