* Ni zoezi la 'Temeke Afya Check' lililolenga kusogeza huduma za kibingwa kwa wananchi 
MENEJIMENTI
 ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Temeke kwa kushirikiana na ofisi ya 
Mkurugenzi wa Manispaa na Mkuu wa Wilaya ya Temeke wameandaa timu ya 
madaktari bingwa itakayoendesha zoezi la  upimaji wa afya na matibabu 
bila malipo kwa wananchi wa Temeke kwa lengo la kuwasogezea wananchi 
huduma za kibingwa kadri inavyowezekana.
Akizungumza
 na Michuzi TV leo jijini Dar es Salaam Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya 
Rufaa ya Mkoa wa Temeke Dr. Joseph Kimaro amesema, zoezi hilo kubwa la 
'Temeke Afya Check'  litafanyika katika hospitali hiyo kuanzia tarehe 9 
hadi 11 Septemba mwaka huu na huduma za upimaji wa afya bila malipo kwa 
wananchi wote wa Temeke zitatolewa kwa kushirikiana madaktari bingwa 
kutoka ndani na nje ya hospitali ya Temeke.
''Hii
 ni fursa nzuri kwa wananchi wa Temeke kupata huduma za kibingwa na 
tunafanya zoezi hili kwa lengo la kuhakikisha huduma za kibingwa 
zinawafikia wananchi wengi kwa kadri inavyowezekana....Tunafahamu wapo 
wananchi wengi wenye matatizo mbalimbali na wanahitaji kuonana na 
madaktari bingwa hivyo tukaona tushirikiane na wadau mbalimbali na 
kutoa huduma hii bila malipo kwa wananchi wetu ili waweze kunufaika na 
jitihada za Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu 
Hassan katika kuboresha huduma za afya.'' Amesema. Dr. Kimaro.
Pia
 amesema gharama za matibabu hayo yatakayotolewa bure kwa wananchi 
yatagharamiwa na hospitali pamoja na wadau mbalimbali zikiweo kampuni za dawa 
(Pharmacy) ambao watatoa dawa,  vitendanishi na wataalam pamoja na kulipa 
gharama za matibabu kwa wagonjwa watakaotakiwa kufanyiwa upasuaji na 
ushirikiano huo na wadau umelenga kusogeza huduma za kibingwa karibu na 
wananchi pamoja na kuunga mkono jitihada za Serikali ya kuhakikisha 
wananchi wanakuwa na afya bora ya kuzalisha na kuchangia ukuaji wa 
uchumi wa Taifa.
Dr.
 Kimaro amesema, zoezi hilo limefadhiliwa kwa ukaribu na wadau 
mbalimbali wakiwemo MDH, Haidery Plaza, Shamshu pharma, MFAA, Nebula, 
CCBRT, TAI, Consolation Medicare pamoja na Tindwa medical Health ambao 
watatoa madaktari bingwa wa kutoa huduma katika zoezi hilo, pamoja na 
wadau wengine wakiwemo NMB, CRDB, Serengeti na NBC ambao pia wameshiriki 
katika kuhakikisha  wananchi wengi zaidi wanafikiwa.
Kwa
 upande wake Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya zoezi hilo la 'Temeke
 Afya Check' na Daktari bingwa wa Kinywa na Meno Dr. Twisibilega 
Mwakasungule amesema huduma zitakazotolewa bure malipo kuanzia tarehe 9 
had 11 Setemba mwaka huu ni pamoja na magonjwa ya wanawake na uzazi, 
magonjwa ya watoto, magonjwa ya pua, koo na masikio, magonjwa ya mifupa 
na majeraha ya ajali, magonjwa ya njia ya mkojo na tezi dume, magonjwa 
ya sukari, figo, shinikizo la damu, magonjwa ya macho na uoni hafifu, 
magonjwa ya kinywa na meno, upasuaji mkubwa na mdogo pamoja na magonjwa 
ya akili.
Dr.
 Twisibilega amesema madaktari bingwa wa magonjwa hayo watakuwepo 
hospitalini hapo na watatoa huduma na ushauri wa kitaalam na kuwataka wananchi kujitokeza kupata huduma hizo 
walizosogeza karibu yao bila malipo, na wanategemea kuwahudumia wagonjwa 
wapatao 5000 ambao wataonana na madaktari bingwa na kupatiwa huduma.
Pia
 Daktari bingwa wa magonjwa ya macho na mratibu wa huduma za Tiba katika
 Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Temeke Dr.  Husna Msangi amesema huduma 
hizo zitatolewa kuanzia saa mbili na nusu asubuhi hadi saa tisa na nusu 
jioni na wateja wenye bima za afya watapokelewa na kupatiwa matibabu na 
kueleza kuwa katika katika zoezi hilo watapokea wananchi wanaotumia kadi za bima za afya ikiwemo NHIF.
Awali Daktari bingwa wa upasuaji  na 
mratibu wa zoezi hilo Dr. Kelvin Rogathe  amesema idara kwa 
kushiirikiana na wadau wamejipanga kufanya uchunguzi na kutoa matibabu 
kwa wananchi hasa katika magonjwa ya mdomo sungura kwa watoto, vichwa 
kujaa maji, majeraha yaliyotokana na moto na henia na wote watachunguzwa
 na kupatiwa huduma.
Daktari
 bingwa wa mifupa kutoka hospitali hiyo Dr. Kiandiko Liseki amesema 
wamejipanga kufanya uchunguzi na kutoa matibabu bure kwa wagonjwa wenye 
matatizo ya mifupa ikiwemo miguu kufa ganzi, majeraha ya kuvunjika, majeraha 
yaliyotokana na ajali ambapo watafanya uchunguzi, kutibu na kuunga mifupa  kwa wagonjwa ambao mifupa yao iliunga vibaya na kupelekea
 kutembea kusiko sahihi  kwa kuwafanyia upasuaji.
 
Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Temeke 
Dr. Joseph Kimaro akizungumza na Michuzi TV na kueleza kuwa, zoezi hilo kubwa la 'Temeke Afya Check'  
litafanyika katika hospitali hiyo kuanzia tarehe 9 hadi 11 Septemba 
mwaka huu na huduma za upimaji wa afya bila malipo kwa wananchi wote wa 
Temeke zitatolewa kwa kushirikiana madaktari bingwa kutoka ndani na nje 
ya hospitali ya Temeke.
 Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Temeke 
Dr. Joseph Kimaro (kulia,) akiteta jambo na Daktari bingwa wa upasuaji  na mratibu wa zoezi hilo Dr. Kelvin Rogathe (kulia,)  wakati walipozungumzaa na waandishi wa habari kuhusiana na  zoezi hilo kubwa la 'Temeke Afya Check'  
litakalofanyika katika hospitali hiyo kuanzia tarehe 9 hadi 11 Septemba 
mwaka huu na huduma za upimaji wa afya bila malipo kwa wananchi wote wa 
Temeke zitatolewa kwa kushirikiana madaktari bingwa kutoka ndani na nje 
ya hospitali ya Temeke.
 
 
 
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...