Mfuko wa Nishati safi ya kupikia (CookFund) Tanzania imetoa ruzuku 
yenye thamani ya Shilingi bilioni 3.2 kwa kampuni 16 zinazojishughulisha
 na utoaji wa huduma za uuzaji wa  nishati safi ya kupikia nchini kwa 
lengo la kuzisaidia kutoa huduma hizo kwa gharama nafuu na zenye ubora 
unaowanufaisha wateja wa kipato cha chini nchini Tanzania. 
Wanufaika
 hao 16 ni matokeo ya mwito wa kwanza wa maombi ya ufadhili yaliyotolewa
 mnamo Septemba 2022 kupitia program hiyo inayofadhiliwa na Umoja wa 
Ulaya (EU) ukilenga katika maeneo ya teknolojia safi ya kupikia hususani
 gesi ya ‘mitungi’ yaani Liquified Petroleum (LPG), majiko ya umeme  
(EPC) ,majiko ya mkaa banifu (ICS) mkaa tofali utokanao na vumbi la 
makaa ya mawe (briquettes) na nishati ya mafuta itokanayo na mabaki ya 
mimea (bioethanol) 
Hafla fupi ya kukabidhi hundi za fedha kwa 
wanufaika hao ilifanyika jijini Dar es Salaam katikati ya wiki hii 
ikiongozwa na Waziri wa Nishati January Makamba sambamba na Balozi wa 
Umoja wa Ulaya Manfredo Fanti, na Mkuu wa Mfuko wa Maendeleo ya Mitaji 
wa Umoja wa Mataifa (UNCDF) Tanzania Peter Malika ambaye mfuko wake ndio
 unaratibu program ya CookFund. 
Akizungumza wakati wa hafla hiyo
 Waziri Makamba aliwasisitiza wanufaika wa ruzuku hiyo kuhakikisha 
wanazitumia fedha hizo kulingana na malengo ya mpango huo ili matokeo 
mazuri ya mpango huo yaweze kuwafikia Watanzania wengi. 
“Ni 
vyema mkafahamu kuwa huu si mkopo bali ni ruzuku ambayo mnaipata moja 
kwa moja kwa jina la nchi yetu.Hivyo ni vyema mkahakikisha Watanzania 
wananufaika kweli kupitia mpango huu kwa kuwafikishia bidhaa zenu za 
nishati kwa bei nafuu ili waweze kuondokana na matumizi ya nishati chafu
 ambazo si rafiki kwa mazingira,’’ alisema 
Akizungumzia zaidi 
programu ya CookFund Waziri Makamba alisema ni moja ya suluhu la msingi 
kwa nchi katika kupambana na matumizi ya nishati chafu kwa sababu 
inawahakikishia wananchi upatikanaji wa nishati safi kwa gharama nafuu. 
Kwa
 upande wake Balozi Manfred Fanti aliwataka wafanyabiashara walionufaika
 na ruzuku hiyo kuonyesha kwamba wanaweza kuuza bidhaa zao za nishati ya
 kupikia kwa bei nafuu na kwa wateja wengi wapya kupitia msaada wa 
kifedha walioupata kupitia mpango huo 
"Umoja wa Ulaya (EU) 
unatarajia ruzuku hizi zitasaidia watumiaji wapya wa nishati ya kupikia 
hapa nchini kuweza kupata vifaa vyote vinavyohusika na mfumo mzima wa 
zana za kupikia kwa bei nafuu na zaidi tuendelea kuhamasisha watanzania 
wengi zaidi waendelee kuachana na mbinu za kupikia ambazo zinachafua na 
kuharibu mazingira". 
 "Tunatumai kushuhudia matokeo ya 
kuridhisha katika siku zijazo na kupungua kwa familia zinazotumia 
nishati ya kuni au mkaa kwa kupikia." Alisema. 
Akitoa shukurani 
zake kwa Serikali ya Tanzania na Umoja wa Ulaya, Bw. Peter Malika 
alisema kwa kuzingatia athari kubwa ya matumizi ya nishati itokanayo na 
mimea katika suala zima la mapishi nchini, ipo haja ya msingi ya 
kuongeza uwekezaji katika mnyororo wa thamani kwenye nishati safi ya 
kupikia ili kuharakisha mabadiliko kuelekea kwenye matumizi ya nishati 
safi ya kupikia. 
 “Kwa kuwa hii ni awamu ya kwanza ya maombi 
yaliyoidhinishwa  ambayo yanahusisha wanufaika 16 ambao kwa jumla 
watahudumia kaya 191,336 katika maeneo yao na kutoa ajira 191 katika 
kipindi cha miaka mitatu, tunatarajia kuzindua mwito mpya wa mapendekezo
 mwezi huu kwa hivyo kuendelea awamu nyingine ya ruzuku kwa kama hizi,’’
 alibainisha. 
CookFund ni programu ya miaka mitatu 
inayofadhiliwa na Umoja wa Ulaya (EU) chini ya Mpango wa mkakati 
jumuishi wa kutumia nishati safi ya kupikia nchini na Mfuko wa 11 wa 
Maendeleo ya Ulaya (EDF), unaolenga kuchangia dhamira ya Tanzania ya 
kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwa kuongeza  sehemu ya idadi ya 
watu na upatikanaji endelevu wa ufumbuzi wa kupikia. 
UNCDF ndiye
 taasisi msimamizi na mtekelezaji wa program ya CookFund. Mpango huu 
unalenga kushughulikia "upungufu wa mitaji" kwa upande wa watendaji wa 
sekta binafsi na changamoto ya kumudu gharama kwa watumiaji wa mwisho 
kwenye kaya. 
Programu ya CookFund inachangia vipaumbele vya 
kimkakati vya Mfumo wa Ushirikiano wa Umoja wa Mataifa nchini Tanzania 
kwa kusaidia upatikanaji bora wa nishati safi na teknolojia, usimamizi 
endelevu wa maliasili na kuongeza kasi ya kazi zenye heshima katika 
sekta rasmi.
Waziri wa Nishati January Makamba (kushoto) akizungumza na wageni waalikwa wakati hafla fupi ya kukabidhi hundi kwa kampuni 16 za nishati safi ya kupikia zilizonufaika na ruzuku kutoka Mpango wa Tanzania CookFund unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya ukilenga kusaidia kampuni hizo kutoa huduma zao kwa bei nafuu na zenye ubora unaowanufaisha wateja wa kipato cha chini katika maeneo ya vijijini na mijini kote nchini.
Balozi wa Umoja wa Ulaya Manfredo Fanti Makamba (kushoto) akizungumza na wageni waalikwa wakati hafla fupi ya kukabidhi hundi kwa kampuni 16 za nishati safi ya kupikia zilizonufaika na ruzuku kutoka Mpango wa Tanzania CookFund unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya ukilenga kusaidia kampuni hizo kutoa huduma zao kwa bei nafuu na zenye ubora unaowanufaisha wateja wa kipato cha chini katika maeneo ya vijijini na mijini kote nchini.
Mkuu wa Mfuko wa Maendeleo ya Mitaji wa Umoja wa Mataifa (UNCDF) Tanzania Peter Malika ambaye mfuko wake ndio unaratibu program ya CookFund akizungumza na wageni waalikwa wakati hafla fupi ya kukabidhi hundi kwa kampuni 16 za nishati safi ya kupikia zilizonufaika na ruzuku kutoka Mpango wa Tanzania CookFund unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya ukilenga kusaidia kampuni hizo kutoa huduma zao kwa bei nafuu na zenye ubora unaowanufaisha wateja wa kipato cha chini katika maeneo ya vijijini na mijini kote nchini.
Waziri wa Nishati January Makamba (wa tatu kushoto) akikabidhi mfano wa hundi ya fedha kwa wawakilishi wa kampuni mbalimbali za nishati safi ya kupikia zilizonufaika na ruzuku kutoka Mpango wa Tanzania CookFund unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya ukilenga kusaidia kampuni hizo kutoa huduma hizo kwa bei nafuu na zenye ubora unaowanufaisha wateja wa kipato cha chini katika maeneo ya vijijini na mijini kote nchini. Wanaoshuhudia ni pamoja na Balozi wa Umoja wa Ulaya Manfredo Fanti (Katikati), Mkuu wa Mfuko wa Maendeleo ya Mitaji wa Umoja wa Mataifa (UNCDF) Tanzania Peter Malika (wa pili kulia) na wadau wengine muhimu wa mpango huo.
Baadhi ya wageni waalikwa wakifuatilia hafla hiyo.
Waziri wa Nishati January
Makamba (katikati mstari wa nyuma) akiwa kwenye picha ya pamoja na wageni
waalikwa pamoja na wadau muhimu wa Mpango wa Tanzania CookFund wakati wa hafla
fupi ya kukabidhi mfano wa hundi ya fedha 
kwa wawakilishi wa kampuni mbalimbali za nishati safi ya kupikia
zilizonufaika na ruzuku kutoka Mpango wa Tanzania CookFund unaofadhiliwa na
Umoja wa Ulaya ukilenga kusaidia kampuni hizo kutoa huduma hizo kwa bei nafuu
na zenye ubora unaowanufaisha wateja wa kipato cha chini katika maeneo ya
vijijini na mijini kote nchini. 


 











Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...