Na Mwandishi Wetu

SHIRIKISHO la Wenye Viwanda nchini (CTI), limesema wafanyabiashara wa Tanzania wanapaswa kuachana na kawaida ya kuuza nje ya nchi malighafi na badala yake wapeleke bidhaa zilizoongezewa thamani.

Hayo yalisemwa jana na Mwenyekiti wa shirikisho hilo, Paul Makanza wakati wakati mkutano wa sekta binafsi ya Marekani na Tanzania uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Mkutano huo ulioandaliwa na Shirikisho la Wenye Viwanda nchini (CTI) na Shirikisho la Wafanyabiashara wa Marekani Afrika Cooperate Council of Africa (CCA).

Alisema bado Tanzania haijalitumia vyema soko kubwa la Marekani kwani imekua ikipeleka malighafi nyingi hasa mazao ya kilimo na madini mbalimbali badala ya kupeleka bidhaa zilizoongezewa thamani.

“Hatupaswi kupeleka malighafi nchini Marekani na tumejadili fursa zilizopo kwenye mpango wa AGOA kwa sasa kuna kampuni kama mbili tu zinapeleka nguo kwenye soko hili kwa hiyo tumejadili namna ya kuongeza ushiriki wa wafanyabaishara,” alisema
Makanza alisema CTI imekuwa na ushirikiano wa siku nyingi na Shirikisho la Wafanyabiashara wa Marekani kwa lengo la kukuza biashara na uhusiano kati ya Marekani na Tanzania.

Alisema mkutano huo umejadili namna ambavyo wenye viwanda nchini wanaweza kupenya kwenye soko la Marekani na wafanyabiashara wa Marekani wanavyoweza kutumia fursa ya soko la bidhaa mbalimbali nchini Tanzania.

“Tumejadiliana namna ambavyo bidhaa za Marekani zinaweza kuja kirahisi kwenye soko la Tanzania na namna wafanyabiashara wa Marekani wanavyoweza kuja kuwekeza kwenye kutengeneza bidhaa zao hapahapa nchini kwa kuziongezea thamani,” alisema

Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Dk. Elsie Kanza, alisema kuna umuhimu wa kuwapa wafanyabiashara taarifa kuhusu bidhaa zinazotakiwa nchini Marekani na kuzitengeneza kwa kuzingatia viwango vitakavyokubaliwa kwenye soko hilo.

“Soko la Marekani ni kubwa sana lakini wafanyabaishara wengi wanashindwa kufikia viwango vinavyotakiwa na siyo tu Tanzania wafanyabiashara wa nchi nyingi za Afrika wamekuwa wakishindwa kuvifikia,” alisema

Balozi alisema katika mkutano maalum wa AGOA uliofanyika kwa siku nne nchini Afrika Kusini wamekubaliana kuwawezesha wafanyabiashara wa mataifa ya Afrika ili waweze kufikia viwango vinavyotakiwa ili waweze kunufaika na fursa ya soko hilo.

“Kwenye mkutano huu tumezungumza sana na kupokea hoja za sekta binafsi ya Marekani na sekta binafsi ya Tanzania ili kuhakikisha tunashirikinana kukuza mauzo ya Tanzania kwenda Marekani na mauzo ya Marekani kuja Tanzania,” alisema

Naye Balozi wa Marekani nchini Tanzania, Michael Battle, alisema serikali inapaswa kutengeneza sekta binafsi imara ili kufikia maendeleo makubwa ya biashara na ujenzi wa viwanda vingi vitakavyoongeza kasi ya ukuaji wa uchumi na kuongeza ajira.

Amesema ushirikiano wa muda mrefu wa kibiashara baina ya sekta binafsi ya Marekani na ya Tanzania umekuwa nguzo muhimu katika maendeleo ya biashara na ukuaaji wa uchumi baina ya nchi hizo mbili.

Alisema sekta binafsi imara imekuwa msingi mkubwa wa ukuaji wa uchumi kwenye mataifa mengi yaliyoendelea na imekuwa ikisaidia kutengeneza fursa nyingi za ajira zinazosaidia kuwaondoa wananchi kwenye lindi la umaskini na kuwa katika tabaka la kati.

Alisema kama serikali inataka kufikia malengo yake kwa njia nyepesi inapaswa kuendelea kuiwekea mazingira mazuri kuiimarisha sekta binafsi kwani ndiyo yenye uwezo wa kutengeneza fursa nyingi za ajira na kuchangamsha uchumi wa nchi.

Kuhusu Mpango wa Ukuaji na Fursa wa Afrika uliotolewa na Marekani AGOA, Balozi Michael alisema mpango huo umekuwa na manufaa makubwa kwa ukuaji wa uchumi wa mataifa mengi ya Afrika na vyama vyote vikubwa vya Republican na Democrat vimekuwa vikiuunga mkono muda wote.

Alisema hata Rais wa Marekani Joe Biden anaunga mkono mpango huo ambao anaamini utaendelea kutoa mchango mkubwa kwa maendeleo ya nchi za Afrika.

“Rais wa Marekani Jose Biden anaunga mkono AGOA, Bunge la Marekani linaunga mkono mpango huu na bila shaka mnaweza kushuhudia ambavyo umekuwa mkombozi kwa bidhaa za nchi nyingi kuingia kwenye soko la Marekani,” alisema Balozi.

“Mjadala huu wa unaonyesha namna nchi zote mbili zinavyojali uhusiano wa kibiashara kwasababu kuna fursa nyingi za kibiashara baina yetu na tuna wajibu wa kuendeleza uhusiano huu kwa maslahi ya watu wetu,” alisema

Mkurugenzi Mkuu wa (CTI), Leodegar Tenga alisema mkutano ulikwenda vizuri na wameazimia kuendeleza ushirikiano uliopo kwa kuwa karibu na kufahamu wafanyabiashara wa Marekani wana kitu gani na wenzao wa Tanzania wana nini.

“Soko la Marekani ni kubwa mno, nisisi tu ambao tunaweza kutumia hiyo nafasi kukuza uchumi wetu na jana wamarekani walituambia kwamba chini ya mpango wa AGOA bado hatujanufaika sana na nchi zote za Afrika chini ya mpango huu tunauza Dola milioni 4 tu kwa mwaka wakati Bangladesh peke yake inauza Marekani Dola milioni 38 kwa mwaka,” alisema

 Mkurugenzi wa Shirikisho la Wenye Viwanda CTI, Leodegar Tenga akizungumza kwenye mjadala baina ya wafanyabiashara wa Marekani na Tanzania jana jijini Dar es Salaam.

Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Dk Elsie Kanza akizungumza kwenye mjadala baina yaa wafanyabiashara wa Marekani na Tanzania ulioandaliwa na CTI
 

Balozi wa Marekani Michael Battle akiwa kwenye mkutano huo


Sehemu ya washiriki wa mkutano baina ya wafanyabiashara wa Marekani na Tanzania ulioandaliwa na CTI

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...