Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma

Makamu wa Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ametoa Maagizo 10 kwa Wizara ikiwemo Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Fedha,Wizara ya Kilimo,Ofisi ya Raisi Tamisemi,Wizara ya mambo ya nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Vyuo vya mafunzo ya nyuki ikiwemo chuo cha kilimo SUA,Wananchi na Vyombo vya habari Nchini kuhakikisha wanasimamia ukuaji wa sekta ya ufugaji nyuki.

Wakati huo huo Dkt. Philip Mpango ametoa Rai kwa wote wenye dhamana ya kusimamia maeneo yaliohifadhiwa kulinda na kuendeleza ipasavyo maeneo hayo ili yasiharibiwe kutokana na shughuli mbalimbali za kibinadamu.

Makamu wa Rais ametoa rai hiyo leo May 20,2024 katika Hotuba yake kwenye Maadhimisho ya Siku ya Nyuki Duniani yaliyofanyika Kitaifa Jijini Dodoma.

Na kuongeza kuwa Utunzaji wa maeneo hayo ni lazima uende sambamba na utaratibu utakaowezesha wananchi kufuga nyuki na kujipatia kipato huku wakitunza mazingira.

Ameitaka Wizara ya Maliasili na Utalii kushirikiana na Wadau katika kutoa elimu kwa wafugaji nyuki ili waweze kufuga kitaalam kwa kutumia vifaa sahihi vitakavyoongeza kiwango cha uzalishaji na ufugaji wa tija.

"Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kushirikiana na wadau wengine ianze sasa utekelezaji wa mipa go ya kuendeleza sekta ya ufugaji nyuki ambao tumezindua leo".

Makamu wa Rais ameilekeza Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais – TAMISEMI kuyatambua na kuyahifadhi kisheria maeneo yote yaliyobaki yenye uoto uliotawaliwa na mimea ya aina mbalimbali inayotoa chakula kwa nyuki hususani katika Mikoa ya Dodoma na Singida.

Amesema Uoto huo umetawaliwa na mimea jamii ya Mndarambwe na Mnang’ana ambao unakadiriwa kuwa kwenye eneo lenye ukubwa wa hekta 410,000 na taarifa zilizopo zinaonesha kuwa uoto huo hupatikana katika nchi mbili tu hapa duniani, yaani Tanzania na Zambia, huku sehemu kubwa ya uoto huu ikiwa Tanzania katika mikoa ya Singida na Dodoma. Aidha amesema wananchi waliopo kwenye maeneo hayo waelimishwe kuhusu ufugaji nyuki kibiashara na utunzaji wa mazingira.

Vilevile Makamu wa Rais ametoa wito kwa Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia TFS na Mfuko wa Misitu kuhakikisha wanawawezesha Wananchi hasa wale wanaopakana na maeneo ya hifadhi kwa kuwapatia mafunzo ya ufugaji nyuki pamoja na mizinga ya kisasa ya kufugia nyuki.

"Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia TFS na Mfuko wa Misitu hakikisheni mna wawezesha wananchi hasa wale wanapaka na hifadhi kwa kuwapatia mafunzo ya ufugaji nyuki pamoja na mizinga ya kisasa ya kufugia".

Pia amesema TAMISEMI inapaswa kuhakikisha kuwa Halmashauri hasa zenye fursa kubwa ya ufugaji nyuki zinaajiri Wataalam wa ufugaji nyuki watakaotumika kwenda kutoa huduma ya ugani kwa wananchi.

"Ofisi ya Raisi Tamisemi muhakikishe Halmashauri na hasa zenye fursa kubwa ya ufugaji nyuki zinaajiri wataalamu wa ufugaji nyuki watakao tumika kwenda kutoa huduma ya ugani kwa wananchi ".

Halikadhalika ameziasa Balozi za Tanzania nje ya Nchi kujidhatiti katika kutafuta masoko ya mazao ya nyuki yanayozalishwa nchini ili kuweza kuongeza fedha za kigeni. Amesema Wizara ya Fedha iangalie uwekezano wa kupunguza kodi katika vifaa mbalimbali vya kuchakata mazao ya nyuki kama njia ya kuhamasisha uongezaji thamani ya mazao ya nyuki na kukuza mauzo nje ya nchi.Aidha Makamu wa Rais amesema Vyuo vya Veta vilivyopo katika maeneo ya vijijini ni muhimu kuwa na programu za ufugaji na uchakaji wa mazao ya nyuki.

Ameongeza kwamba Vyuo vya Elimu ya Nyuki na Vyuo Vikuu ni vema kuwatumia wajasiriamali waliofanikiwa katika sekta ya ufugaji nyuki kutoa elimu katika vyuo hivyo ili kuwa hamasa kwa vijana waliopo vyuoni.

Kwa upande wake Waziri wa Maliasili na Utalii Angellah Kairuki amesema Wizara itaendelea kuongeza ufugaji nyuki na kuhakikisha uzalishaji wa asali unaongezeka kutoka tani 32671 za sasa hadi kufikia uzalishaji usiopungua tani 138000 ifikapo 2034.

Amesema Wizara itaongeza uzalishaji wa Chavua, kuhamasisha na kuongeza idadi ya mizinga, kuongeza uzalishaji wa asali ya nyuki wasiodunga, kuongeza thamani ya aina sita za mazao ya nyuki kwa kutumia mazao mengine kama sumu ya nyuki na gundi ya nyuki. Aidha amesema Wizara itawajengea uwezo wa wataalamu ili waweze kufanya kazi zaidi pamoja na kutenga fedha na kuhakikisha vitendea kazi na miundombinu vinaimarishwa katika maeneo ya kufugia nyuki.

Naye Waziri Ofisi ya Makamu wa Raisi Muungano na Mazingira Dkt Suleiman Jafo amewaomba Watanzania wote kuhakikisha ajenda ya utunzaji wa mazingira inwekwa msingi mzuri katika sekta ya nyuki.

"Naishukuru sana Wizara ya Maliasili na Utalii pamoja na Wakala wa misitu Tanzania TFS imesaidia sana katika ajenda ya kupanda miti katika kuhakikisha wanapata sehemu salama ya akufanya uzalishaji wao".

"Niwaombe sana Watanzania wote kuhakikisha ajenda ya utunzaji mazingira inawekwa kama msingi katika sekta ya nyuki Nchini.

Kilele cha Maadhimisho haya kiliongozwa na kauli mbiu inayosema :Nyuki kwa Afya na Maendeleo, Tuwatunze #Apimondio 2027 Tanzania ipo tayari.





Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...