-Apongeza jitihada zao katika sekta za elimu, afya,maji ,kilimo
-Pia amewahimiza kuendelea kulinda maadili, kukemea maovu

Na Said Mwishehe,Michuzi TV

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan amesema Kanisa la Anglikana Tanzania ni miongoni mwa makanisa makongwe nchini na yamekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya Taifa.

Akizungumza leo Agosti 15,2023 wakati wa uzinduzi wa jengo la Kitega Uchumi la Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Centrel Tanganyika Dodoma , Rais Samia amesema Kanisa hilo hapa nchini limeanza mwaka 1927.

“Ukienda kwenye hisoria unakwenda mpaka miaka ya 18 ,40 na huko ndiko mambo haya yalianza kuchukua nafasi.Niwaambie tu kwamba lango kuu la Kanisa hili ni kule nilikokutaja Kiungani na Mkunazini Zanzibar…

“Ikachukua njia ya Mombasa ikashuka Tanga na kwingineko na ikachukua njia ya kupita Bagamoyo ikaja Dodoma na kwingineko, kwa hiyo kama nilivyosema ninyi ni ndugu zangu.

“Tangu kuingia kwake nchini Kanisa la Anglikana limefanya kazi kubwa katika kutoa huduma kwa watanzania.Kama ilivyosemwa hapa baadhi ya shule za sekondari za mwanzo kabisa zilizoanzishwa na Kanila la Anglikana ikiwemo shule ya Wasichana ya Mvumi iliyoanza mwaka 1928.

“Na Shule ya Wasichana Msalato ambayo kwa sasa inamilikiwa na Serikali. Mbali na hizo Kanisa hili lina shule nyingi za msingi, sekondari vyuo vya ufundi na vyuo vikuu kwa upande afya umejenga zahanati, vituo vya afya,hospitali na taasisi za afya ikiwemo Mvumi Health Istititute Sayansi,”amesema.

Amesema amefurahi kusikia Kanisa hilo linajihusisha na masuala ya kilimo na usalama wa chakula hasa mkoani Dodoma ambapo kuna uhaba mkubwa wa mvua.Pia wanatoa elimu ya kilimo hifadhi, kilimo bora na kusambaza mbegu bora huko vijijini.

Amesema azma ya kazi hiyo ni kuhakikisha watu wanakuwa na chakula cha kutosha na chakula salama kama ilivyoamrishwa kwenye Zaburi 145 mstari wa 15 na 16 .

“Naomba ninukuu inasema hivi macho ya wote yanakuangalia wewe nawe huwapa chakula chao kwa wakati”.

Rais Samia amesisitiza hiyo ndio kazi inayofanywa na Kanisa hilo , hiyo ni Zaburi ya 15 na 16 ambayo pia inasema “Naufungua mkono wako na kuushibisha kila kilicho hai matakwa yake.” Hiyo kazi inafanywa na Kanisa hili tunawashukuru sana.

Pia Rais Samia amemshukuru Baba Askofu kumpatia Itifaki ya Biblia sababu kuzitafuta hizo Aya na mistari kwake ni kazi kweli kweli , hivyo inabidi akeshe kwenye Biblia anatafuta vipande lakini jana amejifundisha kuna jedwali ukibonyeza inakupa zile namba za aya.

“Sasa nimefurahi kupata kitabu cha Itifaki ambacho kitaniongoza vizuri.Lakini niseme kwenye jukumu la kilimo ni jukumu kubwa mnalobeba na kwa kweli mnaisaidia sana Serikali.

“Kwani suala la kilimo na usalama wa chakula ni miongoni mwa ajenda kuu za Serikali , ndio maana tumeanza kutekeleza programu kubwa inayojulikana kama Jenga kesho iliyobora inayolenga kuhamasisha vijana kuingia kwenye shughuli za kilimo , mifugo na uvuvi

“Kwa hiyo tutaangalia jinsi ya serikali na taasisi za dini zinafanya kazi pamoja kwenye eneo hili ili vijana wengi zaidi waingie kwenye shughuli hizo.Muhimu zaidi Kanisa limekuwa likiwajali watoto wenye mahitaji maalumu…

“Ikiwemo wenye ulemavu wa aina mbalimbali , pia mmejielekeza kuwasaidia watoto yatima, wajane, masikini na wasiojiweza. Na huu ndio utumishi mwema na wito kuu wa Kanisa,”amesema Rais Samia.

Ametumia nafasi hiyo kulipongeza Kanisa Anglikana kwa ujumla na kwa kazi hiyo iliyotukuka huku akiwatia ari waendelee kutenda kazi ya Bwana kwani watalipwa kwa wakati wake na hapo kazi kubwa na hiyo inayofanyika.

Pia amewahimiza kulinda maadili na kukemea maovu , wawafundishe vijana na hata wakubwa wale ambao wanalitumia Kanisa kufanya mambo ya hovyo.“Naomba kemeaneni.”

Amefafanua kama wenyeji wao Wagogo wanavyosema kwamba tukiwatumikia watu tunamtumikia Mwenyezi Mungu , kwa hiyo waendelee na anawatia ari.

“Tumekutana hapa kusherehekea mafanikio ya Dayosisi ya Centrel Tanganyika na Kanisa Anglikana kwa ujumla kwa kufungua jengo hili la kitega uchumi ambalo ni la aina yake kwa usanifu na muonekano wake

“Nimefika hapa leo nikasema wao!!! , nimejitahidi kufanya michoro mizuri mizuri kule Magufuli City lakini hapa mmenipiga kidogo , kwa hiyo tutashirikiana na wachoraji waje watuchoree mengine ambayo yanaendelea kujengwa hapa Dodoma.

“Na kama alivyosema baba Askofu jengo hili la kitega uchumi litaongeza dayosisi kujitegemea na kutoa huduma zaidi kwa Watanzania hivyo nitumie fursa hii kutoa pongezi zangu za dhati kabisa kwa ubunifu huu mkubwa, hongereni.

“Nataka mtambue Serikali itaendelea kuenzi na kuthamini mchango wa Kanisa Anglikana Tanzania pamoja na kudumisha ushirikiano wa karibu na Kanisa hili pamoja na taasisi zote za kidini nchini,”amesema.

Ameongeza bila shaka wakifanya kazi kwa pamoja wataweza kuongeza kasi ya maendeleo kwa taifa na kuifikisha Tanzania pale inapotakiwa kuwa na kufika kuwa na Tanzania tunayoitaka

Ametoa mwito kwa Kanisa Anglikana hususani Dayosisi ya Centrel Tanganyika kuendelea kuwahimiza waumini wao kuendelea kufanya kazi kwa bidii na kuchangamkia fursa zinazotokana na kuhamishia makao makuu ya Serikali hapa Dodoma.

“Tunataka maendeleo yawe na Dayosisi hii yaende sambamba na maendeleo ya Jiji na Mkoa wetu wa Dodoma.Pia nimpongeze Baba Askofu Dk.Dickson Chilongani kwa kuandika kitabu kiitwacho Dodoma kuwa Jiji na ujio wa Serikali ,fursa na changamoto kwa wakazi na wenyeji wa Dodoma na Kanisa.

“Na imani yangu nami nitapa Copy(Nakala) lakini nanyi waumini mtakisoma vizuri ili muone changamoto na fursa zilizomo katika Serikali kuja hapa. Nikizungumzia ujio wa Serikali hapa Dodoma nadhani sote humu ndani ni mashahidi wa jinsi Jiji hili linavyobadilika siku hadi siku.

“Kuna usemi unaosemwa Roma haikujengwa kwa siku moja, hivyo hivyo Dodoma haitajengwa kwa muda mfupi lakini jitihada kwa upande wa Serikali zinaonekana.”

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Viongozi mbalimbali pamoja na Waumini wa Kanisa la Anglikana Tanzania mara baada ya kufungua Jengo la Kitega Uchumi (Safina House) la Kanisa hilo katika Sherehe zilizofanyika kwenye viwanja vya Kanisa Kuu la Roho Mtakatifu Jijini Dodoma tarehe 15 Agosti, 2023. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye Sherehe za ufunguzi wa Jengo la Kitega Uchumi (Safina House) la Kanisa hilo katika Sherehe zilizofanyika kwenye viwanja vya Kanisa Kuu la Roho Mtakatifu Jijini Dodoma tarehe 15 Agosti, 2023.

 



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya Kitabu (Itifaki ya Biblia) kutoka kwa Askofu wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Central Tanganyika (DCT) Dkt. Dickson Chilongani mara baada ya kufungua Jengo la Kitega Uchumi (Safina House) la Kanisa hilo Jijini Dodoma tarehe 15 Agosti, 2023.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akipokea kamba kama ishara ya kupokea zawadi ya Ng’ombe wa maziwa kutoka kwa Askofu wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Central Tanganyika (DCT) Dkt. Dickson Chilongani mara baada ya kufungua Jengo la Kitega Uchumi (Safina House) la Kanisa hilo Jijini Dodoma tarehe 15 Agosti, 2023

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...