Waziri wa Elimu, Sayansi na
Teknolojia, Mhe Prof Adolf Mkenda (kulia) akipokea nyaraka za ofisi kutoka kwa
aliyekuwa Waziri wa wizara hiyo, Prof Joyce Ndalichako ambaye ni Waziri wa Nchi
Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu wakati wa makabidhiano
ya ofisi yaliyofanyika tarehe 13 Januari 2022, jijini Dodoma. (Picha Zote Na Mathias Canal)
Waziri wa Elimu, Sayansi na
Teknolojia, Prof Adolf Mkenda akizungumza na Viongozi mbalimbali wa wizara hiyo
wakati wa hafla ya makabidhiano ya nyaraka za ofisi iliyofanyika jijini Dodoma,
tarehe 13 Januari 2022.
WAZIRI wa Elimu, Sanyansi na Teknolojia Mhe Prof Adolf Mkenda amekabidhiwa rasmi Ofisi na aliyekuwa Waziri wa wizara hiyo Prof Joyce Ndalichako huku akiwasisitiza watumishi wa wizara hiyo kufanya kazi bila nidhamu ya uoga.
Kauli hiyo ameitoa jijini Dodoma tarehe 13 Januari 2022 mara baada ya kukabidhiwa ofisi zikiwemo nyaraka mbalimbali na taarifa zinazoeleza kilichofanyika ndani ya wizara na Profesa Ndalichako ambaye kwa sasa ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu
Profesa Mkenda amesema anafahamu uchapakazi wa Profesa Ndalichako ambao umefikisha wizara ilipo kwa sasa na kusababisha mafanikio makubwa.
"Tuliobaki hapa tufanye kazi bila nidhamu ya uoga na kwa ujasiri na kabla ya kufanya maamuzi ya jambo fulani tuambiane ukweli pale tunapokosea, kila mtu awe anazungumza na hata kama mmeona mimi nimekosea nikosoeni kuwa ulisema hiki lakini ukweli ni huu ikishindikana omba miadi ya kuonana na mimi," Amekaririwa Waziri Mkenda
Profesa Mkenda amesema kuwa kwa sasa miongozo ipo ikiwemo ya kubuni vitu vipya maana ipo sayansi na Teknolojia mbalimbali nchini na michakato ipo na inaendelea na kazi kubwa imefanyika ikiwemo mapitio ya mitaala.
Kwa upande wake, Profesa Ndalichako amesema kuwa Wizara ya elimu inahusika na utungaji Sera za elimu ngazi zote za awali na vyuo vikuu na usimamizi wa ithibati ya elimu.
"Wizara ina Taasisi 30 zinazojishugulisha na masuala mbalimbali hivyo hakikisha unashirikiana nazo kwenye utekelezaji wa majukumu yako ili isonge mbele, Kuna changamoto ya wahadhiri nchini lakini fedha zimetengwa kusomesha wataalamu hao ili wawepo wa kutosha," Amesisitiza Prof Ndalichako
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...