Na Mwandishi Wetu, Dodoma

BODI ya Usajili wa Makandarasi (CRB), inatarajia kuwakutanisha makandarasi na wadau mbalimbali wa sekta ya ujenzi mkoani Dodoma kwaajili ya kujadili mchango wa Makandarasi katika Uchumi wa Tanzania.

Mkutano huo wa siku mbili wa mashauriano utafanyika katika ukumbi wa Jakaya Kikwete Convention Center mkoani Dodoma kuanzia Mei 12 na 13 mwaka huu wa 2022.

Kwa mujibu wa Msajili wa Bodi hiyo, Mhandisi Rhoben Nkori mkutano huo utawashirikisha wadau wote wakiwemo waajiri, wataalamu washauri, wahandisi na wabunifu majengo.

Amewataja wengine kuwa ni wakadiriaji majenzi, watunga sera za uwezeshaji wananchi kiuchumi na wataalamu mbalimbali katika sekta ya ujenzi na kwamba kauli mbiu ya mwaka huu ni ‘Umuhimu na Mchango wa Makandarasi katika uchumi wa Tanzania’.

“Mkutano huu wa mashauriano ambao unafanyika kila mwaka ni muhimu sana kwa maendeleo ya sekta ya ujenzi kwa ujumla wake. Wataalamu wa sekta mbalimbali wanakaribishwa kujisajili mapema ili washiriki katika mkutano,” amesema Mhandisi Nkori

Mhandisi Nkori ametaja mada zitakazotolewa kwenye mkutano huo kuwa ni mchango wa makandarasi katika uchumi wa Tanzania na changamoto zinazoathiri mchango wa makandarasi katika uchumi wa nchi.

Ametaja mada zingine kuwa ni masuala ya kodi ya kuzingatiwa kwa makandarasi ili kuboresha mchango wao katika uchumi wa taifa na fursa katika sheria na kanuni za manunuzi ya umma kuwezesha mchango wa makandarasi wa ndani.

Aidha, ametaja mada zingine zitakazotolewa kuwa ni utatuzi wa migogoro katika ununuzi wa umma na kwamba kwenye mkutano huo pia kutakuwa na maonesho ya teknolojia, huduma na vifaa vya ujenzi.

Akizungumza kuhusu maonesho, Mhandisi Nkori amesema CRB inayakaribisha mashirika na makampuni mbalimbali binafsi na ya umma kwenda kuonesha teknolojia, bidhaa, vifaa na zana za ujenzi.

“Mkutano utakuwa na wadau wengi wa sekta ya ujenzi hivyo tunawakaribisha watu binafsi na mashirika kuja kuonesha bidhaa walizonazo kwa washiriki wa mkutano huu wa mwaka,” amesema Mhandisi Nkori
Msajili wa Bodi ya Usajili wa Makandarasi (CRB), Mhandisi Rhoben Nkori akizungumza kwenye mkutano wa makandasi uliofanyika jijini Mbeya mwaka jana

Mwenyekiti wa Bodi ya Usajili wa Makandarasi (CRB), Consolata Ngimbwa akizungumza kwenye mkutano wa makandarasi uliofanyika hivi karibuni mkoani Dodoma.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...