Abdullatif Yunus - Michuzi TV Kagera.
Vijana Watanzania Waishio Nje na Ndani ya Nchi, Wameshauriwa kuwekeza Nyumbani pindi wapatapo Fursa, ili kuacha alama ya Kukumbukwa ikiwa ni sehemu ya kuleta maendeleo katika jamii inayowazunguka, kama walivyofanya Waasisi wengi walioacha alama katika maeneo mbalimbali aliwemo Hayati Askofu Dkt. Samson Mushemba
Ushauri huo umetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI Mhe. Innocent Bashungwa wakati wa Hotuba yake aliyoitoa katika Maadhimisho ya Kumbukizi ya Hayati Askofu Dkt. Samson Mushemba yaliyofanyika Aprili 09, 2022 shuleni Mushemba Trinity.
Waziri Bashungwa amesema kuna haja ya Vijana kuanza kufikiria kuishi Kijijini kuliko kubanana Mijini huku akitolea mfano Viongozi wastaafu na Viongozi wa Dini kama Askofu Dkt. Benson Bagonza ambaye mara nyingi amekuwa akifuatilia mambo mengi yanayotokea Duniani akiwa Kijijini kwake anapoishi.
"....Mkoa wetu ni Mzuri na Kijijni ni Pazuri, Tuwekeze Nyumbani, kupitia Wazee hawa wananihamasisha kurudi Kijijini, hata baada ya kumaliza Utumishi wangu nitarudi kuishi Kijijini nitoe Wito kwa Vijana wenzangu wa DIASPORA, hata wale mnaoishi Arusha, Dar na kwingine tukumbuke kuwekeza Nyumbani.." amesema Bashungwa.
Aidha Waziri Bashungwa ameshukuru Uongozi wa Mushemba Foundation kwa namna ambavyo wameamua kuwekeza Nyumbani na hasa kujali zaidi katika kundi la Watu wenye uhitaji wa Elimu, ambapo kwa kufanya hivyo ni kuunga mkono Juhudi za Serikali ambayo inahakikisha inatoa Elimu bure kwa Watoto wa Kitanzania ambapo mpaka sasa zaidi ya Trioni 1.43 zimekwishatolewa katika kutekeleza sera ya Elimu bila malipo, hivyo kupitia juhudi hizo Serikali pamoja na yeye Binafsi watakuwa tayari kushirikiana na Taasisi katika yale ambayo yatazidi kuisogeza mbele, huku akimuagiza Meneja wa Tarura Wilaya ya Bukoba kufanya Tathmini ya kipande cha Barabara inayoingia Shuleni Mushemba, chenye urefu wa Mita 700 ambacho kimeonekana kuwa kero kishughulikiwe mara moja.
Maadhimisho hayo ynafanyika ikiwa ni Kumbukizi ya Miaka Miwili ya Kifo cha Muasisi wa Mushemba Foundation Hayati Dkt. Samson Mushemba aliyeanzisha Shule ya Mushemba Trinity kwa Ajili ya kuwapatia Elimu bure Watoto wanaotoka katika mazingira magumu.


Baba Askofu Alex Malasusa akitoa neno wakati wa maadhimisho ya Mushemba Day, Askofu Malasusa ndiye aliyeongoza Misa ya Kumuombea Hayati Askofu Dkt. Samson Mushemba.







Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...