Na Mwandishi wetu

Wananchi katika maeneo mbalimbali wameonesha kuchukizwa na kauli iliyotolewa na mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Freeman Mbowe ikionesha kuwatuhumu viongozi wa serikali kutokana na upande wanaotoka katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mbowe ametoa kauli yenye uelekeo wa tuhuma kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan na Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa katika sakata la mkataba wa uendelezaji wa bandari kati ya Serikali za Tanzania na Serikali ya Dubai Dubai kupitia kampuni ya DP WORLD.

Akiongea kupitia mtandao wa zoom jana Juni 07, 2023 kutokea nchini Ujerumani na kutoa msimamo wa awali wa chama chake kuhusu sakata la bandari alinukuliwa akisema.

"Makubaliano kati ya Serikali za Tanzania na Dubai yataleta mgogoro mkubwa kati ya wananchi wa Tanganyika au Tanzania Bara na wale wa Zanzibar na hivyo kuhatarisha muungano wetu. 


Mkataba huu (wa uendelezaji wa bandari) ulisainiwa na Prof. Mbarawa ambaye anatoka upande wa pili wa Muungano yaani Zanzibar na amekasimiwa madaraka na Rais wetu Samia Suluhu Hassan ambaye pia anatoka upande wa pili wa Muungano yaani Zanzibar huku mkataba huu ukihusu bandari za Tanganyika (Tanzania Bara) peke yake. Jambo kama hili linaweza kuwa na nia njema lakini linaweza kuzua taharuki" alisema Mbowe na kuongeza

""Katika mazingira ya mkataba huu (wa uendelezaji wa bandari) Watanganyika wana haki ya kuhisi Wazanzibari hawa wawili wanagawana mali za Tanganyika kwa wageni kwa faida zao binafsi wakati wakilinda mali zao wenyewe upande wa Zanzibar"

Miongoni mwa wanaopinga ameeleza kuwa, labda kiongozi huyo (Mbowe) amesahau kuwa hii ni Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na hivyo Mtanzania yeyote kutoka pande yoyote ya Muungano, kanda yoyote au kabila lolote ana haki ya kuwa kiongozi wa nchi na kufanya maamuzi kwa uzalendo kwa maslahi ya pande zote mbili za Muungano.

Tunu hii ya umoja tuliachiwa na waasisi wa Muungano Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Abeid Karume.

Tangu alipoingia madarakani, Rais Samia ameonesha uzalendo mkubwa wa kufungua nchi na kuongoza siasa za maridhiano na uvimilivu huku akipanua uwanja wa uhuru, haki na demokrasia.

Kwa kuhoji U-Zanzibar wa Rais na Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi kwenye mjadala wa mkataba wa DP WORLD, Mbowe amekusudia kupandikiza chuki, uhasama na mfarakano kati ya Tanzania Bara na Zanzibar ili kuligawa Taifa.

Kiongozi bora huliunganisha na kuliponya Taifa, sio kuligawa Taifa na kulirejesha kwenye siasa za chuki, uhasama na mfarakano.

Hatutakubali kutenganishwa kama taifa na kupandikizwa chuki kati ya pande zetu za Muungano na tofauti ya itikadi


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...