WAZIRI wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa ameelezea kuridhishwa kwake na kasi ya ujenzi wa Barabara ya Mabasi yaendayo haraka – (BRT) III na kumtaka mkandarasi Sinohydro anaejenga Barabara hiyo kuhakikisha inakamilika ifikapo Machi Mwakani.
Akizungumza alipokagua ujenzi huo Prof. Mbarawa amewataka wakazi wa Jiji la Dar es Salaam wanaotumia Barabara hiyo inayoanzia Posta ya zamani hadi Gongo la Mboto kuwa wavumilivu katika kipindi hiki ambacho ujenzi huo unaendelea.
“Nia ya Serikali ni kupunguza msongamano jijini Dar es Salaam hususan barabara hii inayokwenda katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julias Nyerere hivyo hakikisheni ujenzi unakwenda kwa haraka na ubora ili kuleta tija kwa Wananchi,” amesisitiza Prof. Mbarawa.
Aidha amewataka madereva wa magari katika barabara ambazo ujenzi wake bado unaendelea kutoa ushirikiano wa kutosha kwa wakandarasi ili kulinda usalama wa abiria, wajenzi na magari kwa
ujumla.
“…TANROADS hakikisheni magari yanaongozwa vizuri wakati wa asubuhi na jioni katika kipindi hiki ujenzi ukiendelea kwani hatuhitaji ajali zitokee hivyo tutii maelekezo ya wataalam wetu yenye nia ya kupunguza msongamano na kulinda usalama wa watu na magari,” amesisitiza Prof. Mbarawa.
Waziri huyo wa ujenzi ameitaka TANROADS kutoa kipaumbele cha ajira kwa wananchi waliojirani na mradi huo na kuwataka watakaopata kazi kuwa wazalendo kwa kuepuka vitendo vya
hujuma na wizi.
Naye Meneja wa Mradi wa BRT , Eng. Barakaeli Mmari amesema mradi huo wenye kilometa 23.3 utakuwa na vituo vidogo 32, vituo vikubwa 2 na daraja moja la waenda kwa miguu utakapokamilika na kupunguza msongamano. Aidha amesisitiza kuwa TANROADS imejipanga vizuri kumsimamia mkandarasi ili kazi hiyo ikamilike kwa wakati, ubora na kuleta tija kwa wananchi na taifa.
Kwa upande wake Meneja wa TANROADS Mkoa wa Dar es Salaam Eng. Harun Senkuku amesema wamejipanga kikamilifu kuhakikisha ujenzi wa barabara hiyo unaendana na program ya kupendezesha jiji kwa kuweka miundombinu rafiki kwa watumiaji wa barabara na yenye mvuto ili kuendana na maendeleo ya sayansi na teknolojia.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...