NA K-VIS BLOG/KHALFAN SAID, MVOMERO
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Mhe. Deogratius Ndejembi, amesema ni matarajio ya Serikali kuona uzalishaji katika kiwanda cha sukari cha Mtibwa unarejea kwa haraka.
Mhe. Ndejembi ametoa kauli hiyo hivi
karibuni alipofika katika kiwanda hicho ili kujionea mwenyewe hali halisi
iliyopelekea ajali ya kupasuka kwa bomba la kusafirisha mvuke (steam) iliyotokea
Mei 23, 2024 na kusababisha wafanyakazi 11 kufariki papo hapo na wengine wawili
kufariki baadaye wakiwa wanapatiwa matibabu hospitalini.
Amesema “Uzalishaji ukirejea haraka
maana yake wafanyakazi watarudi kufanya kazi, wakulima watauza miwa yao kiwandani
na hivyo mtazalisha na sukari itapatikana sokoni”.
Mhe. Ndejembi ameelekeza uchunguzi wa
kina wa ajali hiyo ukamilike haraka ili tupate taarifa ya kitaalamu itakayo saidia
kutumika kwa njia salama zaidi na kuepuka ajali
Ametoa pole kwa wote walio poteza wapendwa
wao na kuwahakikishia, kuwa Serikali kupitia Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi
(WCF) uko bega kwa bega na uongozi wa kiwanda tangu ajali ilipotokea ili
kuhakikisha familia zote zilizo poteza wapendwa wao wanapatiwa fidia stahiki na
kwa wakati. “Mmeona umuhimu wa kujisaji
WCF? Ni kwamba ajali zikitokea kutokana na kazi basi Serikali inalipa fidia
wahusika kupitia WCF.” Mhe. Waziri ameuhakikishia Uongozi wa Kiwanda.
Aidha Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dkt.
John Mduma ambaye naye alikuwepo kwenye ziara hiyo, alisema tayari timu ya
wataalamu kutoka Mfuko huo imeanza mchakato wa kuwezesha wategemezi wa wafiwa kupata
fidia kwa mujibu wa sheria.
“Baada ya tukio la ajali kujulikana
tulituma timu yetu maramoja kutokea ofisi yetu ya Morogoro na kufika kiwandani
na tayari imekwsiha chukua taarifa za awali ili kuwatambua walengwa na kuanza
kuchakata fidia kwa wale walioachwa - wawe ni wenza au watoto.” Amebainisha
Dkt. Mduma
Naye Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya
Usalama na Afya mahali pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda amesema uchunguzi wa
awali umeonyesha kuwa ubadilishaji wa mfumo wa kusafirisha mvuke ndio
uliopelekea tatizo hilo. Hata hivyo
alisisitiza kwamba chanzo halisi cha ajali kitajulikana hapo uchunguzi
utakapomalizika.
Aidha mmiliki wa kiwanda hicho Bw.
Nassor Ali Seif, amesema tayari kiwanda kimeanza kuchukua hatua mbalimbali za
muda mfupi na kuanza mipango ya muda mrefu ili kuhakikisha kwamba tukio kama
hilo halijitokezi tena.
Mhe. Ndejembi akiwa na mmiliki wa kiwanda, Bw. Nassor Ali Seif, wakati akiangalia uharibifu uliotokana na ajali hiyo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...