Na. WAF - Tanga

Watumishi wawili wakutwa na tuhuma za kujibu kwenye kifo cha Bi. Mariam Zahoro mkazi wa Kijiji cha Mumbwi katika Wilaya ya Handeni kilichotokea kwenye Kituo cha Afya Kabuku, Mkoa wa Tanga.

Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu amesema hayo leo baada ya kupokea taarifa ya uchunguzi wa kifo cha mama mjamzito na kichanga chake katika kituo cha Afya Kabuku Halmashauri ya Wilaya ya Handeni Mkoani Tanga. 

“Serikali imepokea mapendekezo ya kamati iliyoundwa na tayari tumeanza kufanyiwa kazi ikiwa ni pamoja na Baraza la Madaktari Tanganyika (MCT) kutoa notisi ya kumtaka Daktari kujibu tuhuma zinazomkabili pamoja na Baraza la Uuguzi na Ukunga Tanzania (TNMC) kutoa notisi kwa Muuguzi na kutakiwa kujibu tuhuma hizi ndani ya siku 14 kuanzia leo.” Amesema Waziri Ummy 

Waziri Ummy wakati akifafanua taarifa hiyo amesema kuwa Watumishi hao wawili ambao ni Daktari wa zamu namba 2 (Dkt xxx) na Muuguzi wa kutoa huduma za usingizi xxx kushindwa kuzingatia maadili na weledi wa taaluma zao katika kumuhudumia mgonnjwa huyu. 

“Kamati imebaini kuwa Daktari wa zamu namba 2 alishindwa kufika kwa wakati kutoa huduma za dharura licha ya kupewa taarifa mara kwa mara ya kutakiwa kufika Kituoni kutoa huduma ya dharura kwa mgonjwa huyu.” Amesema Waziri Ummy


Amesema, Daktari huyu licha ya kufika Kituoni kwa kuchelewa bado alishindwa kutimiza wajibu wake wa kitaaluma ikiwemo kutoa rufaa kwa mgonjwa kwenda kuhudumiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Handeni (ambayo ipo takribani kilometa kutoka Kituo cha Afya Kabuku) baada ya mtaalamu wa usingizi kutopatikana kwenye simu na hivyo mgonjwa kutofanyiwa upasuaji kwa wakati. 

“Kamati imebaini kuwa Daktari huyu alishindwa kutoa Taarifa ya dharura hii kwa Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya au Mganga Mkuu wa Halmashauri ili wawezi kuchukua hatua za haraka kwa ajili ya kuokoa maisha ya mama huyu.” Amesema Waziri Ummy 

Aidha Kamati imebaini ukiukwaji wa Maadili kwa Muuguzi xxx mwenye utaalamu wa kutoa huduma ya dawa ya usingizi ambapo imepelekea kutakiwa kutoa maelezo ndani ya siku 14. 

Aidha, Waziri Ummy amepiga Marufuku kwa Viongozi na wataalamu kufanya maamuzi ya kuwatoza fedha wananchi kupitia vikao vya makubaliano pasi na kuwashirikisha wananchi kutokana na Majibu ya taarifa ya Uchunguzi kuonyesha kuwa yaliweka makubaliano  kuwatoza wajawazito gharama hizo za Shilingi laki na nusu kwa watakojifungua kwa Upasuaji.

"Kifo cha Bi. MARIAMU ZAHORO kingeweza kuepukika kutokana na taarifa iliyotolewa, tusubiri majibu ndani ya hizo siku 14 lakini kwa sasa hawatarudi kazini hii iwe funzo na onyo kwa wengine.” Amesema Waziri Ummy.






Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...