Na  Said Mwishehe, Michuzi TV

NCHI za Tanzania na Uganda zimeamua kuingia makubaliano ya ushirikiano katika udhibiti wa magonjwa ya wanyama yanayovuka mipaka na yanayoambukiza binadamu kutoka kwa wanyama katika maeneo ya mipakani.

Makubaliano ya ushirikiano huo yamefanyika leo Septemba 7, 2023 kati  ya  Waziri wa Mifugo, Abdalla Ulega na Waziri wa Mifugo wa  Uganda , Bright Rwamirama wakati wa mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula Afrika(AGRF) unaoendelea jijini Dar es Salaam.

Akizungumza baada ya kuingia makubaliano hayo Waziri Ulega ameeleza kwamba  nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki zimeathiriwa na magonjwa ya wanyama yanayovuka mipaka  na yanayoambukiza binadamu kutoka kwa wanyama.

Amefafanua kuwa  uwepo wa magonjwa hayo umeathiri uzalishaji na uzalianaji wa mifugo, afya ya jamii, usalama wa chakula , uhifadhi wa wanyamapori , utalii na biashara ya mifugo na mazao yake.

Ameongeza ni muhimu kuwepo kwa mkataba wa makubaliano utakaowezesha ushirikiano wa pamoja katika kupanga na kutekeleza mikakati ya kudhibiti  magonjwa yanayovuka mipaka na yanayoambukiza  binadamu kutoka kwa wanyama.

Ametumia nafasi hiyo kutaja baadhi ya magonjwa yanayovuka mipaka  ni homa ya mapafu ya ng'ombe,nguruwe  mbuzi, sotoka ya mbuzi na kondoo, kideli, ugonjwa wa miguu, midomo na mapele ya ngozi.

Wakati kwa magonjwa yanayovuka mipaka na kuambukiza binadamu ni  Ebola,  Marburg,  homa ya bonde la ufa, na homa nyingine zinazoambatana na damu kuvilia mwilini, mafua makali ya ndege na kimeta.

"Katika mpaka wa Tanzania na Uganda kumekuwa na mwingiliano mkubwa wa mifugo, wanyamapori na mazao ya wanyama  jambo ambalo limekuwa likihatarisha  kusambaa kwa magonjwa ya wanyama  kwa kila upande," ameeleza Waziri Ulega.

Akielezea zaidi maeneo  ya ushirikiano baina ya nchi hizo ni kufanya utaratibu, utambuzi na udhibiti wa wanyama , kuendeleza miundombinu ya mifugo iliyopo mipakani na rasilimali watu na  kitumia teknolojia za kisasa.

Pia kuna mipango ya pamoja ya utafiti na udhibiti wa magonjwa hayo na maeneo mengine kulingana kama yatakavyokubaliwa na kamati ya pamoja na wataalamu.

 Pamoja na hayo amewataka wakurugenzi wa mifugo wa nchi za Tanzania na Uganda wahakikishe wanachukua hatua na kalenda zao ziwe zinawiana katika uchanjaji.

Kwa upande wakeWaziri wa Mifugo wa  Uganda Bright Rwamirama baada ya kuingia makubaliano ya ushirikiano huo amesema makubaliano hayo yataleta tija kwa pande zote  mbili.

Amesisitiza kupitia ushirikiano huo sekta ya mifugo watahakikisha inakuwa na tija kwa wafugaji wa nchi hizo katika harakati za kukuza uchumi.

Ameongeza kwamba silimia 70 ya magonjwa ya binadamu yanatokana na mifugo hivyo lazima kuwepo na mikakati  madhubuti ya kuhakikisha magonjwa hayo yanadhibitiwa.




Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...